WASOMI
mbalimbali wameinesha kushangazwa kwao na tabia ya Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha mapinduzi(CCM)
Bara, kutumika kama Mkuu wa Upelezi wa
Makosa ya Jinai(DCI) na Mwendesha Mashataka Mkuu(DPP) ambako amekuwa akitoa maneno na video mbalimbali kama njia
mojawapo ya kutaka kuhalalisha matukio yaliyofanywa na wanachama wa upinzani.
Hayo
yalisemwa jana na Mhadhiri wa Sheria kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam,
Onesmo Kyauke, wakati alipokuwa akichokoza mada kwenye kongamano la kuangalia
mustakabali wa nchi, lililoandaliwa na Wanazuoni wa Chuo Kikuu cha Dar es
Salaam(UDASA).
Akitolea
mfano wa matukio ambayo Nchemba amekuwa akiyafanya ni pamoja na lile la
kuonesha ushiriki wa kupanga tukio la ugaidi la Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama
wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo(Chadema), Wilfred Lwakatare.
Tukio
lingine Kyauke alisema ni la wakati wa kampeni za uchaguzi wa udiwani Jijini
Arusha, ambako kiongozi huyo aliwataka wananchi wa Jiji hilo kutochagua
madiwani wa Chadema kwa kuwa ni chama cha ugaidi kwa madai kwamba ndio
waliohusika kummwagia tindikali kijana wa Igunga.
Kutokana
na matamshi hayo, Mhadhiri huyu alisema
baadhi ya wanachama wa Chadema waliweza kukamatwa kama njia mojawapo ya
kuisaidia polisi jambo linalowafanya kama wasomi kujiuliza kuwa Mwigulu siku
hizi kawa DCI au DDP?
Akizungumzia
kuhusu utendaji wa Jeshi la Polisi, alisema ndilo limekuwa chanzo kikubwa cha
uvunjifu wa amani kwa kupoka haki ya kikatiba ya wananchi kuandamana na kufanya
mikutano huku akitolea mfano wa mauaji waliyoyafaya ya Mwandishi wa habari
Daudi Mwangosi Kijijini Nyororo Mkoani Iringa
wakati wa kuzindua matawi ya Chadema.
Katika
mauaji hayo, alisema ushahidi wa wazi umeonesha namna gani Plisi walivyoshiriki
na tume zote zilizoundwa zikaelekezea kidole Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa
Iringa na Msajili wa Vyama vya Siasa, lakini hakuna hatua zilizochukuliwa hadi
leo zaidi ya polisi mwenye cheo kidogo akitolewa kafara huku mkubwa wake
akiendelea kupandishwa cheo.
Pia
alisema kumekuwepo na upendeleo wa Jeshi hilo wa kutetea chama tawala ikiwemo
enzi za Mahita kudai kuwashilikilia wanachama wa Chama cha Wananchi (CUF) na
majambia ambako hadi leo wamekosa uthibitisho ambako kutokana na uongo huo
wameshindwa kumchukulia hatua kiongozi huyo.
Katika
mapendekezo yake, Kyauke aliitaka Polisi
kubadili mfumo wake wa kufanya kazi, Waziri Nchimbi aeleze ni kwa nini Tanzania
ni dhambi kuandamana, Waziri Mkuu kufuta kauli yake ya kutaka wanachi kupigwa
tu na Jeshi hilo na wanasaiasa kubadilika katika kufanya siasa zao ambalo wengi
wa sasa hivi wamekuwa wakitanguliza matusi katika kueneza propaganda zao.
Kwa
upande wake Benadetha Kilya, ambaye ni
Mtaalam wa Sayansi ya Siasa na Utawala
kwa Umma, alisema mpaka sasa bado kiini cha uvunjifu wa amani hakijagundulika
na badala yake pande zote zimekuwa zikirushiana mpira ikiwemo Serikali,
wananchi na wanasiasa.
Kilya
alizitaja sababu zinazochangia matukio hayo kuwa ni pamoja na hali ya upinzani
kuja juu hivyo chama tawala kinajihami
kutokana na mabadiliko hayo, nyingine ni kuongezeka kwa kiwango cha umasikini
na mfumo wa kiliberali ambao umechangia
matabaka, uhuru wa kutoa maoni tofauti na enzi za ujamaa.
Ayoub Rioba, Mhadhiri wa Chuo cha Uandishi wa
habari katika masomo ya Habari na Mawasiliano kwa Umma, alisema suala la amani
sio la kuombewa bali ni la kisayansi zaidi
na kudai kwamba wanasiasa wamekuwa wakijidanganya pale wanapowahimiza
watu kuliombea taifa hili amani.
Pia
Rioba alikanusha kwamba vyombo vya habari vimekuwa vikichangia kuharibu amani
na badala yake alivifananisha vyombo hivyo na bunduki ambako kama isipotumiwa
kamwe haiwezi kuharibu amani.
