NDOA YANGU, Ningejua!
NITAMPATAJE MCHUMBA
Hiki ni kitabu changu kipya cha pili. Vijana wengi wanapata shida katika kuanza na kuendeleza mahusiano yatakayowafikisha katika maisha ya ndoa. WENGI HAWAJUI NINI M,AANA YA MCHUMBA NA MCHUMBA NI MTU GANI Wengi hawajui waanzisheni urafiki sahihi na wa kweli, maisha yanayopaswa kuishi katika urafiki, na uchumba, Hivyo kitabu hiki kinafundisha namna ya kuanzisha urafiki, mambio ya kuchunguza wakati wa urafiki, namna ya kuanzisha uchumba, haki na wajibu wa wachumba na wazazi wao, muda sahihi wa kusihi katika uchumba na hatimaye mambo ya msingi yanayopaswa kukamilisha ama kufuatwa siku ya ndoa. Nawakaribisheni kukisoma watu wa rika zote kwa maana kuna wanandoa wengi ambao hawakufuata misingi sahihi ya kuanzishwa kwa ndoa yao na ndio maana wanalia sasa.
NACHEKA KWA UCHUNGU; TANZANIA NA UONGOZI WA DAMU
Nacheka kwa uchungu Jan 14
Tanzania
na uongozi wa damu
NIMELAZIMIKA kuyakumbuka maneno mazito aliyotoa
Spika wa Bunge la Tanzania Anne Makinda wakati wa msiba wa Waziri wa Fedha na
Uchumi, Dk William Mgimwa aliyefariki mwanzoni mwa mwezi huu nchini Afrika
Kusini.
Mbele ya umati wa waombolezaji, Makinda alisema
ingekuwa ni amri yake angekufa mtu (kwa namna nyingine waziri) mwingine lakini
sio Mgimwa!
Sitaki kurejea namna alivyoshambuliwa kwa maneno,
na mijadala ilivyotamalaki katika vyombo vya habari kuhusiana na kauli hiyo.
Kilichonisukuma kukmumbuka maneno ya mama Makinda
ni kile kinachoendelea katika wilaya ya Bunda mkoani Mara.
Juzi nililazimika kushuka katika mji huo mdogo
nikitoka Musoma kikazi ili niwe kama Yule Thomaso tunayemsoma katika Biblia
ambaye alipoambiwa Yesu Kristo amefufuka alikataa hadi amwone kwa macho yake na
kugusa makovu ya misumari aliyoshindiliwa msalabani.
Mji mzima wa Bunda unatikisika kwa sasa kutokana
na kampeni za uchaguzi mdogo wa diwani wa kata ya
Nyasura, baada ya kiti hicho kubaki wazi kufuatia kifo cha aliyekuwa diwani
wake Zamberi Ngobayi (Chadema).
Katika kampeni hizi ambazo vyama viwili, Chama cha
Mapinduzi (CCM) ambacho ni dhahiri kitamsimamisha Alex Mwikwabe ambaye inadaiwa
alipatikana baada ya wagombea wawili wa awali kujitoa na Chama cha Demokrasia
na Maendeleo (Chadema) kilichomsimamisha Magambo Webiro zinaendeshwa katika
hali inayodhihirisha ubabe, vitisho, hila na ubabaishaji wa hali ya juu.
Nimeshuhudia kampeni za kuchafuana majina, hadhi
na heshima ya wagombea zikifanywa na watu wazima kabisa, tena viongozi
waliostahili kuionesha jamii kuwa wanawathamini watanzania na wanaheshima
matakwa ya watu ya nani awe kiongozi wao.
Nimeshituka zaidi hata baada ya kuona upande mmoja
ukijaribu kuwadanganya wapiga kura kwa hoja za kipuuzi za kwamba mgombea wa
Chadema ni mganga wa kienyeji na hivyo hafai kuchaguliwa. Tena wanaosema hivyo
ni viongozi wengine wa CCM ngazi ya wilaya. Ni hoja ya ajabu kwa sababu hakuna
popote katika katiba ambapo mtu anayetibu watu kwa kutumia dawa za kienyeji
haruhusiwi kuchaguliwa na kuwa kiongozi. Na kwa kutambua hilo, hao hao
wanaosema hivyo, wanasahau kuwa mmoja wa wabunge wake wa bunge la Muungano ni
mganga wa kienyeji ambaye katika uchaguzi uliopita alimbwaga daktari mwenye PhD!
Je viongozi wa CCM wa wilaya ya Bunda kwa hoja
hiyo ya uganga iliyokanushwa na mhusika mwenyewe, wanataka kusema kuwa wapiga
kura Korogwe vijijini walifanya kosa kumchagua mganga wa kienyeji pia Prof Maji
Marefu (CCM)kuwa Mbunge wao?
Na katika namna ya kushangaza, baadhi ya viongozi
wa CCM sasa wanadaiwa kumwandaa mwana mama mmoja atakayetembea kata nzima
kueleza namna mgombea wa Chadema alivyotapeli kwa kutumia uganga wake. Mama
huyo anadaiwa kuwa atatangaza jinsi mgombea wa Chadema alivyomtapeli mamilioni
ya fedha ili amtibu!
Fikiri tu kwamba suala la uganga limechukua nafasi
kubwa katika kampeni huku upande wa pili yaani Chadema, badala ya kupuuza
propaganda hizo, nao wamejikita kujibu hoja na kusahau kutangaza sera.
