Nacheka
kwa uchungu
Tanzania
na uongozi wa damu
Na Charles Misango
NIMELAZIMIKA kuyakumbuka maneno mazito aliyotoa
Spika wa Bunge la Tanzania Anne Makinda wakati wa msiba wa Waziri wa Fedha na
Uchumi, Dk William Mgimwa aliyefariki mwanzoni mwa mwezi huu nchini Afrika
Kusini.
Mbele ya umati wa waombolezaji, Makinda alisema
ingekuwa ni amri yake angekufa mtu (kwa namna nyingine waziri) mwingine lakini
sio Mgimwa!
Sitaki kurejea namna alivyoshambuliwa kwa maneno,
na mijadala ilivyotamalaki katika vyombo vya habari kuhusiana na kauli hiyo.
Kilichonisukuma kukmumbuka maneno ya mama Makinda
ni kile kinachoendelea katika wilaya ya Bunda mkoani Mara.
Juzi nililazimika kushuka katika mji huo mdogo
nikitoka Musoma kikazi ili niwe kama Yule Thomaso tunayemsoma katika Biblia
ambaye alipoambiwa Yesu Kristo amefufuka alikataa hadi amwone kwa macho yake na
kugusa makovu ya misumari aliyoshindiliwa msalabani.
Mji mzima wa Bunda unatikisika kwa sasa kutokana
na kampeni za uchaguzi mdogo wa diwani wa kata ya
Nyasura, baada ya kiti hicho kubaki wazi kufuatia kifo cha aliyekuwa diwani
wake Zamberi Ngobayi (Chadema).
Katika kampeni hizi ambazo vyama viwili, Chama cha
Mapinduzi (CCM) ambacho ni dhahiri kitamsimamisha Alex Mwikwabe ambaye inadaiwa
alipatikana baada ya wagombea wawili wa awali kujitoa na Chama cha Demokrasia
na Maendeleo (Chadema) kilichomsimamisha Magambo Webiro zinaendeshwa katika
hali inayodhihirisha ubabe, vitisho, hila na ubabaishaji wa hali ya juu.
Nimeshuhudia kampeni za kuchafuana majina, hadhi
na heshima ya wagombea zikifanywa na watu wazima kabisa, tena viongozi
waliostahili kuionesha jamii kuwa wanawathamini watanzania na wanaheshima
matakwa ya watu ya nani awe kiongozi wao.
Nimeshituka zaidi hata baada ya kuona upande mmoja
ukijaribu kuwadanganya wapiga kura kwa hoja za kipuuzi za kwamba mgombea wa
Chadema ni mganga wa kienyeji na hivyo hafai kuchaguliwa. Tena wanaosema hivyo
ni viongozi wengine wa CCM ngazi ya wilaya. Ni hoja ya ajabu kwa sababu hakuna
popote katika katiba ambapo mtu anayetibu watu kwa kutumia dawa za kienyeji
haruhusiwi kuchaguliwa na kuwa kiongozi. Na kwa kutambua hilo, hao hao
wanaosema hivyo, wanasahau kuwa mmoja wa wabunge wake wa bunge la Muungano ni
mganga wa kienyeji ambaye katika uchaguzi uliopita alimbwaga daktari mwenye PhD!
Je viongozi wa CCM wa wilaya ya Bunda kwa hoja
hiyo ya uganga iliyokanushwa na mhusika mwenyewe, wanataka kusema kuwa wapiga
kura Korogwe vijijini walifanya kosa kumchagua mganga wa kienyeji pia Prof Maji
Marefu (CCM)kuwa Mbunge wao?
Na katika namna ya kushangaza, baadhi ya viongozi
wa CCM sasa wanadaiwa kumwandaa mwana mama mmoja atakayetembea kata nzima
kueleza namna mgombea wa Chadema alivyotapeli kwa kutumia uganga wake. Mama
huyo anadaiwa kuwa atatangaza jinsi mgombea wa Chadema alivyomtapeli mamilioni
ya fedha ili amtibu!
Fikiri tu kwamba suala la uganga limechukua nafasi
kubwa katika kampeni huku upande wa pili yaani Chadema, badala ya kupuuza
propaganda hizo, nao wamejikita kujibu hoja na kusahau kutangaza sera.
Mbali na hoja ya uganga, wapinzani wa mgombea huyu
wameingiza ubaguzi wa kikabila na kimaeneo. Wanajaribu kuwaaminisha wapiga kura
kuwa ni hatari kumchagua mgombea huyo kwa sababu sio mzawa wa Nyasura bali
mhamiaji aliyefukuzwa kutoka Kata nyingine ya Kunzugu katika kitongoji cha Bokole.
Kana kwamba hoja hizo kwa viongozi wa chama tawala
hazina madhala kwa taifa, sasa wanatuhumiwa kuibua jambo baya zaidi ambalo
limeanza kuwatisha na kuwapa kiwewe baadhi ya wananchi sio wa Kata ya Nyasura
tu bali wilaya nzima ya Bunda.
Hili ni kuwepo kwa tuhuma kwamba zipo njama za
kutaka kumkamata mgombea wa upinzani na kumbambika kashfa ya kuiba nyaraka sa
siri za serikali.
