Ni zama za ufashisti
mambo leo
Na
Absalom Kibanda
BAADA
ya kuwa nje ya ofisi kwa zaidi ya mwezi mmoja sasa kwa likizo maalumu ya kikazi
niliyoichukua baada ya kufanya kazi mfululizo kwa miaka takriban miwili pasipo
kupata mapumziko ya kutosha, nimerejea tena kazini.
Kwa
makusudi niliamua kutumia sehemu ya likizo yangu kusafiri kwa mafunzo ya muda
mfupi hadi katika mji mdogo wa Grahamstown nchini Afrika Kusini ambako
nilihudhuria mafunzo ya uandishi wa habari wa takwimu au kwa kimombo, ‘data
journalism’.
Siku
moja baada ya kumaliza mafunzo hayo ambayo yalihusisha pia wanahabari wengine
kutoka mataifa mbalimbali ya Afrika, nilipata fursa ya kuhudhuria mkutano wa
kila mwaka ujulikanao kama ‘Highway Africa’ unaoandaliwa na Shule ya Uandishi
wa Habari ya Chuo Kikuu cha Rhodes kilichoko katika mji huo huo wa Grahamstown.
Highway
Africa ni mkutano mkubwa unaowakutanisha waandishi wa habari, wadau wa habari
na wanataaluma wengine ambao fani zao zinaingiliana na uandishi wa habari
kutoka katika nchi takriban zote za Afrika na nje ya bara hili. Zaidi ya watu
600 walihudhuria mkutano huo wa siku mbili.
Ulikuwa
ni mkutano muhimu na nyeti ambao ulinipa fursa ya kubadilishana mawazo na
wanahabari wenzangu wa mataifa mbalimbali ya Afrika kuhusu afya ya taaluma ya
habari katika taifa langu na mengine Afrika na namna uhuru wa upashanaji habari
na utoaji maoni unavyokabiliwa na changamoto lukuki nyakati hizi.
Mijadala
rasmi na ile isiyokuwa rasmi ambayo nilishiriki ilinifumbua macho na kuanza
kuliangalia taifa langu na mengine kadha wa kadha ya Afrika na yale ya nje ya
bara hili kwa jicho ambalo lilinipa majibu ambayo pengine nisingeyabaini iwapo
ningekosa fursa ya kukutana na magwiji wa habari wa Afrika na ulimwenguni
wanavyoitazama afya ya tasnia ya habari katika bara hili na pengine katika nchi
moja moja.
Mbali
ya kushangilia ushindi aliopata Mtanzania mwenzetu, Ndesanjo Macha kwa kuwa
mwanahabari wa Afrika mwenye blogu bora, kikubwa ambacho niliondoka nacho
katika mkutano huo ni kubaini kwangu kuwa Tanzania na baadhi ya mataifa yaliyo
katika bara hili yanapita katika kipindi kigumu cha mabadiliko ya kimfumo na
kiutawala.
Kipindi
hiki kinachokuja miaka 50 baada ya uhuru wa mataifa mengi ya Afrika, kinabeba
taswira ya kuanza kuzorota na kukwama kwa kile ambacho kilianza kuonekana kuwa
ni kuongezeka kwa wigo wa uhuru wa kutoa maoni na kupashana habari.
Hali
hii ilionekana kuwagusa wanazuoni wengi ambao tayari wameshaanza kufanya tafiti
ili kubaini ni kitu gani hasa kimekuwa kikitokea ndani ya tawala za
kidemokrasia ambazo katika mwelekeo wa kushangaza na kushtusha ghafla
zinaonekana kuanza kubeba chembechembe hatari zinazoashiria kuminywa kwa uhuru
wa habari.
Nje
ya vyumba vya mikutano huko Grahamstown nilihojiwa na wadau wa habari waliokuwa
na shauku kubwa ya kufahamu kile walichokiona kupitia mitandao ya intaneti
kuhusu kuuawa kwa mwandishi wa habari Daudi Mwangosi wakati akiwa katika mikono
ya polisi.
Kilichoonekana
kuwashtua wadadisi hao ni picha iliyopigwa na Mpigapicha Mkuu wa gazeti hili,
Joseph Senga ambayo ilikuwa ikionyesha namna Mwangosi alivyokuwa amezongwa
katikati ya kundi la askari polisi sekunde chache kabla ya kufikwa na mauti
yaliyocharanga kabisa mwili wake kwa kiwango cha kusababisha picha za mauti
yake kuwa za kuogofya sana.
Picha
ya Senga iliyosambazwa katika mitandao mbalimbali ya inteneti na katika ukurasa
wa mbele wa gazeti la Mwananchi la siku ya pili ya tukio kabla ya kurudiwa tena
katika gazeti hili siku iliyofuata iliibua tafakari ya namna yake dhidi ya
serikali za baadhi ya watawala waliochaguliwa kidemokrasia zinavyoonekana
kuchukua maamuzi ya kikatili kama si ya kimabavu dhidi ya uhuru wa habari, wa
kujieleza na ule wa kutoa maoni.
Taswira
ya picha zile za Mwangosi ilikumbusha wadadisi hao matukio kama yale
yaliyotokea huko huko Afrika Kusini siku chache tu zilizopita ambako askari
polisi waliwaua kwa kuwafyatulia risasi wafanyakazi zaidi ya 40 wa migodi
katika eneo la Marikani waliokuwa wakiandamana kudai nyongeza ya mishahara yao.
Hawakuishia
hapo, mijadala ilikwenda mbali zaidi na kuzungumzia matukio kama yale ya
kufungiwa kwa gazeti la MwanaHALISI ambalo kwa jicho la wasomaji wa taarifa
zake wanaotoka nje ya Tanzania wanaliona kuwa lililokuwa likiibua hoja nzito
dhidi ya serikali na viongozi wake.