Akifafanua
hili alisema vyombo vya habari vitaharibu amani endapo tu wanasiasa watavitumia
na kuitaka jamii ielewe kwamba vyombo hivyo
vina dhima kubwa kama mlinzi wa Taifa na ndio maana wakati mwingine
vinapendekezwa kuwa NGO’s ili viweze kufanya kazi kwa uhuru zaidi.
Wito
wake kwa vyombo vya habari, Rioba alivitaka kujua histiroa ya nchi kuanzia enzi za utumwa, kujua dhima ya vyombo vya habari, sheria za vyama vingi,
kujua katiba za vyama kuwa karibu na wananchi na kuepuka kuwa mashabiki wa
migogoro.
Vile
vile aliwataka wanahabari kuwa makini katika kutoa fursa kwa pande zote mbili
zenye migogorokuwa na tabia ya kuuliza maswali ya kutafuta suluhu badala ya
kuchochea na kuchimba na kuchunguza zaidi kuhusu kiini cha mgogoro badala ya
kudandia hoja.
Akichangia
hoja katika mdahalo huo Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo
(Chadema) Dk Slaa alisema mchawi wa hayo yote ni serikali, huku akinukuu ripoti
ya tume ya haki na utawala bora iliyomtuhumu aliyekuwa kamanda wa polisi wa
mkoa wa Iringa, Michael Kamuhanda na Msajili wa vyama vya siasa. Dk Slaa
alisema Amani sio suala la kuhubiriwa au kujadiliwa, amani ni matokeo ya
utekelezaji wa haki mbalimbali.
Dk
Slaa pia alilalamikia vitendo vya ukatili vilivyofanywa Mtwara na vyombo vya
dola dhidi ya wananchi, huku akimnyooshea kidole Brigedia Elia Athanasi
aliyekuwa amemwakilisha Mkuu wa majeshi, Dk Slaa alisema “jeshi letu lilikuwa
linaheshimika sana, lakini siku za hivi karibuni linaelekea kupoteza heshima
yake kwa jamii, tukirejea mfano katika uchaguzi Mkuu uliopita ambapo mnadhimu
wa jeshi Abdulrahman Shimbo alivyotoa kauli yenye utata, jeshi linaingiaje
kwenye siasa wakati suala la uchaguzi ni suala la kiraia? Alihoji Dk Slaa
Hoja
ya Dk Slaa kuhusu utendaji wa jeshi la wananchi Mkoani Mtwara ilipingwa kwa
haraka na Brigedia Athanasi akisema “naomba kuweka wazi kuwa jeshi letu lipo
Mtwara, lina adabu na vitendo ambavyo vimekuwa vikiripotiwa ni vya propaganda
tu kama alivyosema Dk Slaa”.
Licha
ya Mwanajeshi huyo kujitetea, mchangiaji
aliyefuata alikuwa ni Julisu Mtatiro, Naibu Katibu Mkuu Bara wa Chama cha
Wananchi (CUF), aliyethibitisha kuwa wanajeshi wanabaka na walitenda vitendo
vya kikatili dhidi ya raia na viongozi wa CUF akiwemo Mkurugenzi wa Chama hicho
kutoka makao makuu Shaweji Mketo.
NCCR WAJITETEA.
Akichangia
mjadala huo, Katibu Mkuu wa NCCR Mageuzi alisema kwanza Chama chake hakipo
tayari kufanya maandamano, na kwamba Chama chake kimeamua kupambana kwa nguvu
ya hoja, na wataendelea kutumia nguvu ya hoja kama walivyomtuma Mbatia
akapeleka hoja ya Elimu Bungeni na wakaungwa mkono na watanzania wengi.
Akihitimisha
kongamano hilo la Amani, Wazri wa Mambo ya ndani Dk Emmanuel Nchimbi alisema
kuwa kati ya mambo ambayo yanayompa
changamoto ni amani ya nchi hii. Alisema kuwa tulirithi nchi ikiwa na amani,
hivyo tuna deni la kurithisha nchi hii ikiwa ya amani katika kizazi kijacho.
Dk
Nchimbi alikemea suala la udini, akitahadharisha watanzania kuwa wasiingie
katika vurugu na wasikubali kugawanywa kwa sababu ya dini zao. “Tukiingia
katika vurugu za dini hatutapona, Wakristo na waislam wote tukatae kugawanywa
kwa kutumia misingi ya udini kwa manufaa ya Tanzania ya sasa na kizazi kijacho.
