Social Icons

NDOA YANGU, Ningejua!

NDOA YANGU, Ningejua!


JWTZ yakiri kuuawa kwa wanajeshi
*JK awalilia askari wake

Edna Bondo na Shabani  Matutu

JESHI  la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), limekiri kuuawa kwa wanajeshi wake saba na wengine 14 kujeruhiwa akiwamo askari polisi katika shambulio la ghafla lililofanyika Darfur juzi.

Taarifa rasmi ya JWTZ iliyotolewa na msemaji wake Kanali Kapambile Mgawe imesema kuwa shambulizi hilo lilitokea
 juzi saa tatu asubuhi baada ya kikundu cha waasi wa Darfur kuvamia ghafla na kukishambulia kikosi cha askari 36 na ofisa mmoja umbali wa kilomita 20 kutoka Makao Makuu ya kikosi hicho.

Kanali Mgawe alisema kuwa wanajeshi hao walikuwa wakiwasindikiza waangalizi wa amani kutoka Khor Abeche kuelekea eneo la Nyara huko Darfur, ambao pia ulikuwa na
maofisa na  askari kutoka mataifa mengine ambao walijeruhiwa.

Aliongeza kwamba wanajeshi walipatwa na mkasa huo wakitekeleza jukumu la kulinda amani la Umoja wa Mataifa (UN),  nchini Sudan katika eneo la Darfur 

Alisema miili ya marehemu na majeruhi imechukuliwa kutoka katika eneo la tukio na kupelekwa katika hospitali Kuu ya Nyara ambalo ni eneo la operesheni kwa hifadhi na huduma ya matibabu kwa majeruhi.
alisema JWTZ inawasiliana na familia za marehemu kuhusu taratibu za mazishi sambamba na Umoja wa Mataifakuhusu taratibu zote muhimu zinazohusiana na matibabu ya waliojeruhiwa.

Mgawe alisema tayari   ujumbe maalumu umeteuliwa kwenda Khartoum na Darfur kuzungumza na mamlaka kuhusiana na tukio hilo.

“Tunahitaji jeshi letu kuongeza uwezo wa kujilinda na mashambulizi inapobidi pindi kikundi chetu kinapokabiliwa na mashambulizi ya aina hiyo,” alisema Kanali Mgawe

Akifafanua kuhusu hilo alisema kuwa kwa sasa wanatumia aina ya ulinzi unaojulikana kama ‘Chapter 6’ usiowahitaji kutumia nguvu sana na badala yake wamepanga kushauriana na UN kutumia ‘Chapter 7’ itakayo toa nafasi kwa wanajeshi kujilinda kiusalama zaidi.

JK awalilia

Rais Jakaya Kikwete na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi ameshtushwa na tukio la kushambuliwa na kuuawa kwa askari hao, na kujeruhiwa kwa wengine 14 kulikofanywa na kundi la waasi wa Sudan.

Katika salamu zake na ametuma salamu za rambirambi za moyoni mwake kwa Jeshi la Wananchi wa Tanzania na kwa familia za wafiwa wote.

Aidha, Rais Kikwete anaungana na Watanzania wote na hasa maofisa na wapiganaji wa JWTZ na familia za wafiwa kuomboleza vifo vya vijana hao hodari wa Tanzania. Rais pia anaungana na Watanzania wote kuwaombea wale walioumia katika tukio hilo waweze kupona haraka na kuendelea na majukumu yao ya ulinzi wa amani chini ya Umoja wa Mataifa.

Katika salamu zake za rambirambi kwa Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Davis Mwamunynge na familia za wafiwa, Rais Kikwete  alisema:

“Sina maneno ya kutosha ya kuelezea mshtuko, huzuni na masikitiko yangu makubwa kufuatia vifo vya vijana wetu hao ambao wamepoteza maisha yao katika shughuli muhimu sana ya utekelezaji wa majukumu ya Umoja wa Mataifa ya kulinda na kuleta amani katika eneo la dunia ambako maelfu kwa maelfu ya watu wamepoteza maisha yao kwa kushambuliwa na waassi.

”Napenda kwa niaba ya Watanzania wenzangu niwahakikishieni kwamba hakuna shaka kuwa vijana wetu hao tokea walipokwenda Darfur Februari mwaka huu, na kwa hakika tokea Tanzania ilipoanza kuchangia walinzi katika eneo hilo mwaka 2007, wamefanya kazi nzuri sana, kazi iliyoongozwa na weledi wa hali ya juu na kazi ambayo imeiletea nchi yetu heshima kubwa. Tutaendelea kuwaenzi kwa kujivunia kazi yao.”

Rais Kikwete alisema: “Nakutumia wewe Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi salamu za rambirambi za dhati ya moyo wangu kuomboleza vijana wetu hawa. Kupitia kwao, natuma salamu za rambirambi kwa maofisa wakuu na maofisa wadogo pamoja na wapigaji wote wa Jeshi letu kwa kupotelewa na wenzao. “

“Aidha, kupitia kwako, nawatuma salamu zangu kwa wanafamilia za waliopotelewa na wapenzi wao na ndugu zao katika tukio hilo. Wajulishe kuwa naungana nao katika kuomboleza. Wajue kuwa uchungu wao ni uchungu wangu pia na wa Watanzania wote na kuwa kwa pamoja tunamwomba Mwenyezi Mungu awape moyo wa uvumilivu na subira katika kipindi hiki kigumu. Vile vile kwa pamoja tunamwomba Mwenyezi Mungu azilaze peponi roho za marehemu. Amina.’
Kwa walioumia, Rais Kikwete ametoa salamu za pole na kuwaombea kwa Mwenyezi Mungu wapone haraka na kuendelea na shughuli zao za ulinzi wa amani chini ya Umoja wa Mataifa.

Mwisho

No comments:

Post a Comment