Nacheka
kwa uchungu: jan 8,2014
Taifa
likiongozwa kwa siasa chafu
SIKUTAKA kamwe kujadili kinachoendelea ndani ya
chama kikuu cha upinzani nchini, ali maarufu kama Chadema.
Sikutaka kwa sababu, taifa langu linayo mambo
mengi makubwa ya kujadili na kuyatendea kazi. Mambo ya msingi yanayoweza
kuwakomboa wanyonge na umasikini wao wa kukosa elimu bora, afya bora, maisha
bora na usalama wa uhakika!
Nimelazimika kuyajadili katika mada ya leo kwa
sababu yanayotokea ndani ya Chadema yanaelekea kwa kasi kubwa kuchukua sura ya
kitaifa. Sio siri kwamba sasa yanashabikiwa kwa waziwazi ama kwa kificho na
umma wa watanzania, baadhi yao wakiwa wanasiasa wakongwe, wakubwa kabisa na
wengine wakiwa watendaji waandamizi ndani ya serikali ya CCM.
Mtu waweza kucheka kwa uchungu unapofikiria siasa
za Tanzania zilivyo kwa sasa. Ni kama igizo la mwendawazimu! Linaloumiza zaidi,
ni kwamba ‘upuuzi’ huu wa siasa ninazothubutu kuziita za kishamba zinaligharimu
taifa na kuleta hasara kubwa ambayo kwa bahati mbaya, hakuna anayeiona.
Zinagharimu muda wa watu kufanya kazi za kuzalisha
mali. Zinagharimu fedha halisi za watanzania kwa kuwa, wanaoziendesha wanatumia
fedha kwa kuliwasiliana, kulipana posho na hata ‘kuhongana’ ili tu mambo
wanayotaka yaweze kwenda.
Tukio la kuvuliwa madaraka wa Zitto Kabwe na
tishio la kunyang’anywa uanachama sio la kwanza katika siasa za Tanzania.
Ukiachilia mbali wale waliofikwa na jambo linaloelekea kumtokea Zitto ndani ya
upinzani, wapo waliopatwa na hayo enzi za TANU na CCM chini ya utawala wa siasa
ya chama kimoja.
Wengine walilazimishwa kujiondoa wenyewe huku
wakificha sababu halisi za kujivua kwao madaraka. Wakabaki wanaishi kama
wanachama wa kawaida kwa miaka mingi. Wapo waliorudishiwa nafasi za uongozi
baada ya kupita miaka kadhaa.
Tunakumbuka jinsi wanasiasa na viongozi wengine
walivyotimuliwa uongozi na uanachama baada ya kugoma kujiuzulu wenyewe. Wapo
baadhi kwa hofu ya usalama wa maisha yao, walilazimika kuondoka nchini, na
wengine waliendelea kuishi kwa kufanya shughuli nyingine za maendeleo na maisha
yao yakasonga mbele kwa mafanikio makubwa kuliko walivyokuwa katika ulingo wa
siasa.
Yaliyopendeka haya, watanzania hawakusikia
malumbano yaliyojaa matusi, kashifa, dharau, udhalilishaji na aibu kubwa kama
tunayoshuhudia sasa.
Sitaki kusimama upande wowote, lakini swali ambalo
watanzania wanatakiwa kujiuliza bila unafiki ndani yake, ni kwamba iweje leo
wanaotuhumiwa kusaliti chama chao, ndio wanaibuka na kututangazia ‘uozo’ wa
viongozi wenzao ndani ya chama?
Kiongozi anayejaribu kuwashawishi watanzania
waamini kuwa wenzake pia ni waovu kiasi cha kuzua hata utata wa kumiliki nyumba
za umma, kana kwamba watendaji wakuu wa shirika hilo nao ni wapuuzi kiasi cha
kuingia katika mkataba tata, anatushawishi tumuaminije?
Watu makini wanaposikia kwa mfano, watuhumiwa wa
kinachoitwa usaliti sasa wakirusha kete wakidai eti kiongozi fulani naye alipewa fedha mwaka 2005
wakati wa uchaguzi mkuu, wanajiuliza huyu anayetoa tuhuma hizi leo alikuwa wapi
kuyasema miaka yote hiyo?
Ikiwa kwa mfano pana ukweli wa tuhuma za viongozi
wenzake anaowataja kupokea fedha kutoka kwa kiongozi wa CCM, sababu zipi
zilimfanya afumbe mdomo miaka yote hiyo, hadi leo anazitoa baada ya kutishiwa
kufukuzwa? Mtu gani mwenye akili timamu atamwamini tena mwanasiasa wa aina hii.
Mtu gani mwenye busara ataendelea kusadiki yale anayosema sasa na yale
atakayotamka?
Lakini kinachotisha zaidi, sasa zinapotolewa
tuhuma zinazolenga kubainisha kuwa hata kifo cha Chacha Wangwe kilikuwa na
‘mkono’ wa mtu!
Ni siasa zinazotia uchungu mkubwa kuona kwamba, kiongozi anayetaka watu wamwamini anatangaza waziwazi na kurejea leo mwaka 2014 matukio ya 2005! Alikuwa wapi siku zote? Kipi kilimzuia asiseme? Na kwa nini aseme leo baada ya kutimuliwa? Ina maana kama asingechukuliwa hatua angenyamaza? Na kwa nini alikuwa bingwa wa kurusha makombora kwa viongozi wa CCM huku akijua (kama ni kweli) kwamba na wenzake wanapokea fedha kutoka huko huko CCM?
Ni siasa zinazotia uchungu mkubwa kuona kwamba, kiongozi anayetaka watu wamwamini anatangaza waziwazi na kurejea leo mwaka 2014 matukio ya 2005! Alikuwa wapi siku zote? Kipi kilimzuia asiseme? Na kwa nini aseme leo baada ya kutimuliwa? Ina maana kama asingechukuliwa hatua angenyamaza? Na kwa nini alikuwa bingwa wa kurusha makombora kwa viongozi wa CCM huku akijua (kama ni kweli) kwamba na wenzake wanapokea fedha kutoka huko huko CCM?
Nacheka kwa uchungu kuona mtu msomi, anayetaka
demokrasia ya kweli anaibuka na upuuzi huu leo hii, na katika nyakati ambazo
watanzania wamepigika kimaisha. Ni watu wasiofikiri sawa sawa watakaomuamini
tena. Ataamini tu na watu waliochoka kimaisha, wanaokubali kuwa kapu la kubeba
kila aina ya umbea, na walio tayari kusema, kutenda na kushabikia lolote na
chochote kwa sababu wanajua wanapewa pesa. Watu wa ovyo ovyo tu!
Inatia hasira kuona kuwa wakati tunawajibika
kujadili mambo mazito ya mustakhabari wa taifa letu, anasimama kiongozi
anayetaka kuwalisha watanzania ajenda za mambo binafsi ya mtu na familia yake.
Ni upuuzi mkubwa kwa watu waliokomaa kisiasa
kujadili uzinzi bungeni ama kwenye majukwaa, bila ushahidi makini na huku
ukitambua kuwa jambo hilo sio tu litamdhalilisha anayetuhumiwa, bali familia
yake, ndugu na jamaa zake.
Zitto anataka kuwaambia watanzania kuwa wanahitaji
kujua nani mzinzi na nani mtakatifu? Yaani watanzania kweli wanafikishwa mahali
pa kulishwa utumbo wa inzi kiasi hiki?
Tuseme ukweli bila unafiki. Hivi nani anastahili
kulalamika katika hilo linaloitwa sakata la uzinzi wa Mbowe? Ni Mwigulu Nchemba
aliyesema bungeni na Zitto anatutangazia sasa, au mume wa mbunge huyo na mke wa
Mbowe? Kwa nini wamenyamaza? Mtu makini, atanyamaza. Hawezi kujibu ujinga.
Ndivyo walivyofanya mke wa Mbowe na Mume wa Joyce!