Inadaiwa kuwa hizo zinazoitwa nyaraka za siri za
serikali, zile zinazohusiana na sakata la ardhi katika wilaya ya Bunda.
Kwamba mgombea huyo anatembea na nyaraka za
mikataba feki iliyotumika kutaifisha ardhi ya mlima Balili inayosemekana ni
mali halali ya shule ya msingi Balili na pia ya Kanisa la Wasabatho.
Inasemekana tuhuma hizo zinawagusa baadhi ya
watendaji wa wilaya na mkoa, akiwemo mkuu wa mkoa mmoja hapa nchini.
Nyaraka hizo zinazoitwa za siri, pia zinadaiwa
kuwa ni zile zinazofichua kile kinachoitwa tuhuma za waziri mmoja mwandamizi wa
serikali ya CCM anayedaiwa kuchukua kwa mabavu sehemu ya ardhi ya shule moja ya
sekondari.
Kampeni hizo za uchaguzi wa udiwani kata ya
nyasura na zigine 28 nchini
utakaofanyika Februari 9,2014, zinaashiria jambo moja tu. Umwagaji wa damu!
Hali sio shwari, viongozi na wanachama wa vyama
vya upinzani wameungana na lugha inayotamba sasa ni kwamba..’heri kufa kuliko
kuonewa, kuliko kudhulumiwa’
Wapenzi na wanachama wa CCM, nao wanatamba na
kauli,….’kwa gharama yoyote lazima tukomboe kata yetu”.
Kauli hizi sio njema hata kidogo hasa
zinapopaliliwa kwa nguvu na wanasiasa wakomavu ambao chama chao kinaongoza
nchi. Ni kauli ambazo zinaonesha kuwa uwezekano wa kupata viongozi wazuri,
wakweli, waadilifu na wachapakazi kama alivyokuwa waziri Mgimwa ambaye Spika
Makinda hakutaka afe ni ndoto.
Inatia uchungu zaidi ikiwa leo watanzania wanazidi
kushuhudia haki na demokrasia ikikandamizwa kwa gharama za walipa kodi, ili tu
watu wanaowataka wachaguliwe kuwa viongozi wa watu hata kama hawana sifa na
hawapendwi.
Spika Makinda hata kama kauli yake, haikuwa njema
masikioni mwa watu, ajue kuwa chama chake kitasaidia kupatikana kwa viongozi
kama marehemu Mgimwa kikiacha mizengwe, hila, ujanja wa kishamba kuendesha
kampeni zisizo na mashiko.
Spika Makinda ajue kuwa ni jukumu la CCM kushika
na kusimama kama ‘baba wa demokrasia’ na hivyo, kuacha ghiriba za aina yoyote
ile katika chaguzi ziwe ndogo ama kubwa.
Kampeni za kudhalilisha, kukomesha na kutesa
wasiokuwa wapenzi na wanachama wa CCM na kulazimisha kumweka mtu wa ovyo
madarakani kamwe haziwezi kuleta watendaji bora wa serikali. Haziwezi kulipatia
taifa madiwani, wabunge na mawaziri bora.
Kampeni zinazosukumwa na ubabe, uonevu, wizi wa
kura na hata kumwaga damu za wananchi, haziwezi kamwe kuleta manufaa katika
nchi zaidi ya machafuko na umwagaji damu. Kauli ya wana wa Bunda kwamba liwalo
na liwe ni ishara ya kwamba watu wamechoka kunyanyaswa. Ni kauli za waliokosa
matumaini dhidi ya serikali yao, na hawaitaki.
Spika Makinda atatamani wafe mawaziri wengi ikiwa
leo hii katika kampeni za uchaguzi wa marudio ya udiwani, polisi wanatumika
kupiga na kufungulia watu kesi za kubambika ili tu CCM ishinde.
Makinda ajue kuwa kama kweli ana uchungu na taifa
hili, basi awaambie viongozi wenzake kuwa wanalo jukumu la kuheshimu matakwa ya
watu. Wanalo jukumu la kujua na kutekeleza kile watanzania wanachokitaka na sio
kuwalazimisha kwa mbinu chafu hata za kumwaga damu.
Bado watanzania wanakumbuka jinsi viongozi wa
upinzani walivyofunguliwa mashitaka ya ovyo, kupigwa, kudhalilishwa na kuteswa
kisa tu walisimama kuwania uongozi katika chaguzi mbalimbali. Ni viongozi hao
hao wa CCM ambao Spika Makinda ni mmojawao, ambao wametumia nguvu na maarifa
mengi kuwaaminisha watanzania kuwa wapinzani ni watu wa ovyo, hatari na
wanaotakiwa kuogopwa kama ukoma.
Kibaya zaidi, Spika Makinda mwwenyewe mara nyingi
tu ameruhusu na kushiriki kukandamiza haki za wapinzani hata katika masuala ya
msingi ya nchi. Kiti chake kimeshiriki mara nyingi kunyamazisha sauti za
watanzania kupitia wabunge wao.
Wabunge wangapi wa upinzani wamekandamizwa
walipokuja na hoja zenye maslahi ya nchi? Wabunge wangapi wa upinzani wameitwa
wazushi na waongo walipoibua tuhuma dhidi ya mawaziri? Kama Kiti cha Spika
kingeruhusu hoja kujadiliwa na hatua madhubuti kuchukuliwa, leo hii uovu na
uvundo katika sekta ya elimu ingefikia hatua hii?
Ni mawaziri wangapi walilindwa na kiti cha Spika
pale walipotoa majibu ya uongo, ubabaishaji na yenye hasara kwa taifa? Kwa nini
kiti cha spika kiliwakingia kifua alafu leo kiti hicho hicho kinalia? Dhihaka?
Inatia uchungu basi tunaposikiaNi ajabu kwamba leo
eti analiachuklia wapinzani na kuwanachama makini na anayeheshimu demokrasia
hawezi kufurahia ushindi uliopatikana kwa kukandamiza na kuonea watu.
KUMBUKUMBU YA NYERERE (1999 - 2013)
Usomi, Uhuru na Ukweli
Mwalimu Julius
Kambarage Nyerere (1922 – 1999) anakumbukwa kwenye historia ya Tanzania kwa
kuwa msomi wa kwanza kupata shahada ya uzamili kwenye taaluma ya ualimu wa
historia ya uchumi. Kwa jinsi ya pekee, Mwalimu Nyerere alionesha matumizi
mazuri ya akili ya usomi tangu alipokuwa akisoma chuo kikuu cha Afrika ya
Mashariki (Makerere) na baadaye Edinburg. Kwa jinsi hiyo, Mwalimu Nyerere
anaweza kuingia kwenye historia ya wasomi waliyesoma katika Tanganyika ya
wakati wake na baadaye Tanzania chini ya muungano!
Hatuwezi
kumkumbuka Mwalimu Nyerere kama wafanyavyo kasuku kwa kurudia yaleyale kila siku
kwenye kipindi cha ‘Wosia wa Baba.” Na hatuwezi kujiweka kwenye mizani ya
usomi, kama ni wasomi kweli kwenye vyuo vikuu na kada zote za shahada za
uzamivu, uzamili na shahada za taaluma kama hatutasimama kwenye uhuru (wa kutoa
maoni) na kusimamia ukweli ambao ndio chimbuko la uhuru!
Zamani
nilipokuwa mtoto wa miaka mitano hadi naanza darasa la kwanza (mwaka 1978)
nilikuwa na fikra kwamba, usomi ni kujua kwamba ukweli ni kweli na lazima
usimamiwe! Kadri siku zilivyokuwa zikinitupa mkono, hadi nilipoingia chuo kikuu
kama mwanafunzi nilitamani nisome ili niwe ‘mkweli’ na msadikishaji wa ukweli.
Baada ya kusoma na kuanza kazi kwenye kada ya taaluma, nilikuwa na tamaa kubwa
ya kumsoma Mwalimu Nyerere na wanafalsafa wengine wa dunia wenye mitazamo
tofauti na wanaosimama kwenye uhuru na ukweli. Na kwa kuanzia nilianza na
walimu waliyenifundisha na kwa sasa sehemu yao ndio ninaofanya nao kazi ya
kusoma ukweli kwa njia ya utafiti, hoja za kisayansi na mantiki.
Mwalimu
Nyerere alitaka wasomi wawe huru; hata hivyo, sehemu kubwa ya wasomi wa siku
hizi kwenye vyuo vingi ni watumwa wa akili (mental slaves). Kama alivyowahi
kuimba mwanamuziki nguli wa reggae duniani, Robert Nester Marley (Bob Marley);
sijui ni lini wasomi hawa uchwara watajikomboa kutoka kwenye utumwa wa akili?
Sijui! Uhuru wa wasomi, si kukariri maandiko kama wendawazimu, bali wanatakiwa
wawe wakweli kwa maandiko yao kwa kuzingatia utafiti na hoja za kisayansi zenye
mantiki iliyo kuu na inayozingatia mizani ya haki, uhuru, usawa na insafu ya
hoja kwa mujibu wa ukweli unaopatikana kwa misingi ya kutafuta ukweli
uliyofichwa na au kujificha (hidden truth).
Katika
kusimama kwenye nukta hii; Mwalimu Nyerere aliwahi kutumia fursa ya kuhutubia
kwenye Chuo Kikuu cha Liberia mwaka 1968 kwa kuzungumzia: jinsi usomi
unavyotakiwa kuwatumikia wananchi; jinsi vyuo vikuu vinavyotakiwa kufanyakazi;
jinsi wanafunzi wanavyotakiwa kujifunza ukweli; na jinsi walimu wanavyotakiwa
kusimama kwenye ukweli. Nukta hizi zilitolewa na Mwalimu Nyerere (1968)
aliposisitiza juu yake na kuonesha kwa jinsi gani usomi unavyoweza kutumika
katika kupambana na ufisadi.
Mwalimu
Nyerere alianza kwa kusema, ‘Nimekuwa nikitoa maombi kwenye vyuo vikuu vya
Afrika, na kwa wanafunzi waliomo katika vyuo vikuu vya Afrika, pamoja na wale
wengine wote wanaopata elimu ya juu, wawe wazalendo wenye kujitoa kwa nchi zao,
na kufanya kazi zao zote ziwe na shabaha ya kuhudumia nchi zao.’ Leo
tunashuhudia sehemu kubwa ya wanafunzi wa vyuo vikuu wakikosa uzalendo na wengi
wao wakijielimisha kwa utashi wa kibinafsi na si kwa maendeleo ya watu. Huu ni
uzezeta wa usomi mamboleo uliyowashika wanafunzi wengi na baadhi ya walimu wa
vyuo vikuu wanaoyeogopa kusimama kwenye uhuru na ukweli!
Mwalimu Nyerere alisisitiza kwenye hotuba
hiyo kwamba, ‘Kazi ya vyuo vikuu ni kuchimba na kutafuta ukweli.’ Bahati mbaya
sana, siku hizi wasomi wengi wa vyuo vikuu wameacha kuchimba na kutafuta ukweli
badala yake wanafanyakazi kwa kutumia ‘majungu’ na taarifa za kupikwa zisizo na
ushahidi wa kisayansi na mantiki. Kibaya zaidi kwa baadhi ya wasomi waliyepewa
dhamana ya kuatamiza fikra za usomi kwa kizazi kipya wamekuwa waoga wa
kukosolewa na wanapokosolewa hujificha nyuma ya matumizi ya sheria na kanuni
kandamizi katika kuficha akili zao tepetepe zilizoshikwa na ufisadi wa kimfumo
huku wakitumia nafasi zao kuminya uhuru na kuzuia ukweli usijulikane.
Mwalimu
Nyerere aliamini kwamba, ‘Nchi huhudumiwa na ukweli;’ na kwa msisitizo alisema,
‘Naamini kwamba nchi inataka vyuo vikuu, na wanafunzi na walimu wake, wasimame
katika kweli kama wanavyoiona, bila kujali yale yatakayowatokea wao binafsi.’
Hapa Mwalimu Nyerere alikuwa anasisitiza juu ya dhima ya vyuo vikuu katika
kusimamia ukweli; wanafunzi na walimu kusimama ngangari katika kutafuta ukweli
wanaouona kwa jicho la uchunguzi na mantiki ya hoja bila ya kuogopa! Kwa kuwa
marazote mtu anaposimamia ukweli anaodhani ni kweli kuna kila sababu ya kufikwa
na madhara kwa wale wasiyetaka ukweli ujulikane!
Kwa
kutaka vyuo vikuu viwe vitivo vya kukosoa utendaji wa viongozi wa wananchi,
Mwalimu Nyerere alisema, ‘Hakuna binadamu asiyekosa, viongozi na wananchi
wanaoongozwa pia; inawezekana kwamba sisi tumekosea ama kwa sababu ya kutokujua
ama kwa sababu ya inda ya watu. Ni sehemu ya kazi ya wale wasiobeba wajibu wa
kuendesha mambo siku hata siku kutusaidia na kuwasaidia wananchi kwa ukomo wa
uwezo wao. Na kufanya hivyo, wakati mwingine hulazimu kusema maneno
yasiyowapendeza watu, mradi mnayaamini kuwa ni kweli.’ Sehemu ya hotuba hii
inapatikana kwenye kitabu cha Uhuru na Maendeleo (Nyerere, 1973 ukurasa wa 14
hadi wa 15).
Kwa
wale wote, pamoja na vyuo vikuu vinavyojinasibisha na kumuenzi Mwalimu Nyerere
kwa kutenga siku maalumu na au kuanzisha vigoda na hata kuweka wiki ya
kumbukumbu; ni wajibu kujifunza mambo makubwa matatu kwenye hotuba hii. Mosi,
umuhimu wa kuchimba na kutafuta ukweli kuhusu mazingira yanayotuzunguka na
hususan kuangalia utendaji wa viongozi waliyepewa dhamana ya kuongoza umma.
Pili, wasomi wanatakiwa kuwa na ujasiri wa kuwakemea viongozi wanaokwenda
kinyume na maslahi ya umma ili kuwaelimisha juu ya wajibu wa kuwatumikia
wananchi kwa haki, uhuru na usawa. Tatu na mwisho, kujitoa mhanga (kama
ikibidi) ili kutetea haki za wananchi na kufanya hivyo kwa uhuru, haki, ukweli
na uwazi katika kufikia malengo ya ‘elimu lazima itumike kwa manufaa ya wote’
au ‘tujifunze kwa maendeleo ya watu.’
Nukta
zilizoainishwa hapa zinaafikiana sawasawa kama alivyoandika aliyewahi kuwa Mkuu
wa Chuo Kikuu Mzumbe, Ibrahim Mohamed Kaduma kwenye kitabu chake cha ‘Maadili
ya Taifa na Hatma ya Tanzania: Enzi kwa Mwalimu Nyerere.’ Kaduma (2004)
ameandika, ‘Mawazo haya (ya Mwalimu Nyerere) ni muhimu sana kwa Watanzania hasa
katika kipindi hiki cha mmomonyoko mkubwa wa Maadili ya Taifa letu.’ Kaduma
(2004, ukurasa wa 66) amesisitiza, ‘Inafaa wasomi wetu wamtafakari Mwalimu Nyerere
kwa makini zaidi ili kuyaendea mausia (wosia) yake mema kwa ajili ya vizazi
vijavyo.’
Siku
hizi wasomi wetu wengi wanamtumia Mwalimu Nyerere kwa mtindo wa kutafuta sifa
za kijinga na maslahi ya kujipendekeza kwa kulitaja jina la kiongozi huyu huku
matendo yao yamejaa ufisadi, wizi na ubadhilifu wa mali ya umma! Wengi wamekuwa
mstari wa mbele katika kutumia mali ya umma kwa matumizi binafsi kuliko
kuwatumikia wananchi. Kwa mfano, baadhi ya viongozi wa vyuo vyetu vya umma
badala ya kutafuta ukweli na kusimama kwenye uhuru na ukweli wanajipendekeza
kwa viongozi wa siasa mafisadi ili wanufaike na ushirikiano kwa ahadi za kupata
nafasi za kiutendaji serikalini ambazo ndizo zinazotumika kuendeleza ufisadi wa
kimfumo na wa ndani ya mfumo.
Mwalimu
Nyerere (1962 na 1968) alifundisha kwamba, ‘Kujielimisha siyo maana yake kwenda
shule; isipokuwa, kujielimisha ni kutafuta ukweli na kutumia ukweli kwa ajili
ya maendeleo ya watu wote. Hata hivyo, vyuo vyetu vikuu siku hizi vina baadhi
ya wasomi hususan waliyepewa madaraka ya kuongoza vyuo hivyo wenye ugonjwa wa
upumbavu. Mpumbavu ni yule anayeyapa mambo sababu zisizo za kweli na anashauri
dawa isiyo ya kweli (Nyerere, 1962: 8). Inasikitisha kuona baadhi ya wasomi na
walimu wa vyuo vikuu wanayedhaniwa wamesoma na kuelimika wakishindwa kuyapatia
matatizo ya wananchi majibu. Baadhi ya vyuo vikuu, wanafunzi wengi wa vyuo
vikuu na baadhi ya walimu wa vyuo vikuu vya Tanzania wamekuwa sehemu ya mfumo
wa ufisadi, kama alivyowahi kusema Mwalimu Nyerere, ‘nchi inanuka rushwa.’
Natambua
kwamba, wengi hawapendi kuambiwa ukweli; na au wanapofanya mambo yao ya
kibaradhuli, kifedhuli na au kifisadi! Wasomi wa sampuli ya wale wanaoogopa
ukweli ni sawasawa na nyani anayechutama kuficha ngoko yake huku hatoweza
kutembea hadi ngoko itakapoonekana! Usomi ni ukweli na ukweli ni uhuru; msomi
wa kweli haogopi kukosolewa. Tujisahihishe, tuache upumbavu!
Mwandishi wa makala
ni:
Bakari M Mohamed
Simu ya kiganjani:
+255 713 593347
Barua pepe: maligwa1968@yahoo.com
RAIS WANGU KIKWETE UONGOZI WETU KAMA KISHADA TUTOKAKO TUENDAKO HAKUJULIKANI!
Rais
wangu moja kati ya sifa nyingi za mtu dhaifu ni uoga. Anaogopa hata kivuli
chake. Serikali ya Awamu ya nne ikisikia kuna mgomo au hasa maandamano, inatetemeeeka,
utadhani ni utete dhaifu unaosukumwa na mkondo mkali wa maji ya mto yaendayo
kasi! Yohani, ‘John Pombe Magufuli’ ni uzao halisi wa udongo wa nchi hii.
Amefukua vya kufukua!
Katumbua
jibu na sasa usaha unamwagika. Mwenye jipu yaani serikali, inanuka usaha mwili
mzima! Kwakuwa Wahenga wenye busara walisema dawa ya jipu ni kulitumbua na
kwakuwa Waziri wetu wa Ujenzi amelitumbua, basi wote wenye mapenzi mema
wanapaswa kumpongeza kwa kazi njema aliyoifanya.
Rais
wangu palipo na ukweli tutasema. Lazima tuusimamie ukweli hata kama kwa kuusema
ukweli huo mjinga atasema tunamchukia mtu na mpumbavu atasema tumenunuliwa na
mtu! Kuacha kusema ukweli kwa kuogopa kuonekana unamchukia mtu au kuogopa
kusemwa umenunuliwa ni upungufu alionao mwanadamu dhaifu. Jasiri hatikiswi na
hilo!
Magufuli
sifahamiani naye, lakini ni mtu mwema gani asiyeujua utendaji kazi wake ulivyo
mahiri? Tangu waende akina Sokoine na Mrema nani mwingine wakutolea mfano?
Huyu
siyo malaika. Aliposhirikiana na genge la walanguzi tukulangua nyumba zetu,
wenyewe wakiziita za serikali tulimlaani wote! Na kwa hilo hajasamehewa! Na
hatasamehewa mpaka pale atakapowarudishia wananchi nyumba zao! Lakini kwakuwa
hatuko hapa kuangalia sura za watu, tuko hapa kujadili utendaji kazi mahiri kwa
maslahi ya nchi yetu na wananchi wake, anayefanya jambo jema kama alilolifanya
Magufuli, kusimamia sheria za nchi, hatuna budi tumpongeze wote.
