Social Icons

Featured Posts

NDOA YANGU, Ningejua!

NDOA YANGU, Ningejua!

NITAMPATAJE MCHUMBA

Hiki ni kitabu changu kipya cha pili. Vijana wengi wanapata shida katika kuanza na kuendeleza mahusiano yatakayowafikisha katika maisha ya ndoa. WENGI HAWAJUI NINI M,AANA YA MCHUMBA NA MCHUMBA NI MTU GANI Wengi hawajui waanzisheni urafiki sahihi na wa kweli, maisha yanayopaswa kuishi katika urafiki, na uchumba, Hivyo kitabu hiki kinafundisha namna ya kuanzisha urafiki, mambio ya kuchunguza wakati wa urafiki, namna ya kuanzisha uchumba, haki na wajibu wa wachumba na wazazi wao, muda sahihi wa kusihi katika uchumba na hatimaye mambo ya msingi yanayopaswa kukamilisha ama kufuatwa siku ya ndoa. Nawakaribisheni kukisoma watu wa rika zote kwa maana kuna wanandoa wengi ambao hawakufuata misingi sahihi ya kuanzishwa kwa ndoa yao na ndio maana wanalia sasa.

NACHEKA KWA UCHUNGU; TANZANIA NA UONGOZI WA DAMU



Nacheka kwa uchungu Jan 14
Tanzania na uongozi wa damu
NIMELAZIMIKA kuyakumbuka maneno mazito aliyotoa Spika wa Bunge la Tanzania Anne Makinda wakati wa msiba wa Waziri wa Fedha na Uchumi, Dk William Mgimwa aliyefariki mwanzoni mwa mwezi huu nchini Afrika Kusini.
Mbele ya umati wa waombolezaji, Makinda alisema ingekuwa ni amri yake angekufa mtu (kwa namna nyingine waziri) mwingine lakini sio Mgimwa!
Sitaki kurejea namna alivyoshambuliwa kwa maneno, na mijadala ilivyotamalaki katika vyombo vya habari kuhusiana na kauli hiyo.
Kilichonisukuma kukmumbuka maneno ya mama Makinda ni kile kinachoendelea katika wilaya ya Bunda mkoani Mara.
Juzi nililazimika kushuka katika mji huo mdogo nikitoka Musoma kikazi ili niwe kama Yule Thomaso tunayemsoma katika Biblia ambaye alipoambiwa Yesu Kristo amefufuka alikataa hadi amwone kwa macho yake na kugusa makovu ya misumari aliyoshindiliwa msalabani.
Mji mzima wa Bunda unatikisika kwa sasa kutokana na kampeni za uchaguzi mdogo wa diwani wa kata ya Nyasura, baada ya kiti hicho kubaki wazi kufuatia kifo cha aliyekuwa diwani wake Zamberi Ngobayi (Chadema).
Katika kampeni hizi ambazo vyama viwili, Chama cha Mapinduzi (CCM) ambacho ni dhahiri kitamsimamisha Alex Mwikwabe ambaye inadaiwa alipatikana baada ya wagombea wawili wa awali kujitoa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kilichomsimamisha Magambo Webiro zinaendeshwa katika hali inayodhihirisha ubabe, vitisho, hila na ubabaishaji wa hali ya juu.
Nimeshuhudia kampeni za kuchafuana majina, hadhi na heshima ya wagombea zikifanywa na watu wazima kabisa, tena viongozi waliostahili kuionesha jamii kuwa wanawathamini watanzania na wanaheshima matakwa ya watu ya nani awe kiongozi wao.
Nimeshituka zaidi hata baada ya kuona upande mmoja ukijaribu kuwadanganya wapiga kura kwa hoja za kipuuzi za kwamba mgombea wa Chadema ni mganga wa kienyeji na hivyo hafai kuchaguliwa. Tena wanaosema hivyo ni viongozi wengine wa CCM ngazi ya wilaya. Ni hoja ya ajabu kwa sababu hakuna popote katika katiba ambapo mtu anayetibu watu kwa kutumia dawa za kienyeji haruhusiwi kuchaguliwa na kuwa kiongozi. Na kwa kutambua hilo, hao hao wanaosema hivyo, wanasahau kuwa mmoja wa wabunge wake wa bunge la Muungano ni mganga wa kienyeji ambaye katika uchaguzi uliopita alimbwaga daktari mwenye PhD!
Je viongozi wa CCM wa wilaya ya Bunda kwa hoja hiyo ya uganga iliyokanushwa na mhusika mwenyewe, wanataka kusema kuwa wapiga kura Korogwe vijijini walifanya kosa kumchagua mganga wa kienyeji pia Prof Maji Marefu (CCM)kuwa Mbunge wao?