Mbali na hoja ya uganga, wapinzani wa mgombea huyu
wameingiza ubaguzi wa kikabila na kimaeneo. Wanajaribu kuwaaminisha wapiga kura
kuwa ni hatari kumchagua mgombea huyo kwa sababu sio mzawa wa Nyasura bali
mhamiaji aliyefukuzwa kutoka Kata nyingine ya Kunzugu katika kitongoji cha Bokole.
Kana kwamba hoja hizo kwa viongozi wa chama tawala
hazina madhala kwa taifa, sasa wanatuhumiwa kuibua jambo baya zaidi ambalo
limeanza kuwatisha na kuwapa kiwewe baadhi ya wananchi sio wa Kata ya Nyasura
tu bali wilaya nzima ya Bunda.
Hili ni kuwepo kwa tuhuma kwamba zipo njama za
kutaka kumkamata mgombea wa upinzani na kumbambika kashfa ya kuiba nyaraka sa
siri za serikali.
Inadaiwa kuwa hizo zinazoitwa nyaraka za siri za
serikali, zile zinazohusiana na sakata la ardhi katika wilaya ya Bunda.
Kwamba mgombea huyo anatembea na nyaraka za
mikataba feki iliyotumika kutaifisha ardhi ya mlima Balili inayosemekana ni
mali halali ya shule ya msingi Balili na pia ya Kanisa la Wasabatho.
Inasemekana tuhuma hizo zinawagusa baadhi ya
watendaji wa wilaya na mkoa, akiwemo mkuu wa mkoa mmoja hapa nchini.
Nyaraka hizo zinazoitwa za siri, pia zinadaiwa
kuwa ni zile zinazofichua kile kinachoitwa tuhuma za waziri mmoja mwandamizi wa
serikali ya CCM anayedaiwa kuchukua kwa mabavu sehemu ya ardhi ya shule moja ya
sekondari.
Kampeni hizo za uchaguzi wa udiwani kata ya
nyasura na zigine 28 nchini
utakaofanyika Februari 9,2014, zinaashiria jambo moja tu. Umwagaji wa damu!
Hali sio shwari, viongozi na wanachama wa vyama
vya upinzani wameungana na lugha inayotamba sasa ni kwamba..’heri kufa kuliko
kuonewa, kuliko kudhulumiwa’
Wapenzi na wanachama wa CCM, nao wanatamba na
kauli,….’kwa gharama yoyote lazima tukomboe kata yetu”.
Kauli hizi sio njema hata kidogo hasa
zinapopaliliwa kwa nguvu na wanasiasa wakomavu ambao chama chao kinaongoza
nchi. Ni kauli ambazo zinaonesha kuwa uwezekano wa kupata viongozi wazuri,
wakweli, waadilifu na wachapakazi kama alivyokuwa waziri Mgimwa ambaye Spika
Makinda hakutaka afe ni ndoto.
Inatia uchungu zaidi ikiwa leo watanzania wanazidi
kushuhudia haki na demokrasia ikikandamizwa kwa gharama za walipa kodi, ili tu
watu wanaowataka wachaguliwe kuwa viongozi wa watu hata kama hawana sifa na
hawapendwi.
Spika Makinda hata kama kauli yake, haikuwa njema
masikioni mwa watu, ajue kuwa chama chake kitasaidia kupatikana kwa viongozi
kama marehemu Mgimwa kikiacha mizengwe, hila, ujanja wa kishamba kuendesha
kampeni zisizo na mashiko.
Spika Makinda ajue kuwa ni jukumu la CCM kushika
na kusimama kama ‘baba wa demokrasia’ na hivyo, kuacha ghiriba za aina yoyote
ile katika chaguzi ziwe ndogo ama kubwa.
Kampeni za kudhalilisha, kukomesha na kutesa
wasiokuwa wapenzi na wanachama wa CCM na kulazimisha kumweka mtu wa ovyo
madarakani kamwe haziwezi kuleta watendaji bora wa serikali. Haziwezi kulipatia
taifa madiwani, wabunge na mawaziri bora.
Kampeni zinazosukumwa na ubabe, uonevu, wizi wa
kura na hata kumwaga damu za wananchi, haziwezi kamwe kuleta manufaa katika
nchi zaidi ya machafuko na umwagaji damu. Kauli ya wana wa Bunda kwamba liwalo
na liwe ni ishara ya kwamba watu wamechoka kunyanyaswa. Ni kauli za waliokosa
matumaini dhidi ya serikali yao, na hawaitaki.
Spika Makinda atatamani wafe mawaziri wengi ikiwa
leo hii katika kampeni za uchaguzi wa marudio ya udiwani, polisi wanatumika
kupiga na kufungulia watu kesi za kubambika ili tu CCM ishinde.
Makinda ajue kuwa kama kweli ana uchungu na taifa
hili, basi awaambie viongozi wenzake kuwa wanalo jukumu la kuheshimu matakwa ya
watu. Wanalo jukumu la kujua na kutekeleza kile watanzania wanachokitaka na sio
kuwalazimisha kwa mbinu chafu hata za kumwaga damu.
