Social Icons

NDOA YANGU, Ningejua!

NDOA YANGU, Ningejua!

BISIMBA: Tanzania iwe na rais Mwanamke


Hellen Kijio- Bisimba:

Tanzania iwe na Rais Mwanamke

Ni mmoja kati ya wanawake wasomi wakubwa hapa nchini, mwenye kiwango cha elimu ya udaktari katika sheria. Ni mwana harakati maarufu na mashuhuri ambaye msimamo na kauli zake katika kupigania haki zimewatisha na kuwatikisa viongozi walafi, wabadhilifu na wazembe.

Ni mtu anayestahili kupewa hadhi zote za usomi, kwa maana kwamba sio tu katioka sheria, bali amebobea pia katika mambo ya elimu hususan katika shule za sekondari na vyuo. Akazama zaidi katika ujuzi na weledi katika masuala ya haki za watoto, na mambo ya ardhi
Ujasiri wake katika kupigania mambo ya msingi, haki, maendeleo ya wananchi hususan makundi yanayoonewa, wakiwemo wanawake na watoto, uliusukuma Umoja wa Mataifa kumpa tuzo ya mwanamke jasiri mapema mwaka jana.
Huyu ni Hellen Kijo-Bisimba, ambaye ni mmoja ya matunda ya shule ya sekondari ya wasichana ya Weruweru iliyoko mkoani Kilimanjaro, iliyotimiza miaka 50 tangu kuanzishwa kwake.
Kabla ya kuingia katika ulimwengu wa kazi na wajibu nyingine za kuwa mke na mama wa familia, Hellen Kiji-Bisimba aliyezaliwa Oktoba 10, 1954 amepata kufanya kazi sehemu mbalimbali, kuandika vitabu na machapisho kadhaa yanayohusu elimu, haki za watoto na ardhi.
Hakuna shaka kwamba mafanikio makubwa aliyonayo, yanatokana na msingi mzuri na imara wa elimu ya sekondari aliyoipata katika shule ya sekondari ya wasichana Weruweru alikosoma hadi kidato cha nne kisha kufaulu na kuingia kidato cha tano na sita katika shule ya sekondari  Korogwe alikohitimu mwaka 1974.
Alipata stashahada ya elimu kutoka chuo cha ualimu, mwaka 1977, kabla ya kubadilisha taaluma na kuchukua masomo ya sheria toka chuo kikuu cha Dar es salaam na kupata shahada yake mwaka 1985.
Akisukumwa na kiu ya masomo, alihitimu shahada ya uzamili katika sheria kutoka chuo kikuu cha Dar es salaam mwaka 1994 na akatimiza ndoto yake baada ya kupata shahada ya uzamivu (Doctor of Philosophy in Law) PhD kutoka chuo kikuu cha Warwick, (UK) mwaka  2012
Katika mahojiano maalum na Tanzania Daima, Bisimba haachi kusema kile anachoamini kuwa msingi wa mafanikio, maendeleo yake binafsi, ya wanafunzi wenzake waliosoma shuleni Weruweru; lakini zaidi akikosoa kile anachoamini kimechangia sana kuangusha fani nzima ya elimu hapa nchini.

Tanzania Daima: Wanafunzi waliochaguliwa kujiunga Weruweru nyakati zenu walijisikiaje, kulinganisha na wale waliokwenda shule nyingine?

Hellen: Wanafunzi waliochaguliwa kujiunga Weruweru wakati huo ikiwa Assumpta College walijisikia vizuri sana. Kwenda shule hiyo ilimaanisha kuwa ulifanya vizuri sana hasa kwenye masomo ya Kiingereza na Hesabu. Mimi nilijiunga mwaka mmoja kabla haijawa Weruweru (1969)

Tanzania Daima: Hali ya ushindani ilikuwaje? Uliwahi kuchaguliwa kushika wadhifa wowote shuleni.

Hellen: Hali ya ushindani shuleni ilikua zaidi kati ya wale waliokuwa wanasoma Sayansi na wale wa Arts. Waliokuwa wanasoma Arts walijaribu kuwaonyesha wa Sayansi kuwa hata nao wana uwezo kwa vile wa sayansi walionyesha wao ndio wasomi zaidi.

Sikuwahi kushika wadhifa wowowte maana nilikua mtoto mpekupeku sana, hivyo isingekua rahisi kupewa hata ‘umonita’ tu.

Tanzania Daima: Hali ya ufundishaji na mazingira ya shule yalikuwa ya aina gani; je, yaliwapa hamasa ya kusoma ama mlifanya hivyo kwa sababu ya woga wa wazazi/walimu?

Hellen: Hali ya ufundishaji ilikua ni nzuri sana.Tulikua na Waalimu kwa kila somo na vitabu vya kiada na ziada. Tulikua na maktaba nzuri sana. Kila siku jioni tulikua na muda wakujisomea (PREP.) Mazingira ya shule yalikua safi sana na shule ilikua chini ya Mlima Kilimanjaro kwa hiyo majira ya usiku ukiangalia unaona mlima unang’aa   inapendeza sana.

Usafi wa shule ulikua si wa kawaida kwani Sehemu za vyooni tuliweza kutumia kujisomea usiku kwa vile taa za vyoo zilikua hazizimwi. Mandhari ya shule ilikua na miti na ukoka mzuri sana na maua siku ya kutembelewa tunakaa na wageni wetu kwenye ukoka chini ya miti. Mabweni yalikua si mambwalo kwa maana ya hanga kubwa lililo wazi. Yalikua katika mfumo wa vyumba vidogo tukiviita ‘cubicles’ ambapo wasichana watatu huishi kwenye chumba kimoja kwa viongozi na wadada wa form four (kidato cha nne) wao walikua wanaishi wawili tu.