Na katika namna ya kushangaza, baadhi ya viongozi wa CCM sasa wanadaiwa kumwandaa mwana mama mmoja atakayetembea kata nzima kueleza namna mgombea wa Chadema alivyotapeli kwa kutumia uganga wake. Mama huyo anadaiwa kuwa atatangaza jinsi mgombea wa Chadema alivyomtapeli mamilioni ya fedha ili amtibu!
Fikiri tu kwamba suala la uganga limechukua nafasi kubwa katika kampeni huku upande wa pili yaani Chadema, badala ya kupuuza propaganda hizo, nao wamejikita kujibu hoja na kusahau kutangaza sera.
Mbali na hoja ya uganga, wapinzani wa mgombea huyu wameingiza ubaguzi wa kikabila na kimaeneo. Wanajaribu kuwaaminisha wapiga kura kuwa ni hatari kumchagua mgombea huyo kwa sababu sio mzawa wa Nyasura bali mhamiaji aliyefukuzwa kutoka Kata nyingine ya Kunzugu katika kitongoji cha Bokole.
Kana kwamba hoja hizo kwa viongozi wa chama tawala hazina madhala kwa taifa, sasa wanatuhumiwa kuibua jambo baya zaidi ambalo limeanza kuwatisha na kuwapa kiwewe baadhi ya wananchi sio wa Kata ya Nyasura tu bali wilaya nzima ya Bunda.
Hili ni kuwepo kwa tuhuma kwamba zipo njama za kutaka kumkamata mgombea wa upinzani na kumbambika kashfa ya kuiba nyaraka sa siri za serikali.
Inadaiwa kuwa hizo zinazoitwa nyaraka za siri za serikali, zile zinazohusiana na sakata la ardhi katika wilaya ya Bunda.
Kwamba mgombea huyo anatembea na nyaraka za mikataba feki iliyotumika kutaifisha ardhi ya mlima Balili inayosemekana ni mali halali ya shule ya msingi Balili na pia ya Kanisa la Wasabatho.
Inasemekana tuhuma hizo zinawagusa baadhi ya watendaji wa wilaya na mkoa, akiwemo mkuu wa mkoa mmoja hapa nchini.
Nyaraka hizo zinazoitwa za siri, pia zinadaiwa kuwa ni zile zinazofichua kile kinachoitwa tuhuma za waziri mmoja mwandamizi wa serikali ya CCM anayedaiwa kuchukua kwa mabavu sehemu ya ardhi ya shule moja ya sekondari.
Kampeni hizo za uchaguzi wa udiwani kata ya nyasura na zigine 28  nchini utakaofanyika Februari 9,2014, zinaashiria jambo moja tu. Umwagaji wa damu!
Hali sio shwari, viongozi na wanachama wa vyama vya upinzani wameungana na lugha inayotamba sasa ni kwamba..’heri kufa kuliko kuonewa, kuliko kudhulumiwa’
Wapenzi na wanachama wa CCM, nao wanatamba na kauli,….’kwa gharama yoyote lazima tukomboe kata yetu”.
Kauli hizi sio njema hata kidogo hasa zinapopaliliwa kwa nguvu na wanasiasa wakomavu ambao chama chao kinaongoza nchi. Ni kauli ambazo zinaonesha kuwa uwezekano wa kupata viongozi wazuri, wakweli, waadilifu na wachapakazi kama alivyokuwa waziri Mgimwa ambaye Spika Makinda hakutaka afe ni ndoto.
Inatia uchungu zaidi ikiwa leo watanzania wanazidi kushuhudia haki na demokrasia ikikandamizwa kwa gharama za walipa kodi, ili tu watu wanaowataka wachaguliwe kuwa viongozi wa watu hata kama hawana sifa na hawapendwi.
Spika Makinda hata kama kauli yake, haikuwa njema masikioni mwa watu, ajue kuwa chama chake kitasaidia kupatikana kwa viongozi kama marehemu Mgimwa kikiacha mizengwe, hila, ujanja wa kishamba kuendesha kampeni zisizo na mashiko.
Spika Makinda ajue kuwa ni jukumu la CCM kushika na kusimama kama ‘baba wa demokrasia’ na hivyo, kuacha ghiriba za aina yoyote ile katika chaguzi ziwe ndogo ama kubwa.
Kampeni za kudhalilisha, kukomesha na kutesa wasiokuwa wapenzi na wanachama wa CCM na kulazimisha kumweka mtu wa ovyo madarakani kamwe haziwezi kuleta watendaji bora wa serikali. Haziwezi kulipatia taifa madiwani, wabunge na mawaziri bora.
Kampeni zinazosukumwa na ubabe, uonevu, wizi wa kura na hata kumwaga damu za wananchi, haziwezi kamwe kuleta manufaa katika nchi zaidi ya machafuko na umwagaji damu. Kauli ya wana wa Bunda kwamba liwalo na liwe ni ishara ya kwamba watu wamechoka kunyanyaswa. Ni kauli za waliokosa matumaini dhidi ya serikali yao, na hawaitaki.
Spika Makinda atatamani wafe mawaziri wengi ikiwa leo hii katika kampeni za uchaguzi wa marudio ya udiwani, polisi wanatumika kupiga na kufungulia watu kesi za kubambika ili tu CCM ishinde.
Makinda ajue kuwa kama kweli ana uchungu na taifa hili, basi awaambie viongozi wenzake kuwa wanalo jukumu la kuheshimu matakwa ya watu. Wanalo jukumu la kujua na kutekeleza kile watanzania wanachokitaka na sio kuwalazimisha kwa mbinu chafu hata za kumwaga damu.
Bado watanzania wanakumbuka jinsi viongozi wa upinzani walivyofunguliwa mashitaka ya ovyo, kupigwa, kudhalilishwa na kuteswa kisa tu walisimama kuwania uongozi katika chaguzi mbalimbali. Ni viongozi hao hao wa CCM ambao Spika Makinda ni mmojawao, ambao wametumia nguvu na maarifa mengi kuwaaminisha watanzania kuwa wapinzani ni watu wa ovyo, hatari na wanaotakiwa kuogopwa kama ukoma.
Kibaya zaidi, Spika Makinda mwwenyewe mara nyingi tu ameruhusu na kushiriki kukandamiza haki za wapinzani hata katika masuala ya msingi ya nchi. Kiti chake kimeshiriki mara nyingi kunyamazisha sauti za watanzania kupitia wabunge wao.
Wabunge wangapi wa upinzani wamekandamizwa walipokuja na hoja zenye maslahi ya nchi? Wabunge wangapi wa upinzani wameitwa wazushi na waongo walipoibua tuhuma dhidi ya mawaziri? Kama Kiti cha Spika kingeruhusu hoja kujadiliwa na hatua madhubuti kuchukuliwa, leo hii uovu na uvundo katika sekta ya elimu ingefikia hatua hii?
Ni mawaziri wangapi walilindwa na kiti cha Spika pale walipotoa majibu ya uongo, ubabaishaji na yenye hasara kwa taifa? Kwa nini kiti cha spika kiliwakingia kifua alafu leo kiti hicho hicho kinalia? Dhihaka?
Inatia uchungu basi tunaposikiaNi ajabu kwamba leo eti analiachuklia wapinzani na kuwanachama makini na anayeheshimu demokrasia hawezi kufurahia ushindi uliopatikana kwa kukandamiza na kuonea watu.

