Social Icons

NDOA YANGU, Ningejua!

NDOA YANGU, Ningejua!

Mnyika akoswa na Bomu.



Mbunge wa Ubungo John Mnyika amenusurika kupigwa na bomu lililorushwa kutoka kwenye gari ya polisi viwanja vya Sahara jijini Dar es Salaam, badala yake bomu hilo lilimlenga mtu aliyekuwa karibu na Mnyika anayeitwa Thomas Jerome, aliyejeruhiwa sehemu ya paja. Baada ya kutokea tukio hilo Polisi waliwahi kutaka kkumchukua majeruhi huyo na kumweka kwenye gari lao, lakini Mnyika aliwaelekeza wafuasi wa Chadema kumchukua majeruhi huyo kwani polisi wangemchukua wangeficha ushahidi wa jambo hilo. Wafuasi wa Chadema walimchukua na akafanyiwa taratibu za kupelekwa hospitali, hali yake inaendelea vizuri na Chadema wamesema watalilipeleka suala hilo kisheria.
Akielezea jinsi suala hilo lilvyotokea akiwa katika Mkutano mwingine Ubungo, Mnyika alisema Polisi walifika katika viwanja vya Sahara wakiwa na magari matatu wakiwa na lengo la kuja kutawanya wafuasi wa Chadema wasifanye Mkutano huo kwa kigezo kuwa kulikuwa na ziara ya makamu wa Rais katika Wilaya ya Kinondoni, maeneo ya Kinondoni na Kawe, wala sio Ubungo ambapo yeye alikuwa anafanya Mkutano. “Nikiwa nimejiandaa kupanda jukwaani ndio polisi walikuja kusema tuache tusifanye Mkutano, nilisogea karibu na gari kumlalamikia afisa wa polisi kwani kitendo cha kuahirisha mkutano kwa barua waliyoileta saa sita mchana siku ya mkutano wakati sisi tuliwapa taarifa siku nne zilizopita ilikuwa sio haki, nilimwambia Afisa huyo wa Polisi, nilikuwa najadiliana kwa simu na viongozi wakuu wa jeshi  la Polisi kanda maalumu ya Dar es Salaam, na Inspekta Jenerali wa Polisi Saidi Mwema kuwa huku ni kutumika vibaya kwa jeshi la polisi, nilipokuwa bado najibizana naye bila fujo zozote bomu lilirushwa kutoka ndani ya gari ya polisi na kupita karibu na mimi likamjeruhi mtu aliyekuwa karibu yangu na kumjeruhi”
Katika purukushani zilizotokea baada ya bomu kupigwa, Mnyika alipoteza nyaraka mbalimbali alizokuwa amebeba kama ushahidi kuwaonyesha wafuasi wa Chama hicho hasa jinsi serikali ya CCM na wabunge wake walivyopitisha kodi ya huduma za simu, na kodi ya laini za simu, kufuatia hali hiyo, Mnyika aliishia kuwatajia wafuasi wa Chama hicho namba za Mwenyekiti wa kamati ya Bajeti, Mbunge wa Bariadi Andrew Chenge ili aweze kujibu maswali ya wananchi kuhusu kodi hiyo kandamizi kwa watanzania masikini. Alisema kuwa Mbunge yeyote wa Chama cha Mapinduzi au Kiongozi yeyote anayepinga kodi ya huduma za simu na kodi za laini za simu ni mnafiki kwa kuwa walipitisha wote kwa kura za ndio, tena baada ya kumshauri waziri wa fedha Wiliam Mgimwa, na Spika akakiuka utaratibu wa kanuni akasema wote waliokuwa na majedwali ya mabadiliko kuhusu sheria hiyo walipaswa kupeleka kwenye kamati badala ya kujadiliwa bungeni kwa uwazi, “sasa mimi sio mwenyekiti wa kamati, na kikanuni sipaswi kusema hayo yaliyojiri kwenye kamati, muulizeni Chenge”
