WAKATI Rais Jakaya Kikwete na Waziri wa Nishati na
Madini, Prof. Sospeter Muhongo, wakiwabeza Watanzania kuwa hawana uwezo wa
kifedha kuwekeza katika utafiti wa gesi na mafuta, mwanasheria maarufu
nchini, Mabere Marando, ametoboa siri za vyanzo vya fedha za wawekezaji wa
nje wanaopigiwa debe na serikali.
Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika
katika viwanja vya stendi ya Kibiti wilayani Rufiji juzi, Marando alisema
wawekezaji wengi kutoka nje hawaji na fedha mifukoni, badala yake wanatumia
mabenki ya hapa nchini kujipatia mitaji hiyo, jambo alilodai kuwa linaweza
kufanywa na wawekezaji wazawa.
Marando ambaye pia ni mjumbe wa Halmashauri Kuu wa
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na Makamu Mwenyekiti wa chama
Kanda ya Pwani, alisema serikali imeshindwa kuwasaidia wazawa kwa
kuwachukulia dhamana ya kukopa mitaji mikubwa kama inavyofanywa na nchi
nyingine.
Kwamba badala ya kuwawezesha imegeuka kuwasimanga
na kuwabeza kuwa hawana uwezo wa kifedha wa kampuni zao kushiriki katika
michakato hiyo ya kupewa vitalu vya utafiti wa gesi na mafuta. Alisema hali
hiyo ni makusudi ya serikali ya CCM kuwazuia Watanzania kutumia fursa
zilizopo na badala yake inakimbiza fursa hiyo kwa wageni.
“Niliposikia rais akitoa kuli hiyo niliumia sana
lakini nikaja kutambua kuwa huyu mtu hakuwahi kupigika katika maisha ya
tabu na wala hajawahi kufanya biashara kwa maana hao wageni aliokuwa nao
juzi wengi wao wakiwa wanataka vitalu, mimi nimewaandalia nyaraka za kukopa
katika mabenki yetu nchini,” alisema.
Marando aliongeza kuwa mmoja wa waombaji hao wa
uwekezaji katika vitalu vya gesi, ameweka leseni ya kampuni yake kama
dhamana katika moja ya benki hapa nchini ili aweze kupata mkopo, jambo
aliloeleza kuwa linaweza kufanywa na Watanzania wengi wenye dhamana za
kutosha.
Aliongeza kuwa sera ya CHADEMA ni kuwapa
kipaumbele wazawa badala ya wageni katika kumiliki vyanzo vya rasilimali
hali aliyoeleza kuwa ni tofauti na serikali ya CCM.
Marando alisisitiza kuwa makubaliano ya uwekezaji
wa eneo lolote nchini unapaswa uanzie kwa mwekezaji kukubaliana na mmiliki
wa eneo analotaka kuwekeza tofauti na ilivyo sasa kwa serikali kuamua bila
kuwashirikisha wananchi.
Alitolea mifano uamuzi wa serikali kushindwa
kuwashirikisha wananchi katika hatua za awali ni matokea ya migongano ya
mara kwa mara baina ya wawekezaji na wananchi wa maeneo husika.
|
No comments:
Post a Comment