MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam,
imewaachia huru Waziri wa zamani, Arcado Ntagazwa na wenzake waliokuwa na
kesi na kujipatia mali kwa njia ya udanganyifu zenye thamani ya sh milioni
74.9, baada ya kuwaona hawana hatia na hawakutenda kosa hilo.
Sambamba na hilo, mahakama hiyo imemshauri
mlalamikaji katika kesi hiyo ambaye ni Noel Severe kufungua kesi ya madai
kama walivyofanya hivi karibuni, ambapo walifungua kesi ya madai dhidi ya
Ntagazwa.
Hakimu Mkazi wa mahakama hiyo, Gene Dudu, alisema
kuwa kesi hiyo ya jinai namba 108/2012 aliyoitolea hukumu jana, haikupaswa
kuwa jinai bali ya madai.
Akisoma hukumu hiyo, saa tano asubuhi, Dudu alisema
upande wa Jamhuri uliokuwa ukiwakilishwa na Wakili wa Serikali, Charles
Anindo, katika harakati zake za kutaka kuthibitisha kesi yake ulileta
mashahidi watano wakati upande wa washitakiwa waliokuwa wanatetewa na wakili
wa kujtegemea, Alex Mshumbusi, ulileta mashahidi wanne, ambao ni washitakiwa
wenyewe na shahidi mmoja.
Hakimu Dudu alisema mahakama yake ilipata fursa ya
kuchambua ushahidi wa pande zote mbili na mwisho wa siku ikabakiwa na swali
moja la kujiuliza kuwa, je, ni kweli washitakiwa hao walitenda kosa kinyume
cha kifungu cha 320 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002?
Aliongeza kuwa kwa mujibu wa kifungu hicho ni lazima
mtuhumiwa awe ametoa taarifa za uongo kwa mlalamikaji ili ajipatie kitu
fulani kwa njia hiyo ya uongo na awe na nia ovu wakati akitaka kujipatia mali
hizo.
“Lakini kwa mujibu wa ushahidi uliopo mahakamani,
imeonesha wazi kabisa Ntagazwa na mshitakiwa wa pili ambao ni wajumbe wa bodi
wa taasisi ya Ford walitoa oda kwa Kampuni ya Visual Storm ambayo Mkurugenzi
wake ni Severe, ya kuomba watengenezewe fulana 5,000 na kapelo Korea 5,000,
ambapo walifanya hivyo baada ya kikao cha bodi kutenga bajeti ya kutengenezwa
kwa mavazi hayo.
“Mavazi hayo yaligawiwa bure kwa umma siku ya
kumbukumbu ya kifo cha hayati Julius Nyerere, wakiwa na lengo la kutokomeza
ufisadi wakati wa kumuenzi kiongozi huyo, kwa ahadi kuwa wangelipa ndani ya
mwezi mmoja,” alisema Dudu.
Alisema hoja ya kwamba mshitakiwa wa tatu ambaye ni
mtoto wa Ntagazwa, Dk. Webhale Ntagazwa, kuwa ndiye alitoa oda ya kuchapwa
kwa fulana na kofia hizo, hakustahili kushitakiwa kwa kosa hilo kwa sababu
Ford ni taasisi na si mali ya mshitakiwa.
Dudu alisema utetezi wa washitakiwa unaonesha
waliandika barua kwa wafadhili wakiomba fedha za kuweza kufanikisha mradi wao
wa kutaka kumuenzi Nyerere siku ya kumbukumbu ya kifo chake Oktoba 14, na
wafadhili hao waliwakubalia waendelee na taratibu za kuchapisha fulana na
kwamba watatoa fedha za kulipia.
Lakini kabla ya tamasha kufanyika, Ntagazwa na
wenzake walishtukia fulana zao hizo zikibadilishwa nembo na kuonekana ni za
Chama Cha Jamii (CCJ), hali iliyosababisha mfadhili aliyewaahidi fedha
kujitoa akidai hawafadhili vyama.
“Mahakama hii imeona habari hiyo iliyochapishwa
kwenye gazeti la Mtanzania, ambapo hata washitakiwa waliandika barua kwa IGP
Said Mwema kulalamika fulana na kofia zao kuhujumiwa, hivyo kusababisha
washitakiwa wajikute wakishindwa kulipia gharama za uchapishaji kwa kampuni
ya Severe baada ya mfadhili wao kujitoa,” alisema.
Baada ya hakimu huyo kusoma hukumu, Ntagazwa
aliangua kilio nje ya mahakama akisema: “Yaani kumuenzi Nyerere ndiko
kulikosababisha nifunguliwe kosa la jinai? Tena polisi walivyo na roho mbaya
na katiri siku wanakuja kunikamata nyumbani walinikamata uchi wa mnyama
nikiwa bafuni naoga kwa sababu nimehamia CHADEMA.”
Mbali na Ntagazwa, washitakiwa wengine ni mtoto
wake, Dk. Webhale Ntagazwa na mshitakiwa wa kwanza ni Senetor Mirelya (60).
Aprili 23, mwaka 2012, ilidaiwa mahakamani hapo na
wakili wa Serikali, Ladislaus Komanya, kuwa Oktoba 22 mwaka 2009 huko Msasani
Mikoroshini, washitakiwa hao kwa nia ovu walijipatia fulana 5,000 na kofia
5,000 zenye thamani ya sh milioni 74.9 kutoka kwa Noel Severe, kwa
makubaliano kuwa wangemlipa katika kipindi cha mwezi mmoja tangu walipochukua
vifaa hivyo lakini walishindwa.
|
NDOA YANGU, Ningejua!
NTAGAZWA ASHINDA KESI
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment