SIKU chache baada ya Mbunge wa Urambo Magharibi,
Profesa Juma Kapuya (CCM), kudaiwa kutoweka nchini kukwepa mkono wa sheria
dhidi ya tuhuma za kutishia kumuua binti anayedaiwa kumbaka, vigogo wa polisi
wanadaiwa kuhusika kumsaidia kutimkia nje, Tanzania Daima limedokezwa.
Habari ambazo gazeti hili limezipata, zinaeleza kuwa
siku mbunge huyo akikamilisha taratibu za kusafiri, ndiyo siku ambayo Jeshi la
Polisi Mkoa wa Kinondoni lilikuwa limekamilisha kufungua jalada la tuhuma zake
na liliweka mtego wa kumnasa.
“Wakati Polisi Kinondoni wakiweka mtego wa kumnasa,
baadhi ya polisi walimjulisha na hata kumsaidia kuhakikisha anasafiri nje ya
nchi,” alisema mmoja wa maofisa wa juu wa polisi nchini.
Hata hivyo, kuna utata na kauli zinazopingana kuhusu
mbunge huyo. Taarifa nyingine zinasema kuwa mbunge huyo ambaye amepata kuwa
waziri, anadaiwa kusafiri kwenda nchini Sweden kwa masuala ya kikazi, na kwamba
atakuwepo huko kwa muda usiopungua mwezi mmoja.
Chanzo kingine kimedokeza kuwa mbunge huyo alidai
ametumwa kazi na kigogo mmoja serikalini na atakuwepo nchini humo miezi miwili
hadi mitatu.
Hata hivyo, haijajulikana kazi anayokwenda kuifanya
Kapuya ingawa kuna taarifa safari hiyo imelenga kutuliza upepo mbaya wa
kuandamwa na tuhuma za ubakaji ambazo zipo polisi hivi sasa.
Tayari Profesa Kapuya alishafunguliwa jalada namba OB/RB/21124/13
katika Kituo cha Polisi Oysterbay, jijini Dar es Salaam juzi.
Hata hivyo Jeshi la Polisi limesisitiza kuwa linamsaka
mbunge huyo ndani na nje ya nchi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camilius Wambura,
alikaririwa juzi kuwa watamtafuta Kapuya nchi yoyote atakayokwenda iwapo tuhuma
dhidi yake zitathibitika.
Alisema mtandao wa polisi ni mkubwa, hivyo si rahisi
kwa mtuhumiwa yeyote kuukwepa mkono wa sheria endapo itahitajika kufikishwa
kwenye vyombo vya sheria.
“Sisi tunashirikiana na polisi wa nchi mbalimbali
duniani, ndiyo maana inakuwa rahisi kwa mtuhumiwa aliyetoroka nchi fulani
kukamatwa nyingine na kurejeshwa kwao.
“Nataka niwaondoe hofu wale wote wanaodhani polisi
haiwezi kumkamata mtu akikimbia nchini, tuna mkono mrefu sana, na hatufanyi
kazi kinyume na taratibu zetu,” alisema.
Kamanda Wambura pia alikiri polisi kufungua jalada la
Kapuya, huku akiweka wazi kuwa kinachofanyika hivi sasa ni uchunguzi wa tuhuma
zake.
Alisema miongoni mwa maeneo wanayoyafanyia uchunguzi
ni kubaini kama ujumbe ulio katika simu ya binti anayedai kubakwa na kutishiwa
maisha unatoka katika simu ya mbunge huyo.
“Tumefungua jalada, lipo kwa ajili ya uchunguzi na
tukibaini kuwa ni nani anahusika na tuhuma hizo tutamsaka na kumkamata popote
alipo,” alisema Wambura.
Gazeti hili limekuwa likiandika namba ya simu ya Prof.
Kapuya ambayo huwa anaitumia kutuma ujumbe wa vitisho kwa binti huyo, ingawa
kuna vyombo vingine vya habari viliamua kuandika kwa mtazamo tofauti na
kumtuhumu dada wa binti aliyebakwa kuwa ni mtu mzima na kuwa ana uhusiano na
Kapuya, na wana watoto.
Simu hiyo namba 0784993930 inayodaiwa kumilikiwa na
Profesa Kapuya, mbali ya kutuma ujumbe mfupi wa maneno ya kutishia kuua, pia
ndiyo inayodaiwa kutumika kutuma pesa kwa njia ya mtandao kwenda kwa binti
huyo.
Tangu gazeti hili lianze kuandika tuhuma hizi nzito,
kumekuwapo na kusuasua kwa mtuhumiwa huyo kutiwa hatiani na Jeshi la Polisi.
Harakati za kufungua jalada dhidi ya Kapuya zilizoanza
wiki iliyopita ziliendelea hadi juzi ambapo polisi walitumia zaidi ya saa 12
kumhoji binti huyo anayedaiwa kubakwa ili kupata ukweli wa sakata hilo.
Akiwa polisi, binti huyo alikutana na Mkuu wa Polisi
Wilaya ya Kipolisi ya Oysterbay (OCD) na OC-CID wake na kutoa maelezo ya awali
kabla ya viongozi hao kumruhusu ayaweke malalamiko yake katika maandishi kwa
ajili ya kufunguliwa mashitaka.
No comments:
Post a Comment