Serikali
yashitakiwa The Hague
Na Nasra Abdallah
MAUAJI ya Mwandishi wa habari wa kituo cha Luninga cha
Channel Ten, Daudi Mwangosi nay a raia wengine yamezidi kuichafua serikali ya
Tanzania, na sasa imefunguliwa mashitaka katika Mahakama ya Uhalifu ya
Kimataifa(ICC) iliyoko The Hague.
Mbali na mashitaka hayo yaliyopelekwa huko tangu
Septemba 28 mwaka huu, Tanzania pia imeshitakiwa kwenye Tume ya Afrika ya Haki
za Binadamu.
Mashtaka hayo yalifunguliwa na Kituo cha Haki za
Binadamu, ambapo Mkurugenzi Mtendaji wake Hellen Kijo-Bisimba,alisema
wamezitaka mamlaka hizo za kimataifa
kufanya uchunguzi na kuichukulia
hatua stahiki za kisheria Serikali ya Tanzania.
Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu(LHRC) kimechukua
hatua hiyo, kutokana na kuongezeka kwa mauaji ya raia wakiwa katika mikono ya
vyombo vya dola, huku serikali ikigwaya kuwachukulia hatua za kisheria
waliohusika na mauaji hayo.
Hatua hiyo nzito na ya kwanza katika historia ya
Tanzania, imekuja huku kukiwa na kusigana kwingi kwa ripoti ya serikali
iliyoundwa na Waziri wa Mambo ya Ndani, Emmanuel Nchimbi na ile ya Tume ya Haki
za Binadamu na Utawala Bora iliyoongozwa na Jaji Kiongozi Mstaafu, Mussa
Kipenka.
Wakati ripoti ya Serikali chini ya Jaji Mstaafu Ihema,
ikionekana kuwatetea askari Polisi waliohusika na mauaji hayo, na kusukuma
lawama kwa chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ile ya Jaji Kipenka,
imembebesha lawama Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa iringa, Kamuhanda kwa kuhusika na tukio hilo huku
ikikisaficha Chadema.
Ripoti
ya serikali ambayo imewachanganya watanzania na wanasheria wengi, imedai kuwa
"nguvu za kupita kiasi zilizotumiwa na polisi hazikusababisha kifo cha mwangosi", lakini ikishindwa kuweka
wazi kilichosababisha kifo chake kwa madai kwamba shauri hili liko mahakamani
Hata hivyo, Ripoti ya Jaji Kipenka imeanika ukweli wote
na kuwalaumu polisi, msajili wa vyama vya siasa na mamlaka za ulinzi na usalama
za mkoa wa Iringa kwa kukiuka misingi ya haki za kuishi, haki za kukusanyika na
sheria ya sensa ambayo ilitumiwa na baadhi ya mamlaka kuzuia shughuli za
Chadema.
Kadhalika, Ripoti ya Jaji Mstaafu Kipenka alisema wazi
kuwa uchunguzi umebainisha kuwa Chadema walikuwa na haki ya kufanya shughuli
zao za kisiasa kwa mujibu wa sheria na ilikuwa ni makosa kwa mamlaka kuwazuia
kwa sababu za sensa.
Pamoja na hatua ya kushtakiwa kwa serikali katika
mamlaka hizo za dunia, Bisimba alisema bado wanataka kuona viongozi wote wa
Serikali na vyombo vya dola waliohusika kwa namna yoyote na mauaji ya Mwangosi
na raia wengine wakiwajibishwa.
Bisimba alisema hawaoni sababu za viongozi hao
kutojiuzulu ama kuachishwa kazi na kufikishwa mahakamani kujibu tuhuma hizo.
Aidha Mkurugenzi huyo aliitaka Serikali kuacha
propaganda zinazotaka kuchochea vurugu katika Taifa ambazo hazina tija na
kutaka itambue kuwa sasa ni wakati wa mfumo wa vyama vingi hivyo ni vyema
ikaacha kutumia vyombo vya dola katika kuleta chuki na mafarakano katika jamii
yanayohatarisha usalama na amani ya watanzania.
Tangu kumalizika kwa uchaguzi mkuu mwaka juzi, kumekuwa
na mauaji ya raia yenye sura za kisiasa, mengi yakitokea katika mikutano,
maandamano na mikusanyiko inayofanywa na Chadema.
Vifo hivi ni vile
vilivyotokea mkoani Arusha, Januari 5, 2011 ambapo watu watatu waliuawa kwa
risasi na polisi katika maandamano ya chadema, wialayani Igunga Novemba 2011,
baada ya kada wa Chadema kuuawa kinyama na watu wasiojulikana na Arumeru Mashariki Aprili 2012 baada ya kuuawa
kwa mwenyekiti wa Chadema wa Kata.
Mauaji mengine ni yale
yaliyotokea Iramba mwezi Julai 2012 kufuatia kucuka kwa vurugu
katika mkutano wa Chadema ambapo kada mmoja wa CCM aliuawa, Agosti 27, 2012
mkoani Morogoro baada ya kuuawa kwa muuza magazeti na hivi Septemba 2, 2012
mkoani Iringa kwa mwandishi David
Mwangosi.
Mwandishi
akana kuhojiwa na kamati ya Nchimbi
Katika hatua nyingine, mwandishi wa habari wa gazeti
hilo, Abdallah Khamis amekanusha taarifa ya ripoti ya Kamati ya Nchimbi
kuhusiana na kuhojiwa kwake.
Abdallah alisema kuwa yeye alipigiwa simu na mmoja wa
wajumbe wa kamati ya nchimbi akiambiwa ajiandae kukutana na kamayi hiyo, lakini
hakuitwa tena baada ya hapo.
Badala yake, alisema kuwa aliitwa na kuhojiwa na kamati
ya baraza la habari Tanzania (MCT) na kutoa maelezo yake.
Mwandishi huyo ambaye alikuwa na marehemu Mwangosi
tangu kukamatwa, kupigwa na hata kuuawa kwake, ameonesha mshangao wa ajabu
kutokana na taarifa ya kamanda Kamuhanda kwamba hakuwahi kuambiwa na mwandishi
yoyote kwamba aliyekuwa akipigwa na askari ni mwandishi wa habari.
No comments:
Post a Comment