Social Icons

NDOA YANGU, Ningejua!

NDOA YANGU, Ningejua!

JK AHOFIA CCM KUANGUKA 2015





Asifu wapinzani kutembelea wananchi

Mwenyekiti wa CCM taifa Rais Jakaya Kikwete, amekiri kuwa CCM itaanguka katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 kutokana na kukithiri kwa rushwa miongoni mwa watendaji wa chama hicho.

Kikwete alisema kuwa kwa sasa  chama hicho kikongwe kimepoteza matumaini kwa watanzania kutokana na vitendo visivyo vya kiungwana vinavyofanywa na watendaji ndani ya chama.

 Alisema hata kama itatokea kwa chama hicho kushinda uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 kama tabia walizonazo watumishi na viongozi hazitabadilika ni wazi hakitapita kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2020.

Rais Kikwete, alitoa onyo hilo juzi usiku, alipofunga mafunzo maalum ya siku nne kwa makatibu wa mikoa, makatibu na  wenyeviti wa wilaya wa chama hicho nchini mkoani Dodoma.

“Kama hatutabadilika katika suala la rushwa mwaka 2015 tutakuwa na wakati mgumu sana na kama  mwaka huo tutafanikiwa kuishika Serikali basi mwaka 2020 hatutarudi tena madarakani.

“Najua rushwa ipo na mnaendelea kupokea shilingi laki mbili za airtime (muda wa mawasiliano). Jueni kwa mtindo huu hatutafika ama wengine watavuka na wengine kukwama.” Alisema na kuongeza;

“Viongozi wa chama ndiyo mmekuwa mawakala wa kusambaza rushwa bila hata aibu, nawaombeni tubadilike kama tutaendelea hivi hali yetu itakuwa ngumu sana katika chaguzi mbalimbali nawaambieni,”alisema.

Mbali na hilo alisema kuwa inasikitisha kuona kuwa wapo baadhi ya watu ambao wameanza kujipitisha katika viongozi wa chama na kuwapatia hela kwa ajili ya kuwapigia debe ili wawachague katika nafasi mbalimbali za urais ama ubunge.

Alisema kuwa kimsingi kwa sasa wapo watu ambao wameisha anza kuzunguka na kujinadi kutafuta nafasi mbalimbali za kugombea huku wakipenyeza rushwa jambo ambali linaendelea kukishushia adhi chama hicho.

Akizungumzia chuki ndani ya chama alisema watanzania kwa sasa wana akili zao na hawataki kudanganywa.

“Wapo badhi ya viongozi ndani ya chama hawajui hata Ilani ya chama chao wakipanda kwenye majukwaa wanaanza kuzungumzia ujenzi wa daraja la Mkapa ama lile la Malagarasi, watu hawataki kusikia hayo mtu wa Ngara anataka kujua daraja lake limeishaje siyo la Mkapa” alisema

Hata hivyo alisema wazi kuwa kwa sasa vyama vya upinzani vinafanya kazi kubwa zaidi ya kuwatembelea wananchi na kusikiliza kero zao tofauti na ilivyo kwa chama cha mapinduzu kwani kwa sasa CCM viongozi wake wapo mbali na wananchi.

“Nataka niwaambie vyama vya upinzani vinafanya kazi kubwa na wanafika hatua ya kuaminika kwani wanapokwenda kwa wananchi wanaambia kuwa CCM inafanya kazi za maendeleo kwa shinikizo la vyama vya upinzani na wananchi wanaamini.

“Wananchi kwa sasa wanataka maendeleo na kusikilizwa. Kwa sasa ukienda polisi umwambie RPC akuoneshe ratiba za mikutano utaona  orodha ndefu ya mikutano ni ya vyama vya upinzani CCM hawapo mnafikiri hapo mtashinda.

“’Wapo watu ambao wanadai kuwa chama kitafia mikononi mwangu nataka niseme kuwa chama hakifii mikononi mwangu kitafia mikononi mwenu” alisisitiza Mwenyekiti wa chama hicho taifa.


Kikwete alisema kuwa siku hizi watu wana mbadala wa vyama vingine na siyo CCM peke yao.

“Tuna vijana wengi kutoka katika vyuo mbalimbali ambao wanaweza kufanya kazi kwa uadilifu wa hali ya juu hivyo hatuna budi kuachana na hawa wala rushwa ambao watatupotezea sifa yetu kwa wananchi.

“Tukipoteza Urais ndiyo tumekwisha na chama kinaweza kufa.”
 Katika hatua nyingine Kikwete  aliwaonya viongozi ambao wanajihusisha na uuzaji wa mali za chama kama vile viwanja na baadhi yao kuingia mikataba yenye utata.

“Kuna watu wanapoingia mikataba sijui wanakuwa wamelewa...kwanza unashindwa hata kuelewa...kwa mfano utakuta mtu alipangishwa jengo la CCM kwa miaka 264 sasa unawaza huu mkataba wa aina gani kwa sisi tuliopo hapa miaka 50 ijayo hakuna atakae kuwepo duniani sasa mmiliki wa lile jengo atakuwa nani,?” alisema

Hata hivyo, aliwataka makatibu hao na wenyeviti wa wilaya na mikoa kuhakikisha wanawatembelea wanachama wao na kutafuta wanachama wapya kwa ajili ya kujiimarisha kwa chaguzi mbalimbali zijazo.

“Viongozi wengi hatuna tabia ya kuwatembelea wanachama wetu na kuwatatulia kero zao hali ambayo inatugharimu wakati wa uchaguzi kupata kura kidogo tofauti na idadi ya wanachama tulionao,” alisema na kuongeza kuwa;

“Wenzenu wakiendelea kutembelea wanachama na kutisha mikutano, nyie mnabakia kuimba wembe ni ule ule ushindi, shauri yenu mtakatwa,”alisema.

Alisema wapinzani  wanarikodi ya kufanya vizuri kwa kufanya mikutano kuliko viongozi wa CCM.

Aidha, alisema iwapo hawatafanya kazi vizuri chama hakitaweza kufanikiwa na kuwataka kutumia maarifa waliyopata katika mafunzo hayo kuhakikisha chama kinakuwa imara na chenye uwezo wa kuongoza.
"Lazima muendelee kuongeza wanachama sio kupanda majukwaani na kuimba iyena iyena...Utendaji mpya wa kuongeza wanachama na kuwatambua na kuwapa majukumu,"alisema.

 Mwisho

No comments:

Post a Comment