NACHEKA KWA UCHUNGU;TAIFA LIKIONGOZWA KWA SIASA CHAFU





Nacheka kwa uchungu: jan 8,2014
Taifa likiongozwa kwa siasa chafu
SIKUTAKA kamwe kujadili kinachoendelea ndani ya chama kikuu cha upinzani nchini, ali maarufu kama Chadema.
Sikutaka kwa sababu, taifa langu linayo mambo mengi makubwa ya kujadili na kuyatendea kazi. Mambo ya msingi yanayoweza kuwakomboa wanyonge na umasikini wao wa kukosa elimu bora, afya bora, maisha bora na usalama wa uhakika!
Nimelazimika kuyajadili katika mada ya leo kwa sababu yanayotokea ndani ya Chadema yanaelekea kwa kasi kubwa kuchukua sura ya kitaifa. Sio siri kwamba sasa yanashabikiwa kwa waziwazi ama kwa kificho na umma wa watanzania, baadhi yao wakiwa wanasiasa wakongwe, wakubwa kabisa na wengine wakiwa watendaji waandamizi ndani ya serikali ya CCM.
Mtu waweza kucheka kwa uchungu unapofikiria siasa za Tanzania zilivyo kwa sasa. Ni kama igizo la mwendawazimu! Linaloumiza zaidi, ni kwamba ‘upuuzi’ huu wa siasa ninazothubutu kuziita za kishamba zinaligharimu taifa na kuleta hasara kubwa ambayo kwa bahati mbaya, hakuna anayeiona.
Zinagharimu muda wa watu kufanya kazi za kuzalisha mali. Zinagharimu fedha halisi za watanzania kwa kuwa, wanaoziendesha wanatumia fedha kwa kuliwasiliana, kulipana posho na hata ‘kuhongana’ ili tu mambo wanayotaka yaweze kwenda.
Tukio la kuvuliwa madaraka wa Zitto Kabwe na tishio la kunyang’anywa uanachama sio la kwanza katika siasa za Tanzania. Ukiachilia mbali wale waliofikwa na jambo linaloelekea kumtokea Zitto ndani ya upinzani, wapo waliopatwa na hayo enzi za TANU na CCM chini ya utawala wa siasa ya chama kimoja.
Wengine walilazimishwa kujiondoa wenyewe huku wakificha sababu halisi za kujivua kwao madaraka. Wakabaki wanaishi kama wanachama wa kawaida kwa miaka mingi. Wapo waliorudishiwa nafasi za uongozi baada ya kupita miaka kadhaa.
Tunakumbuka jinsi wanasiasa na viongozi wengine walivyotimuliwa uongozi na uanachama baada ya kugoma kujiuzulu wenyewe. Wapo baadhi kwa hofu ya usalama wa maisha yao, walilazimika kuondoka nchini, na wengine waliendelea kuishi kwa kufanya shughuli nyingine za maendeleo na maisha yao yakasonga mbele kwa mafanikio makubwa kuliko walivyokuwa katika ulingo wa siasa.
Yaliyopendeka haya, watanzania hawakusikia malumbano yaliyojaa matusi, kashifa, dharau, udhalilishaji na aibu kubwa kama tunayoshuhudia sasa.
Sitaki kusimama upande wowote, lakini swali ambalo watanzania wanatakiwa kujiuliza bila unafiki ndani yake, ni kwamba iweje leo wanaotuhumiwa kusaliti chama chao, ndio wanaibuka na kututangazia ‘uozo’ wa viongozi wenzao ndani ya chama?
Kiongozi anayejaribu kuwashawishi watanzania waamini kuwa wenzake pia ni waovu kiasi cha kuzua hata utata wa kumiliki nyumba za umma, kana kwamba watendaji wakuu wa shirika hilo nao ni wapuuzi kiasi cha kuingia katika mkataba tata, anatushawishi tumuaminije?
Watu makini wanaposikia kwa mfano, watuhumiwa wa kinachoitwa usaliti sasa wakirusha kete wakidai eti  kiongozi fulani naye alipewa fedha mwaka 2005 wakati wa uchaguzi mkuu, wanajiuliza huyu anayetoa tuhuma hizi leo alikuwa wapi kuyasema miaka yote hiyo?
Ikiwa kwa mfano pana ukweli wa tuhuma za viongozi wenzake anaowataja kupokea fedha kutoka kwa kiongozi wa CCM, sababu zipi zilimfanya afumbe mdomo miaka yote hiyo, hadi leo anazitoa baada ya kutishiwa kufukuzwa? Mtu gani mwenye akili timamu atamwamini tena mwanasiasa wa aina hii. Mtu gani mwenye busara ataendelea kusadiki yale anayosema sasa na yale atakayotamka?
Lakini kinachotisha zaidi, sasa zinapotolewa tuhuma zinazolenga kubainisha kuwa hata kifo cha Chacha Wangwe kilikuwa na ‘mkono’ wa mtu!

