KADA mkongwe wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambaye
ni muasisi wa kundi la wabunge waliokuwa wakishinikiza hoja ya Serikali ya
Tanganyika, maarufu kama G55, Njelu Kasaka, ameibuka na kuwashangaa wabunge
wa chama hicho kupinga hoja ya muundo wa serikali tatu wakati ni yao tangu
awali ya kudai mabadiliko ya muundo wa Muungano.
Kasaka aliongeza kuwa hata Baba wa Taifa, hayati
Mwalimu Julius Nyerere, aliona umuhimu wa muundo huo wa serikali tatu,
isipokuwa alitoa tahadhari kuwa kwa aina ya uendeshaji wa serikali uliokuwa
unaendekezwa kwa kuogopana na kulindana Muungano usinge dumu.
Mwanasiasa huyo ambaye amewahi kuwa mbunge wa
Lupa, alitoa kauli hiyo jana katika mahojiano maalumu na gazeti hili jijini
Dar es Salaam, huku akiwaasa wabunge hasa wa CCM kuacha mzaha katika suala
la katiba, akisema ni muhimu na lisipoangaliwa kwa umakini linaweza
kuliingiza taifa katika machafuko.
“Wabunge wote watakapokuwa Dodoma wajue wana
dhamana kubwa sana, wasifanye mzaha na suala la katiba, ni suala muhimu
kwani katiba mbaya inaweza kuangamiza. Suala la kubadilishwa katiba
halifanyiki kama wanavyobadili sheria.”
“Wanapitisha leo, rais anasaini anawarudishia
wakafanye mabadiliko, si kitu rahisi. Wakumbuke kuwa wakiamua vibaya
wataangamiza taifa kwa muda mrefu na wakiamua vizuri watalisaidia taifa,”
alisema.
Kasaka alitumia muda mwingi kuelezea historia ya
kundi hilo (G55), akisema lilianzishwa baada ya manung’uniko ya Wazanzibari
kuwa wanaonewa na Serikali ya Muungano.
“Wazanzibari walisema kuwa Serikali ya Tanganyika
imejifanya kuwa ni ya muungano ili kuitawala Zanzibar bila ridhaa ya
Wazanzibari na kwamba ilizuia Serikali ya Zanzibar kufanya mambo yake.
“Serikai tatu ni wazo la CCM, kwani wakati
tunalianzisha vyama vya upinzani vilikuwa vingine havijasajiliwa na
vilivyokuwapo havikuwa na wabunge, vilikuwa makundi ya wanaharakati wakati
huo, waliunga mkono kutaka mabadiliko,” aliasa.
Kasaka aliongeza kuwa hali ya wakati huo ilimuudhi
kwani mtu wa Bara alikuwa akitaka kwenda Zanzibar inabidi awe na hati ya
kusafiria na kuchukuliwa kama mgeni wakati wanazungumzia nchi moja.
“Nilipeleka hoja bungeni, ikaungwa mkono na Matheo
Qares, Arcado Ntagazwa, Mussa Nkhangaa, William Mpiluka (marehemu),
Sebastian Kinyondo (marehemu) na Jenerali Ulimwengu. Kwa ujumla niliungwa
mkono na wabunge 55, ingawa baadaye wabunge karibu wote walituunga mkono
tukaambiwa halimo katika sera za CCM,” alisema.
Kwa mujibu wa mwanasiasa huyo, serikali tatu au
mabadiliko ya muundo wa Muungano kutoka wakati huo hadi sasa hayaepukiki.
Kwamba, mtazamo wa Wazanzibari wanasema wapo
tayari kutofautiana katika mambo yote kisiasa au kiitikadi lakini hoja ya
Uzanzibari (identity ya nchi) haifi hadi utakapomwondoa Mzanzibari wa
mwisho.
“Kumbuka kuwa aina ya Watanzania wa sasa si wale
wa miaka 30 iliyopita, wakati huo walikuwa wanazaliwa, ila sasa wao ndio
wasomi na wasemaji katika mambo mengi.
“Nawatahadharisha wabunge waangalie idadi ya
Watanzania sasa si ile iliyokuwapo, mwamko wa sasa si ule wa miaka
iliyopita. Mwaka 1993 -1995 watu waliokuwa wanajitambulisha ni wapinzani
walikuwa wanazomewa, sasa wale wanaojitambulisha CCM ndio wanaozomewa,
wakubali mabadiliko, serikali tatu haziepukiki na hii ilikuwa hoja ya
wabunge wa CCM,” alisema.
Kisaka alisema wabunge wakubali kufanya
marekebisho ya sheria iliyorejeshwa na rais, kwani serikali haiwezi
kujitungia katiba, hivyo wabunge wote hasa wa CCM wakubali suala la
serikali tatu, wafanye marekebisho mazuri ili kuondoa uwezekano wa mgogoro
mkubwa kati ya Bara na Zanzibar.
Alimpongeza Rais Jakaya Kikwete kwa kauli yake
aliyoitoa mjini Dodoma hivi karibuni ya kukemea vitendo vya rushwa ndani ya
chama, akisema itawaathiri kwenye Uchaguzi Mkuu ujao ikiwa
hawatajirekebisha.
Alisema anakubaliana na Kikwete kwa asilimia mia
moja kwamba CCM isipoacha rushwa itaanguka, na isipoacha upendeleo na
kulazimisha wagombea wasiokubalika vilevile itakufa.
Kasaka alimtaka Rais Kikwete kuchukua hatua,
asiishie kusema. Kwamba, anaweza kutumia Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na
Rushwa (TAKUKURU) kwa masuala ya kisheria na mengine ya kiutendaji yapo
chini ya uwezo wake.
“CCM watu hawachukuliani hatua, Makamu Mwenyekiti
(Bara), Philip Mangula, alilalamikia rushwa aliposhindwa uenyekiti wa Mkoa
wa Iringa, lakini aliishia kusema kuwa uongozi katika chama unapatikana
kama bidhaa gulioni, na alipochaguliwa kuwa makamu mwenyekiti wala hajawahi
kuchukua hatua,” alisema.
Kasaka aliongeza kuwa hadi Rais Kikwete ameamua
kujitoa kuyasemea hayo nje, ni kwa sababu ndani ya CCM watu si wasikivu,
wengine wana dharau.
“Ukiona mke na mume wanatukanana hadharani ujue
ndani wametukanana vya kutosha na imeshindikana, wameonyana imeshindikana,
ndiyo maana wanakuja hadharani kuja kukemeana mbele yetu,” alisema.
|
No comments:
Post a Comment