Wadadisi
hao walipojua kwamba mimi ndiye mhariri ninayekabiliwa na kesi ya uchochezi kwa
sababu ya makala iliyoandikwa katika gazeti hili na kwamba ndiye ninayeshikilia
wadhifa wa uenyekiti wa Jukwaa la Wahariri, walitarajia mengi kutoka kwangu
kuhusu afya ya uhuru wa habari wa kujieleza na kutoa maoni.
Kwa
kuwa kesi yetu ingali bado iko mahakamani, itoshe tu kutambua kwamba, nilitumia
vyema fursa ya kuhudhuria mkutano huo na kukutana na magwiji wa habari duniani
kwa kuweka kumbukumbu sawia kuhusu hali tete ya utendaji kazi wa vyombo vya
habari hapa nchini zama hizi za serikali ya awamu ya nne.
Wako
walioahidi kuandika vitabu katika siku zijazo kuhusu kile nilichowaeleza
nikitumia taarifa zilizopata kuripotiwa magazetini na zile ninazozijua kwa
undani kuhusu nini hasa kilikuwa kikitokea ndani ya vyumba vya habari na namna
wanahabari wa Tanzania tunavyofanya kazi katika mazingira yaliyojaa mizonge
mingi, tabu na misukosuko ambayo aghalab imefikia hatua ya kutufanya tusiijue
kesho yetu.
Bado
naamini nilifanikiwa kufikisha ipasavyo ujumbe wangu kuhusu matukio kama yale
ya kufungiwa kwa gazeti la MwanaHALISI na lile la kumwagiwa tindikali kwa
Mkurugenzi Mtendaji na Mhariri Mtendaji wa gazeti hilo, Saed Kubenea, miaka
kadhaa iliyopita kama mfano wa matukio ambayo yanaeleza nini kipo nyuma ya
pazia ya kile kinachoitwa uhuru wa habari, kutoa maoni na wa kujieleza hapa
nchini na hususan zama hizi za Serikali ya Awamu ya Nne.
Mmoja
wa waandishi wakongwe alieleza kuguswa na namna vitendo hivi vya baadhi ya
watendaji wa taasisi za dola vinavyoiweka Tanzania karibu kabisa na tanuri la
kuzalisha watuhumiwa wa kwanza wa kesi ya kukandamiza haki za binadamu katika
Mahakama ya Kimataifa ya Haki za Binadamu iliyoko The Hague, Uholanzi.
Mwandishi
mwingine alitaka wanahabari wa Afrika tufanye utafiti wa kina kuhusu kile
alichokiita udikteta wa kidemokrasia ambao alisema unaonekana kuanza kuibuka
katika Afrika na ukitoa mwelekeo wa kuminya uhuru wa habari na ule wa kutoa
maoni kwa njia za panya.
Mwandishi
huyo aliitaja Rwanda ya Paul Kagame na Ethiopia ya zama za Meles Zenawi kuwa
mfano wa mataifa ya Afrika ambayo yalikuwa yamefikia hatua ya kuminya uhuru wa
habari na ule wa kutoa maoni kwa kuwashitaki waandishi na wahariri kwa makosa
mbalimbali kutokana na kile kilichoandikwa au kuripotiwa katika vyombo
wanavyofanyia kazi.
Ni
nyakati hizo hizo tukiwa Grahamstown likaibuka tukio la mchora vibonzo wa India
aliyekamatwa na kufikishwa mahakamani kwa kosa la kudhalilisha mamlaka za dola
kutokana na katuni aliyoichora dhidi ya Bunge la nchi hiyo kwa namna ambayo
iliikera serikali.
Ingawa
sote tulikubaliana kwamba uhuru wa habari na ule wa kutoa maoni ulikuwa unayo
mipaka ambayo inatupasa wahariri, waandishi wa habari na wadau wa habari
kuitambua, bado sote tuliondoka Grahamstown tukiwa na taswira moja kubwa
kwamba, Afrika na dunia kwa ujumla zinapita katika zama za aina mpya si ya
udikteta bali ya ufashisti uliojificha nyuma ya pazia lenye majina mengi
mazuri.
Hitimisho
hilo la Grahamstown nililoondoka nalo nje ya vyumba vya mikutano ya Highway
Africa ndilo ambalo limezaa kichwa cha habari cha makala hii leo ambacho
wanazuoni wana kila sababu za kuanza kukifanyia utafiti kwani dalili za wazi
zinaonyesha na mazingira ya sasa yanathibitisha kwamba tumeanza kushuhudia aina
mpya ya ufashisti wa kistaarabu.
Aina
hii ya ufashisti imebeba sura nyingi. Kwa upande mmoja inabeba sura ya
kuheshimu utawala wa sheria na kwa upande mwingine unaweka ukomo kwa watawala waliochaguliwa
kupitia sanduku la kura kuchokozwa, kukosolewa au hata kuguswa.
Kama
ilivyokuwa kwa ubeberu uliokuja baada ya ubepari kuamua kutoka nje ya mipaka ya
mataifa husika na kwa namna ile ile ukoloni ‘mambo - leo’ ulivyojijenga katika
mataifa huru yaliyoushinda ukoloni halisi ndivyo ilivyo sasa kwa Afrika inayoshangazwa
na namna ufashisti wa kina Musolini, Hitler na wengine unavyorudi kwa mlango wa
nyuma. Hakika hizi ni zama za ufashisti mambo leo.
Mwisho
No comments:
Post a Comment