Social Icons

NDOA YANGU, Ningejua!

NDOA YANGU, Ningejua!

LHRC wataka hukumu ya kifo ifutwe


KITUO cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), kimewataka wabunge na wadau wengine watakaoshiriki katika bunge la katiba kufuta ibara ya 69 ya rasimu inayompa rais mamlaka ya kuidhinisha utekelezwaji wa adhabu ya kifo.

Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Dk. Helen Kijo-Bisimba alisema hayo alipokuwa akitoa tamko kwa vyombo vya habari katika maadhimisho ya siku ya kupinga adhabu ya kifo duniani.

Dk. Bisimba alisema, wabunge hao wanapaswa kuwezesha katiba ijayo kutoa ulinzi wa uhakika kwa haki ya kuishi kama nchi za Msumbiji, Rwanda, Burundi, Angola na Namibia zilivyofanya.

“Hii ni kutokana na ukweli kuwa adhabu hii imeshindwa kukomesha au kuondoa kabisa makosa yanayohukumiwa kwa adhabu hiyo,” alisema.

Mkurugenzi huyo pia alishauri kujifunza kutoka kwa nchi nyingine duniani ambazo hazitekelezi adhabu ya kifo, jinsi gani zimekuwa zikishughulikia watu wenye makosa makubwa kama ya kuua.

Alipendekeza wale watakaokutwa na hatia kutokana na makosa ambayo walipaswa hukumu ya kifo, wafungwe katika gereza maalum, na uanzishwe mfuko wa kuhudumia watoto wa familia za wale wote walioathirika kwa ndugu zao kuuwawa na hao wafungwa.

“Fedha hizo zigharamie matunzo na elimu ya waathirika wa vitendo vya wauaji,” alisisitiza.

Vile vile alishauri kuwa, sheria ya kiwango cha chini cha adhabu irekebishwe ili jaji asilazimishwe kutoa adhabu ya kifo kwa kila mtu atakayepatikana na hatia na kuhukumiwa adhabu ya kifo.

Awali alisema kwa miaka 19 sasa adhabu ya kifo haijatekelezwa hapa nchini ijapokuwa watu wengi wameendelea kuhukumiwa adhabu hii kwa makosa ya mauaji ya kukusudia.

Pia alisema tangu Tanzania ipate uhuru 1961 hadi sasa watu 238 wamenyongwa na idadi ya watu waliohukumiwa kunyongwa imeongezeka kutoka watu 46 mwaka 1961 kufikia 2562 mwaka 2007.

Alisema, kituo hicho kinapinga utekelezwaji na uwepo wa adhabu hiyo kwenye sheria za nchi, kwani pamoja na kuwa inakiuka haki ya kuishi, lakini ikumbukwe kuwa hakuna nchi au mtu mwenye haki ya kuchukua au kukatisha maisha ya binadamu.

No comments:

Post a Comment