Bado watanzania wanakumbuka jinsi viongozi wa
upinzani walivyofunguliwa mashitaka ya ovyo, kupigwa, kudhalilishwa na kuteswa
kisa tu walisimama kuwania uongozi katika chaguzi mbalimbali. Ni viongozi hao
hao wa CCM ambao Spika Makinda ni mmojawao, ambao wametumia nguvu na maarifa
mengi kuwaaminisha watanzania kuwa wapinzani ni watu wa ovyo, hatari na
wanaotakiwa kuogopwa kama ukoma.
Kibaya zaidi, Spika Makinda mwwenyewe mara nyingi
tu ameruhusu na kushiriki kukandamiza haki za wapinzani hata katika masuala ya
msingi ya nchi. Kiti chake kimeshiriki mara nyingi kunyamazisha sauti za
watanzania kupitia wabunge wao.
Wabunge wangapi wa upinzani wamekandamizwa
walipokuja na hoja zenye maslahi ya nchi? Wabunge wangapi wa upinzani wameitwa
wazushi na waongo walipoibua tuhuma dhidi ya mawaziri? Kama Kiti cha Spika
kingeruhusu hoja kujadiliwa na hatua madhubuti kuchukuliwa, leo hii uovu na
uvundo katika sekta ya elimu ingefikia hatua hii?
Ni mawaziri wangapi walilindwa na kiti cha Spika
pale walipotoa majibu ya uongo, ubabaishaji na yenye hasara kwa taifa? Kwa nini
kiti cha spika kiliwakingia kifua alafu leo kiti hicho hicho kinalia? Dhihaka?
Inatia uchungu basi tunaposikiaNi ajabu kwamba leo
eti analiachuklia wapinzani na kuwanachama makini na anayeheshimu demokrasia
hawezi kufurahia ushindi uliopatikana kwa kukandamiza na kuonea watu.
NACHEKA KWA UCHUNGU;TAIFA LIKIONGOZWA KWA SIASA CHAFU
Nacheka
kwa uchungu: jan 8,2014
Taifa
likiongozwa kwa siasa chafu
SIKUTAKA kamwe kujadili kinachoendelea ndani ya
chama kikuu cha upinzani nchini, ali maarufu kama Chadema.
Sikutaka kwa sababu, taifa langu linayo mambo
mengi makubwa ya kujadili na kuyatendea kazi. Mambo ya msingi yanayoweza
kuwakomboa wanyonge na umasikini wao wa kukosa elimu bora, afya bora, maisha
bora na usalama wa uhakika!
Nimelazimika kuyajadili katika mada ya leo kwa
sababu yanayotokea ndani ya Chadema yanaelekea kwa kasi kubwa kuchukua sura ya
kitaifa. Sio siri kwamba sasa yanashabikiwa kwa waziwazi ama kwa kificho na
umma wa watanzania, baadhi yao wakiwa wanasiasa wakongwe, wakubwa kabisa na
wengine wakiwa watendaji waandamizi ndani ya serikali ya CCM.
Mtu waweza kucheka kwa uchungu unapofikiria siasa
za Tanzania zilivyo kwa sasa. Ni kama igizo la mwendawazimu! Linaloumiza zaidi,
ni kwamba ‘upuuzi’ huu wa siasa ninazothubutu kuziita za kishamba zinaligharimu
taifa na kuleta hasara kubwa ambayo kwa bahati mbaya, hakuna anayeiona.
Zinagharimu muda wa watu kufanya kazi za kuzalisha
mali. Zinagharimu fedha halisi za watanzania kwa kuwa, wanaoziendesha wanatumia
fedha kwa kuliwasiliana, kulipana posho na hata ‘kuhongana’ ili tu mambo
wanayotaka yaweze kwenda.
Tukio la kuvuliwa madaraka wa Zitto Kabwe na
tishio la kunyang’anywa uanachama sio la kwanza katika siasa za Tanzania.
Ukiachilia mbali wale waliofikwa na jambo linaloelekea kumtokea Zitto ndani ya
upinzani, wapo waliopatwa na hayo enzi za TANU na CCM chini ya utawala wa siasa
ya chama kimoja.
Wengine walilazimishwa kujiondoa wenyewe huku
wakificha sababu halisi za kujivua kwao madaraka. Wakabaki wanaishi kama
wanachama wa kawaida kwa miaka mingi. Wapo waliorudishiwa nafasi za uongozi
baada ya kupita miaka kadhaa.
Tunakumbuka jinsi wanasiasa na viongozi wengine
walivyotimuliwa uongozi na uanachama baada ya kugoma kujiuzulu wenyewe. Wapo
baadhi kwa hofu ya usalama wa maisha yao, walilazimika kuondoka nchini, na
wengine waliendelea kuishi kwa kufanya shughuli nyingine za maendeleo na maisha
yao yakasonga mbele kwa mafanikio makubwa kuliko walivyokuwa katika ulingo wa
siasa.
Yaliyopendeka haya, watanzania hawakusikia
malumbano yaliyojaa matusi, kashifa, dharau, udhalilishaji na aibu kubwa kama
tunayoshuhudia sasa.
Sitaki kusimama upande wowote, lakini swali ambalo
watanzania wanatakiwa kujiuliza bila unafiki ndani yake, ni kwamba iweje leo
wanaotuhumiwa kusaliti chama chao, ndio wanaibuka na kututangazia ‘uozo’ wa
viongozi wenzao ndani ya chama?