Kiongozi
wa haki mwenye ufahamu timamu akiambiwa ukweli hata kama utamuumiza,
atamheshimu aliyemwambia huo ukweli, akijua kuwa huyo ndiye aliye na mapenzi ya
kweli naye. Na ikimpendeza atamtumia!
Rais
wangu wapinzani wanapokwambia waondoe mawaziri wanaokupotosha hawamchukii mtu
wala hawawachukii hao mawaziri! Wanakutakia mema Rais wangu! Hawataki uonekane
wa ajabu mbele ya watu wako! Tunaoishi na wananchi huku mitaani, vijijini na
mashambani tunaambiwa mengi. Ningekuwa na faragha na wewe mengine ningekuwa
nakunong’oneza, ili ukinieleza niwaeleze wapate kukuelewa kwa maana wako
wanaokupenda! Kwa kuwa sina faragha na wewe nakuwekea maneno ya wananchi wako
hapa ili ukiyasoma ujue ni picha gani wanaokuzunguka wanakutengenezea mbele ya
wananchi!
Mwanamwema
kutoka Iringa aliniandikia ujumbe ambao na mimi nauweka hapa vilevile
alivyoandika! Aliandika, “Mwalimu nimesikitishwa sana na hotuba ya rais
iliyoangaliwa hata na watoto wadogo. Hivi kwa nini anamshambulia mwananchi wake
kwa maneno makali kama yale? Halafu kwa nini kila kitu anasema ‘nimeambiwa’?
Falsafa yake ya mbayuwayu imemshinda? Sasa tena tunaambiwa kumbe hata mswada
wenyewe hajausoma. Kazi tunayo. Nchi za kiafrika haziendelei na moja ya sababu
ni kuongozwa na watu wenye kuambiwa.”
Rais
wangu usipokuwa na pupa utaona kuwa watu wako wanakujali lakini unawakatisha
tamaa! Dunia na Ulimwengu vinatambua hivyo! World Happiness Report 2013
iliyoandaliwa na kundi la wataalamu kutoka Umoja wa Mataifa imedai kuwa
Watanzania ni miongoni mwa watu wasio na furaha na waliokata tamaa hapa
Duniani!
Ndugu
Rais yaliyojiri katika sakata la wenye malori na serikali limezidi kuwakatisha
tamaa Watanzania. Iliandikwa, ‘Pinda amuonya Magufuli’, wengine wakaandika,
‘Serikali yamzima Magufuli’. Wananchi wakabaki kuulizana, hivi Pinda na
Magufuli wako serikali mbili tofauti? Ni serikali gani hii yenye viongozi wenye
kauli tofautitofauti? Hawakutani kwenye Baraza la mawaziri kuweka msimamo wa
serikali?
Waliosema
serikali inapasuka mwanzoni sikuwaelewa. Utoto siyo uchache wa miaka ya
kuzaliwa peke yake! Wala kufanya upuuzi siyo lazima umtukane mtu. Kwakuwa hawa
ni waheshimiwa huwezi kuweka neno watoto au wapuuzi. Isipokuwa viongozi wa
serikali moja kuonekana mbele ya wananchi kama wanatunishiana misuli, ni vyote
viwili, utoto na upuuzi!
Rais
wangu Magufuli anasema anazilinda barabara zetu zisife haraka! Mpaka hapa kuna
ubaya gani? Je, mamlaka hayo anayo? Kaonyesha sheria iliyotungwa na Bunge
kihalali kabisa! Kumbe mamlaka anayo kufuatana na sheria! Sasa ndugu Rais huyu
anayemzima Magufuli au kumuonya yeye alisomea wapi?
Kwa
mdomo wake Waziri Mkuu wetu anasema, “Hatua zilizochukuliwa na Dk Magufuli
kufuta vifungu vilivyokuwa vikiruhusu asilimia tano zilifuata sheria. Tatizo
lililojitokeza ni kutoshirikisha pande zinazohusika ili kushauriana na kupata
uamzi wa pamoja”. Jamani sheria ikishatungwa mnashauriana nini tena?
Akaongeza,
“Sasa suala la asilimia tano, lilitokana na ombi la wadau wa usafirishaji kwa
aliyekuwa waziri wa Ujenzi miaka ya nyuma na haikuwa sheria kamili.
Limeondolewa baada ya kuonekana linatumiwa vibaya.” Kudai kwa nguvu wakati huna
sheria nikufanya fujo!
Bado
anakiri kuwa limeondolewa baada ya kuonekana linatumiwa vibaya! Yaani wenye
malori walitumia vibaya ombi lao. Magufuli kuona hivyo amelifuta. Kwa maelezo
haya ya Waziri mkuu Magufuli amekosea wapi? Kama ombi hilo ovu liliridhiwa na
Waziri wa Ujenzi wa miaka ya nyuma kwa maslahi ya nchi au kwa maslahi ya wenye
malori na waziri mwenyewe haijulikani. Kinachojulikana ni kwamba waziri huyo
hivi sasa serikali imemfikisha mahakamani kwa tuhuma za matumizi mabaya ya
madaraka alipokuwa ofisini siku hizohizo za nyuma.
Waziri
mkuu anasema kosa la Magufuli ni kuilinda hiyo sheria bila kuwashirikisha
wanaoivunja. Jamani, unapomkamata mwizi unamshirikishaje? Unashauriana naye
nini ili mpate uamuzi wa pamoja kama siyo kutaka kumwomba rushwa?
Mzee
Peter Kisumo anasema, “Chama kimebaki cha walalamikaji, kila mtu amekuwa
mlalamikaji. Hata Waziri mkuu amegeuka mlalamikaji. Sijaona watu
wanaowajibishwa kwa ufisadi!”
Rais
wangu bado Waziri mkuu bila sababu ya msingi anaunda tume sijui kamati ambayo
hata hivyo haina uwezo wa kuifuta wala kuirekebisha sheria hiyo! Huku ni kufuja
kodi ya wananchi? Ndugu Rais ni hivi majuzi tu wananchi kwa huzuni kubwa
wameshuhudia mwandishi wa habari Ufoo Saro, baada ya kujeruhiwa vibaya kwa
risasi kadhaa wanawema walimkimbiza hadi Hospitali ya Serikali ya Tumbi lakini
akakosa huduma ya matibabu kwasababu Hospitali hiyo haikuwa na mashine ya Xray.
Kwanini fedha zitakazotumika na tume hii na tume nyingine za aina hii
zisingetumika kununulia mashine ya Xray kwa Hospitali hii? Umuhimu wa Hospitali
ya tumbi uko wazi. Inapokea majeruhi kila siku watokanao na ajali za mara kwa
mara zitokeazo katika barabara hii katili ya Morogoro! Mungu huyu! Maisha ya
wananchi hayana maana mbele ya wenye malori!
Serikali
inayojiendesha bila kutegemea ufadhili wa wafanyabiashara hasa wakati wa
kampeni, wenye malori wangepata wapi kiburi cha kugoma? Sheria kama haifai
hurudishwa Bungeni ikafutwe au ikarekebishwe huku kazi zikiendelea! Wakati wa
Uwaziri mkuu wa Sokoine au wakati wa Mrema, mwenye lori gani angethubutu kuinua
pua yake juu? Serikali kuruhusu kikundi fulani cha watu, wawe wenye malori au
wenye asili fulani, waendelee kuvunja sheria halali huku wananchi wengine
wakiona ni mfano halisi wa uongozi mbovu! Bila kufahamu serikali inawasukuma na
wengine wavunje sheria zinazowakera. Chanzo cha maandamano na migomo
isiyokwisha ni uongozi mbovu!
Ndugu
wananchi kitabu cha mwalimu mkuu wa watu kinaelekeza wazi kuwa jiandaeni
kupokea fedha zitakazochangwa na hawa jamaa. Mkiletewa wakati wa kampeni
zichueni, lakini kura msiwape! Kuita wenye malori ili muafikiane wakati sheria
iko wazi ni kielelezo cha uongozi ulioshindwa kuongoza! Yanini Kuwa na kiongozi
wa namna hiyo? Tumeliona hili kwenye tozo ya simu. Baada ya kusikia kelele za
wananchi ikaamriwa mawaziri na wamiliki wa kampuni za simu au wadau wakae pamoja
wafikie muafaka. Kiko wapi! Uongozi ulioshindwa!
Rais
wangu uongozi wa nchi unapokuwa laini kiasi hiki, wananchi wanapoletewa habari
za kutisha kuwa magaidi wameshamiri nchini mwetu matumaini yao wayaelekeze
wapi? Jeshi la Polisi mkoani Mtwara, linawashikilia vijana 11 kwa tuhuma za
kukutwa mafichoni katika msitu wa mlima Makolionga wilayani Nanyumbu wakifanya
mazoezi ya kijeshi. CD walizokutwa nazo ni za kundi la kigaidi la Al Shabaab.
Zinaonyesha watu wakichinjwa, mauaji ya kiongozi wa Al Qaeda Osama Bin Laden,
Zindukeni Zanzibar, kuaandaa majeshi, mauaji ya Idd Amin na Mogadishu Sniper.
Kamanda
wa Polisi wa Mkoa wa Mtwara Zellote Stephen anasema watuhumiwa walikamatwa,
baada ya polisi kupata taarifa kutoka kwa wasamaria wema. Wananchi wanauliza
bila wasamaria wema magaidi hao si wangemaliza mafunzo yao halafu wakaenda
kwenye utekelezaji bila polisi kuwa na habari? Polisi na vyombo vingine vya
ulinzi na usalama vilikuwa wapi?
Katikati
ya habari hizo zinakuja habari nyingine zinazoarifu kuwa, Ramadhani Twaha mkazi
wa mtaa wa Kirumba jijini Mwanza amefikishwa katika mahakama ya Mkoa wa Mara.
Anatuhumiwa kukutwa akisambaza CD zenye machapisho ya kigaidi katika msikiti wa
Ibadhi ulioko mjini Bunda ambazo zina mafunzo ya kijeshi na zinazochochea
vurugu. Matukio haya mawili yanaashiria jinsi mtandao wa kigaidi ulivyosambaa
nchini. Zinaingizwa vipi na kusambazwa vipi nchini? Nani wanaingiza CD hizi?
Usalama wetu ni wa mashaka matupu!