Aidha, Mkutano huo ambao awali ulitangazwa kuwa ungehutubiwa na Katibu Mkuu wa Chama hicho Dk Wilbrod Slaa, haukuweza kuhutubiwa na Dk Slaa kwa kile alichosema kuwa watu wake wa usalama walimwambia mapema kuwa katika huo mkutano hali sio salama. “nilipata taarifa toka vyanzo vyangu kuwa polisi walikuwa na mpango wa kuleta fujo, hivyo nikaona kwa kuwa wanatuwinda nisingeenda kuhutubia, pengine bomu lililomkosa Mnyika lilikusudiwa kwa kiongozi huyo au mwingine” alisema Dk Slaa alipoongea na gazeti hili kwa njia ya simu baada ya kutoonekana Mkutanoni.
Jeshi la Polisi, kanda maalumu Dar es Salaam, jana liliahirisha mkutano wa Chadema kabla viongozi hao kupanda jukwaani, uliokuwa unapaswa kufanyika katika viwanja vya sahara Jijini Dar es Salaam, ingawa walishindwa kuzuia kabisa mikutano isifanyike baada ya Chadema kuwa wameomba vibali viwili maeneo tofauti, baada ya kuzuiliwa Mabibo, kibali cha Ubungo kilikuwa halali, hivyo Mbunge wa Ubungo aliyekuwa amefika Sahara mabibo kwa ajili ya kuhutubia aliandamana kwa miguu na wafuasi wa Chama hicho hadi Ubungo, huku kukiwa na makachero wengi wa polisi waliofuatilia maandamano hayo
Akizungumza na wananchi katika mkutano mwingine uliofanyika Ubungo baada ya ule wa Mabibo kukataliwa na polisi, Mbunge wa Ubungo John Mnyika alisema, Polisi walifanya kitendo cha kikatili, kusubiri watu wamalize maandalizi, wakusanyike uwanjani ndipo wanaleta barua ya kupiga marufuku mkutano kwa kisingizio kuwa katika Wilaya ya Kinondoni kulikuwa na ziara ya makamu wa Rais katika Jimbo la Kawe na Kindondoni. “Sisi tupo Ubungo, makamu wa Rais yupo Kawe na Kinondoni, sasa suala la kuzuia mikutano isifanyike lilikuwa na maana gani? Kama Jeshi la Polisi walisema hawana askari wa kutosha kulinda mkutano wetu mbona katika kuutawanya wamekuja na magari matatu? Alihoji Mnyika.
Chadema walikuwa wamepeleka taarifa kwa jeshi la Polisi tangu tarehe 17 Julai kwamba wangefanya mkutano katika viwanja hivyo tarehe 21 Julai 2013, lakini jeshi la polisi halikuwajibu hadi walipokuwa wanaenda mkutanoni ndio walipelekewa barua ya jeshi la Polisi yenye kumb. Na.DSM/KINONDONI/SO/7/2/CHADEMA/309, inayosema  “kumbuka barua ya tarehe 17 Julai, yenye kumb. CHADEMA/MKT/UBUN/015/2013 uliyomwandikia kamishna wa polisi kanda maalumu Dar es Salaam, Kamishna wa polisi kanda maalumu ya Dar es salaam amezuia kufanyika kwa mkutano huo tarehe 12 Julai 2013 katika viwanja vya Sahara, Mabibo kwa sababu siku mliyoomba kufanya Mkutano wenu wa hadhara, Wilaya ya Kinondoni ina mapokezi ya ugeni wa ziara ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.”
Mnyika alitumia muda mwingi kulilaumu jeshi la polisi kwanza kwa kuahirisha mkutano muda mfupi  kabla ya viongozi kupanda jukwaani, lakini alilaani  kitendo cha kurushiwa bomu mahali ambapo hakukuwepo fujo zozote, isipokuwa kulikuwa na utendaji mbovu wa polisi.

No comments:

Post a Comment