Kiongozi anayejaribu kuwashawishi watanzania
waamini kuwa wenzake pia ni waovu kiasi cha kuzua hata utata wa kumiliki nyumba
za umma, kana kwamba watendaji wakuu wa shirika hilo nao ni wapuuzi kiasi cha
kuingia katika mkataba tata, anatushawishi tumuaminije?
Watu makini wanaposikia kwa mfano, watuhumiwa wa
kinachoitwa usaliti sasa wakirusha kete wakidai eti kiongozi fulani naye alipewa fedha mwaka 2005
wakati wa uchaguzi mkuu, wanajiuliza huyu anayetoa tuhuma hizi leo alikuwa wapi
kuyasema miaka yote hiyo?
Ikiwa kwa mfano pana ukweli wa tuhuma za viongozi
wenzake anaowataja kupokea fedha kutoka kwa kiongozi wa CCM, sababu zipi
zilimfanya afumbe mdomo miaka yote hiyo, hadi leo anazitoa baada ya kutishiwa
kufukuzwa? Mtu gani mwenye akili timamu atamwamini tena mwanasiasa wa aina hii.
Mtu gani mwenye busara ataendelea kusadiki yale anayosema sasa na yale
atakayotamka?
Lakini kinachotisha zaidi, sasa zinapotolewa
tuhuma zinazolenga kubainisha kuwa hata kifo cha Chacha Wangwe kilikuwa na
‘mkono’ wa mtu!
Ni siasa zinazotia uchungu mkubwa kuona kwamba, kiongozi anayetaka watu wamwamini anatangaza waziwazi na kurejea leo mwaka 2014 matukio ya 2005! Alikuwa wapi siku zote? Kipi kilimzuia asiseme? Na kwa nini aseme leo baada ya kutimuliwa? Ina maana kama asingechukuliwa hatua angenyamaza? Na kwa nini alikuwa bingwa wa kurusha makombora kwa viongozi wa CCM huku akijua (kama ni kweli) kwamba na wenzake wanapokea fedha kutoka huko huko CCM?
Ni siasa zinazotia uchungu mkubwa kuona kwamba, kiongozi anayetaka watu wamwamini anatangaza waziwazi na kurejea leo mwaka 2014 matukio ya 2005! Alikuwa wapi siku zote? Kipi kilimzuia asiseme? Na kwa nini aseme leo baada ya kutimuliwa? Ina maana kama asingechukuliwa hatua angenyamaza? Na kwa nini alikuwa bingwa wa kurusha makombora kwa viongozi wa CCM huku akijua (kama ni kweli) kwamba na wenzake wanapokea fedha kutoka huko huko CCM?
Nacheka kwa uchungu kuona mtu msomi, anayetaka
demokrasia ya kweli anaibuka na upuuzi huu leo hii, na katika nyakati ambazo
watanzania wamepigika kimaisha. Ni watu wasiofikiri sawa sawa watakaomuamini
tena. Ataamini tu na watu waliochoka kimaisha, wanaokubali kuwa kapu la kubeba
kila aina ya umbea, na walio tayari kusema, kutenda na kushabikia lolote na
chochote kwa sababu wanajua wanapewa pesa. Watu wa ovyo ovyo tu!
Inatia hasira kuona kuwa wakati tunawajibika
kujadili mambo mazito ya mustakhabari wa taifa letu, anasimama kiongozi
anayetaka kuwalisha watanzania ajenda za mambo binafsi ya mtu na familia yake.
Ni upuuzi mkubwa kwa watu waliokomaa kisiasa
kujadili uzinzi bungeni ama kwenye majukwaa, bila ushahidi makini na huku
ukitambua kuwa jambo hilo sio tu litamdhalilisha anayetuhumiwa, bali familia
yake, ndugu na jamaa zake.
Zitto anataka kuwaambia watanzania kuwa wanahitaji
kujua nani mzinzi na nani mtakatifu? Yaani watanzania kweli wanafikishwa mahali
pa kulishwa utumbo wa inzi kiasi hiki?
Tuseme ukweli bila unafiki. Hivi nani anastahili
kulalamika katika hilo linaloitwa sakata la uzinzi wa Mbowe? Ni Mwigulu Nchemba
aliyesema bungeni na Zitto anatutangazia sasa, au mume wa mbunge huyo na mke wa
Mbowe? Kwa nini wamenyamaza? Mtu makini, atanyamaza. Hawezi kujibu ujinga.
Ndivyo walivyofanya mke wa Mbowe na Mume wa Joyce!
Lakini pia mtu unajiuliza, hawa wanaowatuhumu
wenzao kwa uzinzi, wao wana usafi kiasi gani basi? Ni malaika wao?
Katika haya yanayoendelea, inahuzunisha zaidi
watanzania wanapobaini kuwa nyuma ya mgogoro huu, kuna mkono wa baadhi ya
wanasiasa waliofilisika wa upande wa pili.
Tulishuhudia namna baadhi ya wanasiasa na viongozi
wa CCM wakitoa shutuma, matusi na lawama kwa uongozi wa juu wa Chadema kwa
kumwondoa Zitto katika madaraka. Swali la kujiuliza, kiliwauma nini? Walikuwa
na maslahi gani na nafasi za kiongozi huyo ndani ya Chadema?
Hivi akitokea mtu akasema, waliumia kwa sababu
walijua mtu aliyempandikiza amebainika na ndio maana wanaumia atakuwa amekosea?