Lakini pia mtu unajiuliza, hawa wanaowatuhumu
wenzao kwa uzinzi, wao wana usafi kiasi gani basi? Ni malaika wao?
Katika haya yanayoendelea, inahuzunisha zaidi
watanzania wanapobaini kuwa nyuma ya mgogoro huu, kuna mkono wa baadhi ya
wanasiasa waliofilisika wa upande wa pili.
Tulishuhudia namna baadhi ya wanasiasa na viongozi
wa CCM wakitoa shutuma, matusi na lawama kwa uongozi wa juu wa Chadema kwa
kumwondoa Zitto katika madaraka. Swali la kujiuliza, kiliwauma nini? Walikuwa
na maslahi gani na nafasi za kiongozi huyo ndani ya Chadema?
Hivi akitokea mtu akasema, waliumia kwa sababu
walijua mtu aliyempandikiza amebainika na ndio maana wanaumia atakuwa amekosea?
Nisaidieni hivi Yule waziri wa serikali aliyetamba kuwa Chadema kitakufa kabla
ya 2015, alikuwa anajivunia nini?
Ndio alitamka waziwazi na tukasikia akitamba kuwa
atahakikisha chama hicho pinzani kinakufa! Waziri mzima, ambaye angetegemewa
asimame na kuwaeleza watanzania kuwa nia yake ya chama chake ni kuhakikisha
adui ujinga, njaa, maradhi na ufujaji wa mali ya umma vinakufa kabla ya 2015,
anakurupuka na kusema Chadema inakufa, kana kwamba ndio kansa ya maendeleo yetu
anastahili kuendelea kuwa madarakani kweli kama tuko makini na uhai wa taifa
letu?
Je, ni kweli kwamba taifa hili limefikishwa mahali
pa watu wanakufa hospitalini kwa kukosa dawa, watoto wanafeli ovyo kwa kukosa
elimu bora, walimu wanapiga mihuri ardhini (wanatembea peku) na madaktari
wanagoma kwa sababu kuna chama kinaitwa Chadema?
Leo hii mangapi yanatokea hapa nchini, tena mabaya
yanayoumiza na kuua utu na heshima yetu kitaifa na kimataifa? Leo hakuna usalama wa uhakika hapa nchini.
Mtu unalala kwa hofu, unatembea kwa hofu, unakunywa kwa hofu,na katika hali
isiyoweza kusemeka sasa wakristo wanakwenda makanisani kwa hofu kubwa!
Hawana uhakika wa kurejea nyumbani kwa
usalama. Wanasali huku wanalindwa utafikiri
ni wafungwa. Wamepigwa mabomu kanisa, wakiimba, wamepigwa risasi wakienda
kusali, wakamwagiwa tindikali bila hatia yoyote.
Leo watu wanakwiba fedha za umma mchana na usiku.
Wanahabari tunawafichua, lakini hatuoni hawa wanaoshambulia wenzao wakichukua
hatua hata za kukemea tu. Hawaoni uchafu unaofanywa ndani ya nchi. Hawaoni
wanyama wanavyoangamizwa. Wao ni kushambuliana tuu!
Badala ya watu kujadili haya, na kujua nani katufikisha
hapa achukuliwe hatua, watu wanaibuka na visa vya ovyo na tuhuma za kitoto
kabisa za fulani anazini na mke wa fulani. Si mwacheni aliyechukuliwa mke ama
mume alalamike?
Watu wazima, wasomi kabisa na watu wanaoonekana
kuwa na busara, wanashinda kutwa nzima wakihangaika namna ya kuwazushia wengine
tuhuma za kipuuzi na kujiapiza namna watakavyoizika chadema.
Nacheka kwa uchungu kila ninapowaza aina ya
viongozi na wanasiasa sasa hawana muda wa kutafuta mbinu za kuinua uchumi wa
taifa letu, njia za kuwafanya watanzania waondokane na umasikini,kuokoa
rasilimali za nchi zinazoporwa usiku na mchana, badala yake kama mazuzu
wanahangaika na vyama vya upinzani na kuendesha siasa za kuchafuana!
No comments:
Post a Comment