Tulikua  tunahamasishwa sana kusoma tukiambiwa kuwa elimu tu ndio itatukomboa watoto wa kike. Hatukulazimishwa lakini mazingira yalifanya tu uwe na hamu ya kusoma.

Tanzania Daima: Unadhani kipi kilichangia kuporomoka kwa umaarufu wa shule hiyo?

Hellen: Kuporomoka kwa shule hiyo kumechangiwa na mambo mengi, moja mabadiliko ya kuifanya shule kuwa ya ’high school’ tu na si kuanzia kidato cha kwanza.  Pia serikali kutojali shule zake kama ilivyokuwa hapo mwanzo

Tanzania Daima: wanafunzi ambao kwa sasa mnalitumikia taifa kwa nyanja mbalimbali, unaweza kusema mmelisaidia taifa kuinuka kimaendeleo kwa kiwango gani?

Hellen: Sisi wanafunzi wa Weruweru tulioko katika utumishi sehemu mbali mbali tumetoa mchango mkubwa sana kwa taifa kuinuka kimaendeleo kwani wengi wetu tumekuwa viongozi  popote tulipo. Na uongozi wa wengi wetu umekuwa mzuri kwamba huwezi kusikia masuala ya ubadhirifu.

Tumewajengea uwezo wengi ambao wamefanya mengi katika kuendeleza familia zao na sehemu walipo ambapo ndio mchango katika  maendeleo ya nchi kwa ujumla. Kuwa tu na watoto ambao nao wameelimika na wanafanya kazi kujenga taifa pia ni mchango mkubwa.

Tanzania Daima: Unajisikiaje unapowaona wanafunzi wenzako wakiongoza kwa ufanisi katika nafasi walizonazo?

Hellen: Ninasikia fahari sana kuona wenzetu wengi wakiwa katika nafasi za uongozi na wakiongoza kwa ufanisi sana na penda sana kuwatambulisha kama wasichana wa Weruweru.

Tanzania Daima: Unadhani elimu yetu imepanda ama imeporomoka? Kama imeporomoka unadhani ni kwa sababu gani?

Hellen: Elimu yetu imeporomoka. Kwanza kwa kukosa utashi wa kisiasa wa kuikuza na kuiendeleza. Kuwakosea waalimu ambao ndio nguzo katika elimu. Mawaziri kufanya watakavyo katika mitaala kwa kuondoa masomo muhimu, kuchanganya masomo na kadhalika. Pia kuwepo na shule binafsi zinazojiamulia masomo kwa kadri ziwezavyo na wakubwa kuwa na nafasi kupeleka watoto wao kusoma nje.

Tanzania Daima: Wanafunzi wengi wa elimu ya juu sasa wamezama zaidi kusoma masomo yale wanayodai 'yanalipa zaidi', je hii inasababishwa na nini?

Hellen: Hii inasababishwa na  kazi zote kutothaminiwa sawa lakini pia kuwepo na mianya  ya kazi fulani fulani kuonekana ndio zenye bei kwa maana ya njia za kupata fedha kwa urahisi wakati nyingine zikiangaliwa kama kazi kavu. Kazi zote hazipewi hadhi sawa kimaslahi na hata kiheshima.

Tanzania Daima: Nini mtazamo wako kama mwanamke msomi, kuhusiana na mwenendo mzima wa utawala na uendeshaji wa siasa ya vyama vingi nchini?
Hellen: Inasikitisha kuwa mfumo wa siasa za vyama vingi ulikubalika kisheria lakini kiutashi ulikua haujakubalika kwa wale waliokua madarakani na kwa sababu hii mfumo huu umekua ukinyimwa nafasi ya kukua na kufikia dhima yake. Unaonekana kama ni uadui na haupati kabisa nafasi ya kutosha kufanya yale yanayotarajiwa katika mfumo wa siasa ya vyama vingi. Badala ya demokrasia kukua inasinyaa.

Tanzania Daima: Je, kwa imani na mtazamo wako, unaamini na ungependa rais ajae awe mwanamke? Kama ndio, unawafikiria akina nani walio katika vyama ama nje wanafaa kuongoza?

Hellen: Ingefurahisha sana kama tungepata rais mwanamke katika uchaguzi ujao. Si rahisi kufikiria watu kwani inategemea sana na mtu mwenyewe kama ana njozi hizo au la, ila tukiangalia kwa uwezo wapo wengi wanaoweza kuwa marais. Mfano Ana Tibaijuka, Mama Getrude Mongela , Dr. Asha rose Migiro.

Tanzania Daima: Kukithiri kwa matukio ya biashara ya dawa za kulevya, utoroshaji wa nyara za taifa, unadhani kunachangiwa na ukosefu wa elimu, maadili ama tamaa na kunatoa ishara gani kwa vijana wetu?

Hellen: Hili ni tatizo la tamaa na ubinafsi kuwa mtu anachojali ni yeye kupata mali bila kuangalia athari kwa wengine na kwa taifa kwa ujumla. Ishara iliopo ni  kuuawa kwa kizazi kijacho kwani vijana wengi nao wangependa kupata mali kwa haraka haraka na wakati hu huo kujiingiza katika kutumia madawa yanayopotea  uwezo kiakili na hata kimwili hatima yake ni kuwa na taifa la mateja. Mungu apitishie mbali.
mwisho



No comments:

Post a Comment