Mafunzo
katika msitu wa Makalionga yalifanywa kwa muda gani? Je, kundi hilo la watu
11 lilikuwa ni kundi la ngapi? Ni katika msitu wa Makalionga tu ndiyo mafunzo
hayo yanakofanyika? Je, waliyokuwa wanapewa mafunzo waliambiwa malengo ya
mafunzo hayo? Walimu wao wako wangapi na wako wapi? Wanafadhiliwa na nani? Je,
huu siyo mwanzo wa vita vya msituni?
Ndugu
Rais raia kutoa taarifa kama hiyo kwa jeshi la polisi ni muhimu na ni ishara ya
uzalendo kwa nchi yake, lakini huko kuwe ni kusaidia tu! Hilo ni jukumu la
polisi na vyombo vingine vya ulinzi na usalama kugundua vyenyewe hatari
zinazolinyemelea Taifa letu! Liwalo na liwe, wenye malori tu hivi! Magaidi
mtawaweza vipi?
Rais
wangu tunaacha ya kwetu tunadandia ya wengine. Viongozi wako kimbelembele
kusaka sifa za bei poa. Nchi yetu ilipopata nafasi adhimu ya kulihutubia Baraza
la Umoja wa Mataifa baadhi ya wananchi walisikika wakiusikitikia muda ambao kwa
maoni yao uliotumika vibaya kuisema ICC badala ya kuyapa nafasi matatizo lukuki
yanayoisibu nchi yetu! Nchi yetu ina ugomvi gani na ICC?
Rais
wangu ni uzalendo kwa bara la Afrika na Waafrika wenzetu ndiyo vinatusumbua?
Hapana! Ni mihemko ya moyo kwa kujihisi tuko kwenye foleni ya kwenda huko
kutokana na tunayoyatenda nchini mwetu? Hili linawezekana! Kwanza ziliisha
sikika habari kuwa kuna baadhi ya matukio ya kinyama yaliyotokea nchi mwetu ambayo
taarifa zake zinatumwa huko! Kujitoa ICC hakuwezi kuzuia tusihukumiwe na
mahakama nyingine. Kinachoweza kuzuia tusihukumiwe ni kutotenda unyama dhidi ya
raia wetu, kama tunaona tunatenda.
Katibu
Mkuu wa zamani wa Umoja wa Mataifa Bwana Koffie Annan amesema ‘itakuwa ni alama
ya aibu’ kwa bara la Afrika iwapo litajiondoa katika mkataba wa Roma uliounda
Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu, ICC. Amesema ikiwa viongozi wa Afrika
wataipinga na kuipiga vita ICC na kujiondoa, itakuwa ni fedheha kubwa kwa kila mmoja
wao na nchi zao. Tumwombee kwa Mungu Rais wangu asije akawa mmoja wao kati ya
marais wanaotaka kuziletea nchi zao fedheha hii kubwa! Mwenye fikra ya
kulipeleka wazo hili Bungeni huyo ni mufilisi, hafai kuwa kiongozi wetu! Tuna
akili gani kubwa ya kutaka kuunga mkono kujitoa ICC kuliko akili ya viongozi
waliotutangulia, waliosaini mkataba wa Roma wa kujiunga na ICC?
Bwana
Annan amewashutumu viongozi wa Afrika kwa kulinda maslahi yao binafsi na si kwa
Waafrika wote huku akisisitiza kuwa njama za nchi za Afrika kutaka kujiondoa
ICC ni ishara dhahiri kuwa kuna desturi ya kutoheshimu sheria.
Watuhumiwa
wanaokabiliwa na mashtaka katika mahakama hiyo wamefikishwa kama watu binafsi
na si kama Bara la Afrika, hivyo dhana kuwa ICC ina dhamira ya kuwaandama
viongozi wa Kiafrika siyo sahihi!
Mtu
mzima tena bila aibu anasema kati ya walioshitakiwa 30 waafrika ni 27. Hawa
ndiyo wale ambao akishtakiwa mhalifu, kama dini yao ni moja anasema wa dini
yetu tunaonewa! Kiongozi kuishiwa fikra ni hatari sana. Muhimu hapa ni kujua
je, walioshtakiwa ni wahalifu? Muhimu siyo rangi ya ngozi yao.
Mwanamwema
Jaji mpya wa Mahakama ya kimataifa ya Uhalifu (ICC) Dk Steven Bwana amesema
viongozi wa nchi za Afrika wanaotaka kujiondoa kwenye mahakama hiyo, wana lengo
la kuficha uovu uliopo katika nchi zao kwani baadhi yao wanajifanya miungu
watu!
Amesema,
“Afrika kuna viongozi wazuri, lakini tusifiche ukweli wapo waovu, wengine nusu
miungu wanaopenda kila kitu kiwe chao, hili halikubaliki. Nchi za kiafrika
kujitoa ni aibu, sababu zilizotufanya tujiunge zipo, tunataka kujiondoa
kwasababu tunadhani ICC inatufuatilia tunapofanya makosa, ICC inatimiza wajibu,
haiwadhalilishi viongozi wa Afrika, watafika kote.”
PASCHALLY
MAYEGA
TEL
0788 37 27 87
poleni sana wanatanzania
ReplyDelete