Ni siasa zinazotia uchungu mkubwa kuona kwamba, kiongozi anayetaka watu wamwamini anatangaza waziwazi na kurejea leo mwaka 2014
matukio ya 2005! Alikuwa wapi siku zote? Kipi kilimzuia asiseme? Na kwa nini aseme leo baada ya kutimuliwa?  Ina maana kama asingechukuliwa hatua angenyamaza? Na kwa nini alikuwa bingwa wa kurusha makombora kwa viongozi wa CCM huku akijua (kama ni kweli) kwamba na wenzake wanapokea fedha kutoka huko huko CCM?
Nacheka kwa uchungu kuona mtu msomi, anayetaka demokrasia ya kweli anaibuka na upuuzi huu leo hii, na katika nyakati ambazo watanzania wamepigika kimaisha. Ni watu wasiofikiri sawa sawa watakaomuamini tena. Ataamini tu na watu waliochoka kimaisha, wanaokubali kuwa kapu la kubeba kila aina ya umbea, na walio tayari kusema, kutenda na kushabikia lolote na chochote kwa sababu wanajua wanapewa pesa. Watu wa ovyo ovyo tu!
Inatia hasira kuona kuwa wakati tunawajibika kujadili mambo mazito ya mustakhabari wa taifa letu, anasimama kiongozi anayetaka kuwalisha watanzania ajenda za mambo binafsi ya mtu na familia yake.
Ni upuuzi mkubwa kwa watu waliokomaa kisiasa kujadili uzinzi bungeni ama kwenye majukwaa, bila ushahidi makini na huku ukitambua kuwa jambo hilo sio tu litamdhalilisha anayetuhumiwa, bali familia yake, ndugu na jamaa zake.
Zitto anataka kuwaambia watanzania kuwa wanahitaji kujua nani mzinzi na nani mtakatifu? Yaani watanzania kweli wanafikishwa mahali pa kulishwa utumbo wa inzi kiasi hiki?
Tuseme ukweli bila unafiki. Hivi nani anastahili kulalamika katika hilo linaloitwa sakata la uzinzi wa Mbowe? Ni Mwigulu Nchemba aliyesema bungeni na Zitto anatutangazia sasa, au mume wa mbunge huyo na mke wa Mbowe? Kwa nini wamenyamaza? Mtu makini, atanyamaza. Hawezi kujibu ujinga. Ndivyo walivyofanya mke wa Mbowe na Mume wa Joyce!
Lakini pia mtu unajiuliza, hawa wanaowatuhumu wenzao kwa uzinzi, wao wana usafi kiasi gani basi? Ni malaika wao?
Katika haya yanayoendelea, inahuzunisha zaidi watanzania wanapobaini kuwa nyuma ya mgogoro huu, kuna mkono wa baadhi ya wanasiasa waliofilisika wa upande wa pili.
Tulishuhudia namna baadhi ya wanasiasa na viongozi wa CCM wakitoa shutuma, matusi na lawama kwa uongozi wa juu wa Chadema kwa kumwondoa Zitto katika madaraka. Swali la kujiuliza, kiliwauma nini? Walikuwa na maslahi gani na nafasi za kiongozi huyo ndani ya Chadema? 
Hivi akitokea mtu akasema, waliumia kwa sababu walijua mtu aliyempandikiza amebainika na ndio maana wanaumia atakuwa amekosea? Nisaidieni hivi Yule waziri wa serikali aliyetamba kuwa Chadema kitakufa kabla ya 2015, alikuwa anajivunia nini?
Ndio alitamka waziwazi na tukasikia akitamba kuwa atahakikisha chama hicho pinzani kinakufa! Waziri mzima, ambaye angetegemewa asimame na kuwaeleza watanzania kuwa nia yake ya chama chake ni kuhakikisha adui ujinga, njaa, maradhi na ufujaji wa mali ya umma vinakufa kabla ya 2015, anakurupuka na kusema Chadema inakufa, kana kwamba ndio kansa ya maendeleo yetu anastahili kuendelea kuwa madarakani kweli kama tuko makini na uhai wa taifa letu?
Je, ni kweli kwamba taifa hili limefikishwa mahali pa watu wanakufa hospitalini kwa kukosa dawa, watoto wanafeli ovyo kwa kukosa elimu bora, walimu wanapiga mihuri ardhini (wanatembea peku) na madaktari wanagoma kwa sababu kuna chama kinaitwa Chadema?
Leo hii mangapi yanatokea hapa nchini, tena mabaya yanayoumiza na kuua utu na heshima yetu kitaifa na kimataifa?  Leo hakuna usalama wa uhakika hapa nchini. Mtu unalala kwa hofu, unatembea kwa hofu, unakunywa kwa hofu,na katika hali isiyoweza kusemeka sasa wakristo wanakwenda makanisani kwa hofu kubwa!
Hawana uhakika wa kurejea nyumbani kwa usalama.  Wanasali huku wanalindwa utafikiri ni wafungwa. Wamepigwa mabomu kanisa, wakiimba, wamepigwa risasi wakienda kusali, wakamwagiwa tindikali bila hatia yoyote.
Leo watu wanakwiba fedha za umma mchana na usiku. Wanahabari tunawafichua, lakini hatuoni hawa wanaoshambulia wenzao wakichukua hatua hata za kukemea tu. Hawaoni uchafu unaofanywa ndani ya nchi. Hawaoni wanyama wanavyoangamizwa. Wao ni kushambuliana tuu!
Badala ya watu kujadili haya, na kujua nani katufikisha hapa achukuliwe hatua, watu wanaibuka na visa vya ovyo na tuhuma za kitoto kabisa za fulani anazini na mke wa fulani. Si mwacheni aliyechukuliwa mke ama mume alalamike?
Watu wazima, wasomi kabisa na watu wanaoonekana kuwa na busara, wanashinda kutwa nzima wakihangaika namna ya kuwazushia wengine tuhuma za kipuuzi na kujiapiza namna watakavyoizika chadema.
Nacheka kwa uchungu kila ninapowaza aina ya viongozi na wanasiasa sasa hawana muda wa kutafuta mbinu za kuinua uchumi wa taifa letu, njia za kuwafanya watanzania waondokane na umasikini,kuokoa rasilimali za nchi zinazoporwa usiku na mchana, badala yake kama mazuzu wanahangaika na vyama vya upinzani na kuendesha siasa za kuchafuana!

KAPUYA AIGONGANISHA POLISI



SIKU chache baada ya Mbunge wa Urambo Magharibi, Profesa Juma Kapuya (CCM), kudaiwa kutoweka nchini kukwepa mkono wa sheria dhidi ya tuhuma za kutishia kumuua binti anayedaiwa kumbaka, vigogo wa polisi wanadaiwa kuhusika kumsaidia kutimkia nje, Tanzania Daima limedokezwa.
Habari ambazo gazeti hili limezipata, zinaeleza kuwa siku mbunge huyo akikamilisha taratibu za kusafiri, ndiyo siku ambayo Jeshi la Polisi Mkoa wa Kinondoni lilikuwa limekamilisha kufungua jalada la tuhuma zake na liliweka mtego wa kumnasa.
“Wakati Polisi Kinondoni wakiweka mtego wa kumnasa, baadhi ya polisi walimjulisha na hata kumsaidia kuhakikisha anasafiri nje ya nchi,” alisema mmoja wa maofisa wa juu wa polisi nchini.
Hata hivyo, kuna utata na kauli zinazopingana kuhusu mbunge huyo. Taarifa nyingine zinasema kuwa mbunge huyo ambaye amepata kuwa waziri, anadaiwa kusafiri kwenda nchini Sweden kwa masuala ya kikazi, na kwamba atakuwepo huko kwa muda usiopungua mwezi mmoja.
Chanzo kingine kimedokeza kuwa mbunge huyo alidai ametumwa kazi na kigogo mmoja serikalini na atakuwepo nchini humo miezi miwili hadi mitatu.
Hata hivyo, haijajulikana kazi anayokwenda kuifanya Kapuya ingawa kuna taarifa safari hiyo imelenga kutuliza upepo mbaya wa kuandamwa na tuhuma za ubakaji ambazo zipo polisi hivi sasa.
Tayari Profesa Kapuya alishafunguliwa jalada namba OB/RB/21124/13 katika Kituo cha Polisi Oysterbay, jijini Dar es Salaam juzi.
Hata hivyo Jeshi la Polisi limesisitiza kuwa linamsaka mbunge huyo ndani na nje ya nchi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camilius Wambura, alikaririwa juzi kuwa watamtafuta Kapuya nchi yoyote atakayokwenda iwapo tuhuma dhidi yake zitathibitika.
Alisema mtandao wa polisi ni mkubwa, hivyo si rahisi kwa mtuhumiwa yeyote kuukwepa mkono wa sheria endapo itahitajika kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.
“Sisi tunashirikiana na polisi wa nchi mbalimbali duniani, ndiyo maana inakuwa rahisi kwa mtuhumiwa aliyetoroka nchi fulani kukamatwa nyingine na kurejeshwa kwao.
“Nataka niwaondoe hofu wale wote wanaodhani polisi haiwezi kumkamata mtu akikimbia nchini, tuna mkono mrefu sana, na hatufanyi kazi kinyume na taratibu zetu,” alisema.
Kamanda Wambura pia alikiri polisi kufungua jalada la Kapuya, huku akiweka wazi kuwa kinachofanyika hivi sasa ni uchunguzi wa tuhuma zake.
Alisema miongoni mwa maeneo wanayoyafanyia uchunguzi ni kubaini kama ujumbe ulio katika simu ya binti anayedai kubakwa na kutishiwa maisha unatoka katika simu ya mbunge huyo.
“Tumefungua jalada, lipo kwa ajili ya uchunguzi na tukibaini kuwa ni nani anahusika na tuhuma hizo tutamsaka na kumkamata popote alipo,” alisema Wambura.
Gazeti hili limekuwa likiandika namba ya simu ya Prof. Kapuya ambayo huwa anaitumia kutuma ujumbe wa vitisho kwa binti huyo, ingawa kuna vyombo vingine vya habari viliamua kuandika kwa mtazamo tofauti na kumtuhumu dada wa binti aliyebakwa kuwa ni mtu mzima na kuwa ana uhusiano na Kapuya, na wana watoto.
Simu hiyo namba 0784993930 inayodaiwa kumilikiwa na Profesa Kapuya, mbali ya kutuma ujumbe mfupi wa maneno ya kutishia kuua, pia ndiyo inayodaiwa kutumika kutuma pesa kwa njia ya mtandao kwenda kwa binti huyo.
Tangu gazeti hili lianze kuandika tuhuma hizi nzito, kumekuwapo na kusuasua kwa mtuhumiwa huyo kutiwa hatiani na Jeshi la Polisi.
Harakati za kufungua jalada dhidi ya Kapuya zilizoanza wiki iliyopita ziliendelea hadi juzi ambapo polisi walitumia zaidi ya saa 12 kumhoji binti huyo anayedaiwa kubakwa ili kupata ukweli wa sakata hilo.
Akiwa polisi, binti huyo alikutana na Mkuu wa Polisi Wilaya ya Kipolisi ya Oysterbay (OCD) na OC-CID wake na kutoa maelezo ya awali kabla ya viongozi hao kumruhusu ayaweke malalamiko yake katika maandishi kwa ajili ya kufunguliwa mashitaka.

