WIZARA ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, imefanya
marekebisho katika upangaji wa viwango vya alama za matokeo ya wanafunzi wa
kidato cha nne kwa kufutwa daraja sifuri na kuwekwa daraja la tano, ambalo
litakuwa la mwisho katika ufaulu.
Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Profesa Sifuni Mchome,
alitangaza mageuzi hayo jana alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari
kuhusu upangaji wa viwango vya alama, matumizi ya alama endelevu ya mwanafunzi
na ufaulu.
Alisema kwa muundo mpya, daraja la kwanza litabakia
kuanzia pointi 7 hadi 17 kama ulivyokuwa muundo wa zamani, ambalo ni kundi la
ufaulu uliojipambanua na bora sana, daraja la pili litaanzia pointi 18 hadi 24,
badala ya pointi 18 hadi 21 kama zamani na likiwa ni kundi la ufaulu mzuri
sana.
Pia daraja la tatu pointi zake zitaanzia 25 hadi 31,
badala ya zile za zamani za 22 hadi 25 na kundi hili litakuwa la ufaulu mzuri
wa wastani.
Kwa mujibu wa Prof. Mchome, daraja la nne litaanzia
pointi 32 hadi 47, badala ya zile za zamani za kuanzia pointi 26 hadi 33, na
kundi hilo litajulikana kama la ufaulu hafifu.
Daraja jipya lililoongezwa ni lile la tano,
litakaloanzia pointi 48 hadi 49, litakalofuta daraja sifuri la zamani,
lililokuwa na pointi 34 hadi 35, na sasa litajulikana kama kundi la ufaulu
usioridhisha.
Prof. Mchome alifafanua kuwa mabadiliko hayo
yamefanyika ili kuendelea kuimarisha mfumo wa elimu na kuweka wazi taratibu
mbalimbali kwa ajili ya mitihani na masuala mengine.
Pia alisema wataalamu wa mifumo ya mitihani
wataufanyia kazi zaidi muundo huo wa madaraja ili uweze kutumika kwa ufanisi
katika kipindi hiki cha mpito.
“Yapo mambo mengi mengine ambayo hayana budi kuendelea
kuimarishwa, ukiwamo mfumo wa mitaala, walimu, mazingira ya kujifunzia na
kufundishia pamoja na vitabu na vifaa vingine muhimu katika elimu,” alisema.
Awali alisema kuwa wizara imekusanya maoni ya wadau wa
elimu kuhusu upangaji wa viwango vya alama katika mitihani ya kuhitimu kidato
cha nne na cha sita pamoja na matumizi ya alama za tathmini endelevu ya
mwanafunzi.
Alisema maoni hayo ya wadau yamekusanywa kwa sababu
kwa muda mrefu sasa upangaji wa viwango vya alama vinavyotumika na utaratibu
wake katika mitihani hiyo yote ni vya elimu ya sekondari.
“Sera ya elimu na mafunzo ya 1995 imeelekeza kwamba
katika kuamua kiwango cha ufaulu wa mwanafunzi wa elimu ya sekondari, alama za
tathmini endelevu ya mwanafunzi zitachangia asilimia 50 na mtihani wa mwisho
asilimia 50.
“Kwa upande wa Zanzibar alama hizo zimekuwa
zikiandaliwa kwa mfumo wa asilimia 40 na mtihani wa mwisho asilimia 60. Pamoja
na kwamba baraza halijawahi kuitumia mifumo hii tokea ilipowekwa, kumekuwa na
mitazamo, maoni na mapendekezo tofauti katika muundo na matumizi ya alama
hizo,” alisema.
Vilevile alisema kuwa wadau wengi walishauri muundo
uliopo sasa wa madaraja uimarishwe ili kuanza kutumia muundo wa wastani wa
alama katika ufaulu (GPA), kwa kuwa ni rahisi kueleweka na kuuandaa kuliko
muundo wa madaraja.
Pia kwa kutumia muundo huo wa GPA inakuwa rahisi
katika kukadiria uwezo wa mwanafunzi kielimu na kufanya uamuzi mbalimbali
ikiwamo kuendelea na masomo katika ngazi mbalimbali za elimu.
Wakati huo huo, Prof. Mchome alisema kuwa mtihani wa
kidato cha nne na mtihani wa maarifa mwaka huu unatarajiwa kufanyika nchini
kote kwa siku 18 kuanzia Novemba 4 hadi 21.
Alisema jumla ya watahiniwa walioandikishwa kufanya
mtihani huo ni 427,906, ambapo kati yao 367,399 ni watahiniwa wa shule na
60,507 ni wa kujitegemea.
Kwa mujibu wa katibu mkuu huyo, hadi sasa maandalizi
na usafirishaji wa mitihani hiyo hadi ngazi ya mkoa yamekamilika.
No comments:
Post a Comment