Nisaidieni hivi Yule waziri wa serikali aliyetamba kuwa Chadema kitakufa kabla
ya 2015, alikuwa anajivunia nini?
Ndio alitamka waziwazi na tukasikia akitamba kuwa
atahakikisha chama hicho pinzani kinakufa! Waziri mzima, ambaye angetegemewa
asimame na kuwaeleza watanzania kuwa nia yake ya chama chake ni kuhakikisha
adui ujinga, njaa, maradhi na ufujaji wa mali ya umma vinakufa kabla ya 2015,
anakurupuka na kusema Chadema inakufa, kana kwamba ndio kansa ya maendeleo yetu
anastahili kuendelea kuwa madarakani kweli kama tuko makini na uhai wa taifa
letu?
Je, ni kweli kwamba taifa hili limefikishwa mahali
pa watu wanakufa hospitalini kwa kukosa dawa, watoto wanafeli ovyo kwa kukosa
elimu bora, walimu wanapiga mihuri ardhini (wanatembea peku) na madaktari
wanagoma kwa sababu kuna chama kinaitwa Chadema?
Leo hii mangapi yanatokea hapa nchini, tena mabaya
yanayoumiza na kuua utu na heshima yetu kitaifa na kimataifa? Leo hakuna usalama wa uhakika hapa nchini.
Mtu unalala kwa hofu, unatembea kwa hofu, unakunywa kwa hofu,na katika hali
isiyoweza kusemeka sasa wakristo wanakwenda makanisani kwa hofu kubwa!
Hawana uhakika wa kurejea nyumbani kwa
usalama. Wanasali huku wanalindwa utafikiri
ni wafungwa. Wamepigwa mabomu kanisa, wakiimba, wamepigwa risasi wakienda
kusali, wakamwagiwa tindikali bila hatia yoyote.
Leo watu wanakwiba fedha za umma mchana na usiku.
Wanahabari tunawafichua, lakini hatuoni hawa wanaoshambulia wenzao wakichukua
hatua hata za kukemea tu. Hawaoni uchafu unaofanywa ndani ya nchi. Hawaoni
wanyama wanavyoangamizwa. Wao ni kushambuliana tuu!
Badala ya watu kujadili haya, na kujua nani katufikisha
hapa achukuliwe hatua, watu wanaibuka na visa vya ovyo na tuhuma za kitoto
kabisa za fulani anazini na mke wa fulani. Si mwacheni aliyechukuliwa mke ama
mume alalamike?
Watu wazima, wasomi kabisa na watu wanaoonekana
kuwa na busara, wanashinda kutwa nzima wakihangaika namna ya kuwazushia wengine
tuhuma za kipuuzi na kujiapiza namna watakavyoizika chadema.
Nacheka kwa uchungu kila ninapowaza aina ya
viongozi na wanasiasa sasa hawana muda wa kutafuta mbinu za kuinua uchumi wa
taifa letu, njia za kuwafanya watanzania waondokane na umasikini,kuokoa
rasilimali za nchi zinazoporwa usiku na mchana, badala yake kama mazuzu
wanahangaika na vyama vya upinzani na kuendesha siasa za kuchafuana!
KAPUYA AIGONGANISHA POLISI
SIKU chache baada ya Mbunge wa Urambo Magharibi,
Profesa Juma Kapuya (CCM), kudaiwa kutoweka nchini kukwepa mkono wa sheria
dhidi ya tuhuma za kutishia kumuua binti anayedaiwa kumbaka, vigogo wa polisi
wanadaiwa kuhusika kumsaidia kutimkia nje, Tanzania Daima limedokezwa.
Habari ambazo gazeti hili limezipata, zinaeleza kuwa
siku mbunge huyo akikamilisha taratibu za kusafiri, ndiyo siku ambayo Jeshi la
Polisi Mkoa wa Kinondoni lilikuwa limekamilisha kufungua jalada la tuhuma zake
na liliweka mtego wa kumnasa.
“Wakati Polisi Kinondoni wakiweka mtego wa kumnasa,
baadhi ya polisi walimjulisha na hata kumsaidia kuhakikisha anasafiri nje ya
nchi,” alisema mmoja wa maofisa wa juu wa polisi nchini.
Hata hivyo, kuna utata na kauli zinazopingana kuhusu
mbunge huyo. Taarifa nyingine zinasema kuwa mbunge huyo ambaye amepata kuwa
waziri, anadaiwa kusafiri kwenda nchini Sweden kwa masuala ya kikazi, na kwamba
atakuwepo huko kwa muda usiopungua mwezi mmoja.
Chanzo kingine kimedokeza kuwa mbunge huyo alidai
ametumwa kazi na kigogo mmoja serikalini na atakuwepo nchini humo miezi miwili
hadi mitatu.
Hata hivyo, haijajulikana kazi anayokwenda kuifanya
Kapuya ingawa kuna taarifa safari hiyo imelenga kutuliza upepo mbaya wa
kuandamwa na tuhuma za ubakaji ambazo zipo polisi hivi sasa.
Tayari Profesa Kapuya alishafunguliwa jalada namba OB/RB/21124/13
katika Kituo cha Polisi Oysterbay, jijini Dar es Salaam juzi.