SIHAMI CHADEMA-ZITTO



HATIMAYE Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe na Mjumbe wa Kamati Kuu (CC), Dk. Kitila Mkumbo waliovuliwa uongozi ndani ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), wamevunja ukimya.
Katika mkutano wao na wahariri na waandishi wa vyombo mbalimbali vya habari, Zitto ambaye alikuwa Naibu Katibu Mkuu CHADEMA, ameapa kuwa hayuko tayari kuondoka ndani ya chama hicho na atakuwa mtu mwisho kuondoka.
Wakati Zitto akiapa kwamba hayuko tayari kuondoka CHADEMA, Dk. Mkumbo ambaye amekuwa mshauri mkuu wa chama hicho maarufu nchini, amesema kuwa kile kinachoitwa uhaini ndani ya CHADEMA ni wasiwasi wa siasa za ushindani kwa watu wasiotaka mabadiliko.
“Wengi walifikiri nikija hapa leo nitajibu mapigo na kutoa uamuzi mgumu. Mimi sitoki CHADEMA, wanaotaka nitoke, wanitoe wao, na hiki kinachoendelea ndani ya chama chetu ni mapambano ya kukuza demokrasia dhidi ya wahafidhina, ni mapambano ya wanaopenda siasa safi dhidi ya wale wanaotukuza siasa za maji taka,” alisema Zitto.
Akieleza sababu za kutokujitoa CHADEMA, Zitto alisema zaidi ya nusu ya maisha yake yamekuwa CHADEMA, kwani alijiunga tangu alipokuwa na miaka 16 hadi sasa ana miaka 37, na amekabiliana na vitisho mbalimbali dhidi ya wasiotaka mageuzi.
“Nataka niwaeleze wanachama wa CHADEMA kwamba mimi sitokuwa sababu ya CHADEMA kuvunjika, kimenilea na kunifikisha hapa na ningependa na mwanangu siku moja awe mwanachama wa CHADEMA, na huu unaoitwa usaliti kwangu dhidi ya CHADEMA ni sawa na mimi kujikata mguu wangu, sitoweza kufanya hivyo,” alisema Zitto.
Mbunge huyo ambaye amepata umaarufu mkubwa tangu alipoingia bungeni, alieleza kuumizwa na shutuma nyingi ambazo zimekuwa zikielekezwa kwake kwa muda mrefu.
Alisema amekuwa akiItwa msaliti, mnafiki, mla rushwa akihongwa kwa ajili ya kukisaliti chama.
“Naomba wanachama wanielewe, nimejiunga na chama hiki nikiwa na miaka 16, ninaposingiziwa, naumia sana, nimefanya kazi ya kuchomeka milingoti ya bendera za chama kwa viongozi wanaofika katika kijiji chetu, ninapozushiwa naumia, nimefanya kazi zangu za kibunge kwa weledi mkubwa kwa nia ya kukitumikia na kukipandisha chama changu, ninaambiwa ninakihujumu, inaniuma sana,” alisema.
Zitto ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Hesabu za Serikali (PAC), alisema akiwa mwanasiasa kijana na binadamu, anaamini ana makosa kwa kuwa hakuna binadamu aliye mkamilifu, na kwamba upungufu wake unapaswa kupimwa na mema aliyoyafanya.
Ataja tuhuma zake
Akizungumzia tuhuma zilizomfanya apokwe nyadhifa zake zote na kubaki kuwa mwanachama, Zitto alisema kuna upotoshaji mkubwa wa taarifa kwani tuhuma alizoambiwa ndani ya Kamati Kuu ni tofauti na zilizotolewa kwa waandishi wa habari.
Alisema tuhuma zote zimekuwa katika taswira mbili zinazomuonyesha kuwa ni mbinafsi na mtu anayetumiwa kukisaliti chama kwa kupokea rushwa kwa ajili ya kufanya hujuma.
Alisema anadaiwa kutoshiriki katika kampeni za mgombea urais mwaka 2010 tuhuma ambazo alidai zimekuwa zikijirudia kila wakati.
Akitoa ufafanuzi wa tuhuma hizo, Zitto alisema kuwa yeye ndiye kiongozi na mgombea ubunge pekee mwaka 2010 aliyezunguka majimbo 16 kumfanyia kampeni mgombea wa urais wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa na Mkoa wa Kigoma uliongoza kwa kutoa kura nyingi za urais kuliko mingine kwa kupata asilimia 46.
Kwa mujibu wa Zitto, tuhuma nyingine iliyoelekezwa kwake ni madai kuwa alishiriki kuwashawishi baadhi ya wagombea katika baadhi ya majimbo wajitoe katika uchaguzi ili kuwapisha wagombea wa CCM wapite bila kupingwa.
Akijibu hilo, Zitto alisema hakuna ushahidi wowote unaoonyesha hali hiyo, na kwamba aliomba uchunguzi ufanyike kubaini ukweli.
Mbunge huyo alisema pamoja na tuhuma zote, kuna tuhuma kubwa ya kudaiwa kukidhalilisha chama chake kwa kutoa tamko kwamba hesabu za chama hicho, hazijakaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na kwamba chama chake kilimtaka awafahamishe mapema ili wajiandae.
“Kwamba ‘kutowatonya’ kwangu ndio nimekidhalilisha chama na kukiweka kundi moja na CCM, na kwamba nastahili kuadhibiwa kwani katika taarifa yangu nilikuwa na nia mbaya na chama chetu. Maelezo yangu niliyoyatoa na ambayo ningependa kuyakariri hapa kuhusu jambo hili ni kama ifuatavyo. Utawala bora hautaki mimi kutumia nafasi yangu ya uenyekiti wa PAC kulinda chama changu na kuonea vyama vingine. Kufanya hivyo ni kuendeleza tabia zilezile ambazo tunazipinga na ambazo tunapigania kuzibadilisha.
“Napenda kusisitiza kwamba hakuna chama ambacho kimewahi kukaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG). Natambua kwamba mahesabu ya chama changu yamekuwa yakikaguliwa na wakaguzi wa nje kwa utaratibu tuliojiwekea. Lakini matakwa ya kisheria ni kwamba mahesabu ya vyama vya siasa hayajakaguliwa na CAG, na hili ni kosa la kisheria, bila kujali kosa hili ni la nani,” alisema Zitto.