Kwa
upande wa siasa, Waziri Nchimbi, huku akimtambua Katibu Mkuu wa Chadema Dk
Slaa, alisema wanasiasa wote wana wajibu wa kuwatumikia wananchi, “Suala la
amani sio suala la chama cha Mapinduzi peke yake, ni suala la wanasiasa wote wa
Chama tawala na wapinzani kutambua kuwa wao ni watumishi wa umma, na
kuvumiliana kisiasa ndio kunaleta amani.
Kuhusu
vyombo vya dola kutumika vibaya Dk Nchimbi aliwatetea polisi, na kusema kuwa
kuna sehemu ambazo pia polisi wanakosea na wanawajibishwa, huku akitaja takwimu
za askari waliowajibishwa kwa mwaka 2012 kuwa Askari 106 wamefukuzwa kazi,
Maafisa 6 wa polisi wamesimamishwa na 95 walifukuzwa Chuo cha Polisi kilichopo
Moshi waliojiunga kinyume cha utaratibu. Dk Nchimbi alikwepa kuzungumzia suala
la mauaji ya Arusha, Morogoro na Iringa ambapo wakati wa mjadala yalijitokeza
sana kuhoji uadilifu wa polisi, hasa aliyekuwa kamanda wa Polisi wa mkoa wa Iringa aliyevunja
sheria na kusababisha kifo cha Mwandishi wa habari Daud Mwangosi
Hakimu ashinda
kesi ya rushwa
Na Happiness
Katabazi
MAHAKAMA ya
Hakimu Mkazi Ilala, jijini Dar es Salaam, imemwachia huru Hakimu wa mahakama
hiyo, Pamela Kalala, aliyekuwa akikabiliwa na makosa mawili ya kuomba na
kupokea rushwa ya sh 100,000 kwa njia ya simu.
Uamuzi huo
ulitolewa jana asubuhi na Hakimu Mkazi, Alocye Katemana, ambaye alisema kwa
mujibu wa vielelezo na ushahidi wa mashahidi saba wa upande wa Jamhuri katika kesi hiyo, mahakama yake
imeona upande wa Jamhuri umeshindwa kuthibitisha kesi yake.
Hakimu Katemana
alisema kwa mujibu wa hati ya mashtaka inaonesha Taasisi ya Kuzuia na Kupambana
na Rushwa, walidai kuwa Kalala aliomba na kupokea rushwa kutoka kwa Josephine
Wage, ambaye ni mke wa mshitakiwa, Abubakar Mzirai ambapo Kalala alikuwa
akisikiliza kesi ya jinai inayomkabili Mzirai ili amfutie kesi.
‘Lakini mimi
nimeyasoma malalamiko yaliyoandikwa na Joseph kuhusu Kalala na nimebaini katika
malalamiko yake, Josephine alikuwa akilalalamika kuwa Hakimu Kalala alipomfutia
dhamana mumewe (Mzirai), hakutaja sababu,” alisema.
Alisema kuwa
Josephine alilalamikia mwenendo wa kesi lakini hakuna mahala popote
alipolalamika kuwa Kalala alimuomba au kumpatia rushwa.
Alisema kuwa
alibaini ni kweli Hakimu Kalala alishindwa kuandika sababu za kumfutia dhamana
mshitakiwa licha ya sababu hiyo kutoweza kuishawishi mahakama hiyo imuone
mshitakiwa ana kesi ya kujibu.
“Na kwa sababu
hiyo mahakama hii inamuachilia huru kwa vile upande wa Jamhuri umeshindwa
kuthibitisha mashitaka hayo ya rushwa dhidi ya Hakimu Kalala,” alisema
Katemana.
Awali ilidaiwa na Wakili wa Serikali, Kasamala
kwamba Pamela akiwa mwajiriwa wa Mahakama, kama Hakimu Mkazi na wakala wa
sheria ya Takukuru, alikiuka kifungu namba 11 cha sheria ya mwaka 2007 kwa
kuomba rushwa kutoka kwa Josephine Wage.
Kasamala alidai
Pamela alitenda kosa hilo ili kumshawishi kutoa uamuzi wa kumpendelea mumewe.
Katika shtaka la pili, Hakimu Mkazi Pamela anadaiwa kuwa Februari 2, mwaka huu,
eneo la Manispaa ya Ilala, akiwa na wadhifa huo, alipokea sh 800,000 kutoka kwa
Josephine.
Pia anadaiwa
kuwa Februari 6, mwaka huu, katika eneo
hilo, alipokea tena sh 100,000 kutoka kwa Josephine.
Hiyo si mara ya
kwanza kwa mahakimu kufikishwa mahakamani hapo kwa makosa ya kuomba na kupokea
rushwa.
Aliyekuwa Hakimu
wa Mahakama ya Wilaya ya Temeke, Jamila Nzota, alifikishwa katika mahakama hiyo
na mwaka 2010 alitiwa hatiani kwa makosa hayo na kufungwa jela miaka mitatu.
Mwisho
No comments:
Post a Comment