Hata hivyo Jeshi la Polisi limesisitiza kuwa linamsaka
mbunge huyo ndani na nje ya nchi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camilius Wambura,
alikaririwa juzi kuwa watamtafuta Kapuya nchi yoyote atakayokwenda iwapo tuhuma
dhidi yake zitathibitika.
Alisema mtandao wa polisi ni mkubwa, hivyo si rahisi
kwa mtuhumiwa yeyote kuukwepa mkono wa sheria endapo itahitajika kufikishwa
kwenye vyombo vya sheria.
“Sisi tunashirikiana na polisi wa nchi mbalimbali
duniani, ndiyo maana inakuwa rahisi kwa mtuhumiwa aliyetoroka nchi fulani
kukamatwa nyingine na kurejeshwa kwao.
“Nataka niwaondoe hofu wale wote wanaodhani polisi
haiwezi kumkamata mtu akikimbia nchini, tuna mkono mrefu sana, na hatufanyi
kazi kinyume na taratibu zetu,” alisema.
Kamanda Wambura pia alikiri polisi kufungua jalada la
Kapuya, huku akiweka wazi kuwa kinachofanyika hivi sasa ni uchunguzi wa tuhuma
zake.
Alisema miongoni mwa maeneo wanayoyafanyia uchunguzi
ni kubaini kama ujumbe ulio katika simu ya binti anayedai kubakwa na kutishiwa
maisha unatoka katika simu ya mbunge huyo.
“Tumefungua jalada, lipo kwa ajili ya uchunguzi na
tukibaini kuwa ni nani anahusika na tuhuma hizo tutamsaka na kumkamata popote
alipo,” alisema Wambura.
Gazeti hili limekuwa likiandika namba ya simu ya Prof.
Kapuya ambayo huwa anaitumia kutuma ujumbe wa vitisho kwa binti huyo, ingawa
kuna vyombo vingine vya habari viliamua kuandika kwa mtazamo tofauti na
kumtuhumu dada wa binti aliyebakwa kuwa ni mtu mzima na kuwa ana uhusiano na
Kapuya, na wana watoto.
Simu hiyo namba 0784993930 inayodaiwa kumilikiwa na
Profesa Kapuya, mbali ya kutuma ujumbe mfupi wa maneno ya kutishia kuua, pia
ndiyo inayodaiwa kutumika kutuma pesa kwa njia ya mtandao kwenda kwa binti
huyo.
Tangu gazeti hili lianze kuandika tuhuma hizi nzito,
kumekuwapo na kusuasua kwa mtuhumiwa huyo kutiwa hatiani na Jeshi la Polisi.
Harakati za kufungua jalada dhidi ya Kapuya zilizoanza
wiki iliyopita ziliendelea hadi juzi ambapo polisi walitumia zaidi ya saa 12
kumhoji binti huyo anayedaiwa kubakwa ili kupata ukweli wa sakata hilo.
Akiwa polisi, binti huyo alikutana na Mkuu wa Polisi
Wilaya ya Kipolisi ya Oysterbay (OCD) na OC-CID wake na kutoa maelezo ya awali
kabla ya viongozi hao kumruhusu ayaweke malalamiko yake katika maandishi kwa
ajili ya kufunguliwa mashitaka.
SIHAMI CHADEMA-ZITTO
HATIMAYE Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe na
Mjumbe wa Kamati Kuu (CC), Dk. Kitila Mkumbo waliovuliwa uongozi ndani ya Chama
cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), wamevunja ukimya.
Katika mkutano wao na wahariri na waandishi wa vyombo
mbalimbali vya habari, Zitto ambaye alikuwa Naibu Katibu Mkuu CHADEMA, ameapa
kuwa hayuko tayari kuondoka ndani ya chama hicho na atakuwa mtu mwisho
kuondoka.
Wakati Zitto akiapa kwamba hayuko tayari kuondoka
CHADEMA, Dk. Mkumbo ambaye amekuwa mshauri mkuu wa chama hicho maarufu nchini,
amesema kuwa kile kinachoitwa uhaini ndani ya CHADEMA ni wasiwasi wa siasa za
ushindani kwa watu wasiotaka mabadiliko.
“Wengi walifikiri nikija hapa leo nitajibu mapigo na
kutoa uamuzi mgumu. Mimi sitoki CHADEMA, wanaotaka nitoke, wanitoe wao, na hiki
kinachoendelea ndani ya chama chetu ni mapambano ya kukuza demokrasia dhidi ya
wahafidhina, ni mapambano ya wanaopenda siasa safi dhidi ya wale wanaotukuza
siasa za maji taka,” alisema Zitto.
Akieleza sababu za kutokujitoa CHADEMA, Zitto alisema
zaidi ya nusu ya maisha yake yamekuwa CHADEMA, kwani alijiunga tangu alipokuwa
na miaka 16 hadi sasa ana miaka 37, na amekabiliana na vitisho mbalimbali dhidi
ya wasiotaka mageuzi.
“Nataka niwaeleze wanachama wa CHADEMA kwamba mimi
sitokuwa sababu ya CHADEMA kuvunjika, kimenilea na kunifikisha hapa na
ningependa na mwanangu siku moja awe mwanachama wa CHADEMA, na huu unaoitwa
usaliti kwangu dhidi ya CHADEMA ni sawa na mimi kujikata mguu wangu, sitoweza
kufanya hivyo,” alisema Zitto.