Akizungumzia usaliti, alisema kuwa tangu alipoacha kuchukua posho mwaka 2011 kama ishara ya kuonyesha kwa vitendo msimamo wa chama chake wa kupinga posho za kukaa na matumizi mengine yasiyofaa katika fedha za umma, alianza kuitwa msaliti.
Alisema suala la kukataa posho za vikao limo ndani ya Ilani ya CHADEMA na kwa upande wake kama waziri kivuli wa fedha alikuwa na wajibu wa kutekeleza jambo hilo kwa vitendo na sio kama alivyotuhumiwa na Mbunge wa Arusha mjini, Godbless Lema, kwamba anachukua fedha nyingi sehemu tofauti.
Kuhusu ripoti ya siri iliyosambazwa katika mitandao ya kijamii, kwamba amehongwa fedha nyingi ili kukihujumu chama chake, alisema kuwa viongozi wenzake walikana kuuandaa na kuusambaza.
Alisema hoja iliyopo ni kuwa waraka huo umesambazwa na watu wa usalama kwa kushirikiana na viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Alisema kwa vile chama kimekana kuhusika, tayari anakusudia kuchukua hatua za kisheria dhidi ya watu wanaohusika iwe ndani au nje ya chama hicho.
Waraka wa mabadiliko ya uongozi
Akizungumzia waraka wa siri unaoeleza mkakati wa mabadiliko ya uongozi CHADEMA ulionaswa na kusambazwa kwenye mitandao ya kijamii, Zitto alisema hajawahi kuuona wala kuusoma na kwa mara ya kwanza aliusikia kwenye kikao cha Kamati Kuu.
Alipobanwa kueleza kama anakubaliana na mapendekezo ya waraka huo wa kumtaka agombee uenyekiti wa CHADEMA taifa wakati ukifika, Zitto alisema kwa bahati mbaya alichelewa kuuona na kama angeupata mapema, angeyafanyia kazi mapendekezo yake.
“Changamoto hizi tunazopitia zimewahi kupitiwa na wanasiasa mahiri duniani kama vile akina Mahadhir Mohammed aliyefukuzwa na baadaye akawa waziri mkuu, Mahindra Gandhi alifukuzwa akiwa waziri mkuu wa nchi aliondolewa na kwenye uongozi wa chama chake, Zuma, na watu walijua alikwisha kabisa, lakini matokeo sasa ndiye Rais wa Afrika Kusini, haya ni lazima kupitia katika kuhakikisha tunajenga demokrasia imara, siasa safi na uongozi bora katika nchi yetu,” alisema Zitto.
Kuhusu siku 14 alizopewa na Kamati Kuu kwa ajili ya kutoa utetezi, Zitto alisema hadi sasa hajapata barua ya mashitaka yake na kwa hali hiyo hajui anatoa utetezi gani.
Dk. Mkumbo amsafisha Zitto na waraka
Kwa upande wake Dk. Mkumbo ambaye alikuwa wa kwanza kuzungumza, alisema alikiri kuuandaa waraka huo kwa kushirikiana na Mwenyekiti wa Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba.
Alisema waraka huo uliandaliwa kwa siri bila kumshirikisha Zitto, na kwamba hajui lolote kwani walipanga kumpelekea endapo chama kingetangaza tarehe ya uchaguzi.
“Ule waraka ulikuwa wa siri, unaelezea mikakati ya kuweka mgombea tuliyeamini kwamba ana sifa za kushika nafasi hiyo, baada ya kukamilisha tungeenda kwake kumwomba agombee, na tungemwonyesha waraka huo ambao unaainisha udhaifu na uwezo wake wa kuwa kiongozi, na hili ni jambo la kawaida na sio la uhaini maana tungetumia boksi la kura kumpata kiongozi,” alisema Dk. Mkumbo.
Katika waraka huo, Zitto alipewa jina la MM, M1 (Mkumbo), M2 ambaye hajulikani hadi sasa na M3 Samson Mwigamba.
Dk. Mkumbo Aliongeza kuwa hata kukiri kwake kwamba anaujua waraka huo kulikuwa na lengo la kuamini mawazo yake katika kupata viongozi ndani ya CHADEMA, aliyoeleza kuwa baadhi ya wajumbe waliutafsiri kuwa ni uhaini.
“Mimi ni miongoni mwa watu ninaoamini kuwa kuna haja ya kubadilisha uongozi wa juu wa chama, na kwa kuwa tulitambua uchaguzi huu ungefanyika kabla ya mwaka huu kuisha, tuliandaa sifa za mtu tuliyemuona anaweza kupokea kijiti na hili hata kwa hao wanaotafsiri ni uhaini limefanyika, sema kwa upande wao waliamua kuweka mkakati wao katika mitandao ya kijamii,” alisema Dk. Mkumbo.
Alisema kuwa hawezi kufanya uhaini wala kukihujumu chama kwani amepewa nafasi nyingi kubwa na kamwe hakuzitumia kukihujumu.
Akitolea mfano, Dk. Mkumbo alisema kuwa yeye ndiye aliyeandaa Ilani ya Uchaguzi ya CHADEMA katika uchaguzi uliopita, amemaliza mgogoro wa kupata viti maalumu ndani ya chama nafasi ambazo angeweza kuzitumia kukihujumu chama.
“Chama kiliniamini na kunipa nafasi nyingi nyeti, na kama ningekuwa mhujumu nilikuwa na fursa nzuri za kufanya uhujumu huo, nimeshiriki kuandaa ilani ya chama ya 2010-2015, kuratibu kampeni za mwaka 2010 nikiwa makamu mwenyekiti wa kampeni chini ya Profesa Baregu, na nilishiriki kutengeneza na kusimamia utaratibu mzuri wa kupata wabunge wa viti maalumu katika chama chetu. Zote hizi ni nafasi nyeti mno ambazo kamwe huwezi kumkabidhi mtu ambaye ni ‘mhaini’ na ‘mhujumu’,” alisema.
Alisema kuwa hata sababu ya kutaka kujiuzulu haikuwa kuogopa aibu ya kufukuzwa, bali ni baada ya kubaini wenzake katika Kamati Kuu hawakuwa na imani naye.