Mbunge huyo ambaye amepata umaarufu mkubwa tangu
alipoingia bungeni, alieleza kuumizwa na shutuma nyingi ambazo zimekuwa
zikielekezwa kwake kwa muda mrefu.
Alisema amekuwa akiItwa msaliti, mnafiki, mla rushwa
akihongwa kwa ajili ya kukisaliti chama.
“Naomba wanachama wanielewe, nimejiunga na chama hiki
nikiwa na miaka 16, ninaposingiziwa, naumia sana, nimefanya kazi ya kuchomeka
milingoti ya bendera za chama kwa viongozi wanaofika katika kijiji chetu,
ninapozushiwa naumia, nimefanya kazi zangu za kibunge kwa weledi mkubwa kwa nia
ya kukitumikia na kukipandisha chama changu, ninaambiwa ninakihujumu, inaniuma
sana,” alisema.
Zitto ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya
Kudumu ya Hesabu za Serikali (PAC), alisema akiwa mwanasiasa kijana na
binadamu, anaamini ana makosa kwa kuwa hakuna binadamu aliye mkamilifu, na
kwamba upungufu wake unapaswa kupimwa na mema aliyoyafanya.
Ataja tuhuma zake
Akizungumzia tuhuma zilizomfanya apokwe nyadhifa zake
zote na kubaki kuwa mwanachama, Zitto alisema kuna upotoshaji mkubwa wa taarifa
kwani tuhuma alizoambiwa ndani ya Kamati Kuu ni tofauti na zilizotolewa kwa
waandishi wa habari.
Alisema tuhuma zote zimekuwa katika taswira mbili
zinazomuonyesha kuwa ni mbinafsi na mtu anayetumiwa kukisaliti chama kwa
kupokea rushwa kwa ajili ya kufanya hujuma.
Alisema anadaiwa kutoshiriki katika kampeni za mgombea
urais mwaka 2010 tuhuma ambazo alidai zimekuwa zikijirudia kila wakati.
Akitoa ufafanuzi wa tuhuma hizo, Zitto alisema kuwa
yeye ndiye kiongozi na mgombea ubunge pekee mwaka 2010 aliyezunguka majimbo 16
kumfanyia kampeni mgombea wa urais wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa na Mkoa wa
Kigoma uliongoza kwa kutoa kura nyingi za urais kuliko mingine kwa kupata
asilimia 46.
Kwa mujibu wa Zitto, tuhuma nyingine iliyoelekezwa
kwake ni madai kuwa alishiriki kuwashawishi baadhi ya wagombea katika baadhi ya
majimbo wajitoe katika uchaguzi ili kuwapisha wagombea wa CCM wapite bila
kupingwa.
Akijibu hilo, Zitto alisema hakuna ushahidi wowote
unaoonyesha hali hiyo, na kwamba aliomba uchunguzi ufanyike kubaini ukweli.
Mbunge huyo alisema pamoja na tuhuma zote, kuna tuhuma
kubwa ya kudaiwa kukidhalilisha chama chake kwa kutoa tamko kwamba hesabu za
chama hicho, hazijakaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali
(CAG) na kwamba chama chake kilimtaka awafahamishe mapema ili wajiandae.
“Kwamba ‘kutowatonya’ kwangu ndio nimekidhalilisha
chama na kukiweka kundi moja na CCM, na kwamba nastahili kuadhibiwa kwani
katika taarifa yangu nilikuwa na nia mbaya na chama chetu. Maelezo yangu
niliyoyatoa na ambayo ningependa kuyakariri hapa kuhusu jambo hili ni kama
ifuatavyo. Utawala bora hautaki mimi kutumia nafasi yangu ya uenyekiti wa PAC
kulinda chama changu na kuonea vyama vingine. Kufanya hivyo ni kuendeleza tabia
zilezile ambazo tunazipinga na ambazo tunapigania kuzibadilisha.
“Napenda kusisitiza kwamba hakuna chama ambacho
kimewahi kukaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG). Natambua
kwamba mahesabu ya chama changu yamekuwa yakikaguliwa na wakaguzi wa nje kwa
utaratibu tuliojiwekea. Lakini matakwa ya kisheria ni kwamba mahesabu ya vyama
vya siasa hayajakaguliwa na CAG, na hili ni kosa la kisheria, bila kujali kosa
hili ni la nani,” alisema Zitto.
Akizungumzia usaliti, alisema kuwa tangu alipoacha
kuchukua posho mwaka 2011 kama ishara ya kuonyesha kwa vitendo msimamo wa chama
chake wa kupinga posho za kukaa na matumizi mengine yasiyofaa katika fedha za
umma, alianza kuitwa msaliti.
Alisema suala la kukataa posho za vikao limo ndani ya
Ilani ya CHADEMA na kwa upande wake kama waziri kivuli wa fedha alikuwa na
wajibu wa kutekeleza jambo hilo kwa vitendo na sio kama alivyotuhumiwa na
Mbunge wa Arusha mjini, Godbless Lema, kwamba anachukua fedha nyingi sehemu
tofauti.
Kuhusu ripoti ya siri iliyosambazwa katika mitandao ya
kijamii, kwamba amehongwa fedha nyingi ili kukihujumu chama chake, alisema kuwa
viongozi wenzake walikana kuuandaa na kuusambaza.
Alisema hoja iliyopo ni kuwa waraka huo umesambazwa na
watu wa usalama kwa kushirikiana na viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Alisema kwa vile chama kimekana kuhusika, tayari
anakusudia kuchukua hatua za kisheria dhidi ya watu wanaohusika iwe ndani au
nje ya chama hicho.
Waraka wa mabadiliko ya uongozi
Akizungumzia waraka wa siri unaoeleza mkakati wa
mabadiliko ya uongozi CHADEMA ulionaswa na kusambazwa kwenye mitandao ya
kijamii, Zitto alisema hajawahi kuuona wala kuusoma na kwa mara ya kwanza
aliusikia kwenye kikao cha Kamati Kuu.
Alipobanwa kueleza kama anakubaliana na mapendekezo ya
waraka huo wa kumtaka agombee uenyekiti wa CHADEMA taifa wakati ukifika, Zitto
alisema kwa bahati mbaya alichelewa kuuona na kama angeupata mapema,
angeyafanyia kazi mapendekezo yake.
“Changamoto hizi tunazopitia zimewahi kupitiwa na
wanasiasa mahiri duniani kama vile akina Mahadhir Mohammed aliyefukuzwa na
baadaye akawa waziri mkuu, Mahindra Gandhi alifukuzwa akiwa waziri mkuu wa nchi
aliondolewa na kwenye uongozi wa chama chake, Zuma, na watu walijua alikwisha
kabisa, lakini matokeo sasa ndiye Rais wa Afrika Kusini, haya ni lazima kupitia
katika kuhakikisha tunajenga demokrasia imara, siasa safi na uongozi bora
katika nchi yetu,” alisema Zitto.
Kuhusu siku 14 alizopewa na Kamati Kuu kwa ajili ya
kutoa utetezi, Zitto alisema hadi sasa hajapata barua ya mashitaka yake na kwa
hali hiyo hajui anatoa utetezi gani.
Dk. Mkumbo amsafisha Zitto na waraka
Kwa upande wake Dk. Mkumbo ambaye alikuwa wa kwanza
kuzungumza, alisema alikiri kuuandaa waraka huo kwa kushirikiana na Mwenyekiti
wa Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba.
Alisema waraka huo uliandaliwa kwa siri bila
kumshirikisha Zitto, na kwamba hajui lolote kwani walipanga kumpelekea endapo
chama kingetangaza tarehe ya uchaguzi.
“Ule waraka ulikuwa wa siri, unaelezea mikakati ya
kuweka mgombea tuliyeamini kwamba ana sifa za kushika nafasi hiyo, baada ya
kukamilisha tungeenda kwake kumwomba agombee, na tungemwonyesha waraka huo
ambao unaainisha udhaifu na uwezo wake wa kuwa kiongozi, na hili ni jambo la
kawaida na sio la uhaini maana tungetumia boksi la kura kumpata kiongozi,”
alisema Dk. Mkumbo.
Katika waraka huo, Zitto alipewa jina la MM, M1
(Mkumbo), M2 ambaye hajulikani hadi sasa na M3 Samson Mwigamba.
Dk. Mkumbo Aliongeza kuwa hata kukiri kwake kwamba
anaujua waraka huo kulikuwa na lengo la kuamini mawazo yake katika kupata
viongozi ndani ya CHADEMA, aliyoeleza kuwa baadhi ya wajumbe waliutafsiri kuwa
ni uhaini.
“Mimi ni miongoni mwa watu ninaoamini kuwa kuna haja
ya kubadilisha uongozi wa juu wa chama, na kwa kuwa tulitambua uchaguzi huu
ungefanyika kabla ya mwaka huu kuisha, tuliandaa sifa za mtu tuliyemuona
anaweza kupokea kijiti na hili hata kwa hao wanaotafsiri ni uhaini limefanyika,
sema kwa upande wao waliamua kuweka mkakati wao katika mitandao ya kijamii,”
alisema Dk. Mkumbo.
Alisema kuwa hawezi kufanya uhaini wala kukihujumu
chama kwani amepewa nafasi nyingi kubwa na kamwe hakuzitumia kukihujumu.
Akitolea mfano, Dk. Mkumbo alisema kuwa yeye ndiye
aliyeandaa Ilani ya Uchaguzi ya CHADEMA katika uchaguzi uliopita, amemaliza
mgogoro wa kupata viti maalumu ndani ya chama nafasi ambazo angeweza kuzitumia
kukihujumu chama.
“Chama kiliniamini na kunipa nafasi nyingi nyeti, na
kama ningekuwa mhujumu nilikuwa na fursa nzuri za kufanya uhujumu huo,
nimeshiriki kuandaa ilani ya chama ya 2010-2015, kuratibu kampeni za mwaka 2010
nikiwa makamu mwenyekiti wa kampeni chini ya Profesa Baregu, na nilishiriki
kutengeneza na kusimamia utaratibu mzuri wa kupata wabunge wa viti maalumu
katika chama chetu. Zote hizi ni nafasi nyeti mno ambazo kamwe huwezi
kumkabidhi mtu ambaye ni ‘mhaini’ na ‘mhujumu’,” alisema.
Alisema kuwa hata sababu ya kutaka kujiuzulu haikuwa
kuogopa aibu ya kufukuzwa, bali ni baada ya kubaini wenzake katika Kamati Kuu
hawakuwa na imani naye.
Subscribe to:
Posts (Atom)