KIJANA mmoja Athuman Peter kwa jina
maarufu mzee wa Genya (26), mkazi wa mtaa wa Nyamakokoto, mjini Bunda, mkoani
Mara, aliyemnyang'anya sh. laki moja na simu moja ya mkononi mama yake mzazi
kwa kutumia silaha, amehukumiwa na mahakama ya wilaya ya Bunda, kutumikia
kifungo cha miaka 30 jela.
Hukumu hiyo imetolewa jana na hakimu mkazi
mfawidhi wa wilaya ya Bunda Said Hamad Kasonso, baada ya kuridhika na ushahidi
uliotolewa mahakani hapo na upande wa mashitaka.
Awali ilidaiwa mahakamani hapo na
mwendesha mashitaka wa polisi, Masoud Mohamed kuwa mshitakiwa huyo alitenda
kosa hilo mnamo novemba 18 mwaka jana majira ya saa 1:30 jioni, katika mtaa wa
Nyamakokoto, mjini Bunda.
Mohamed alisema kuwa siku ya tukio
mshitakiwa huyo alimvamia mama yake mzazi aitwaye Pendo Mgasa, aliyekuwa
nyumbani kwake na kumnyang'anya fedha tasilimu sh. laki moja, pamoja na simu
moja ya mkononi aina ya Nokia yenye thamani ya sh. 20,000.
Alisema kuwa katika kufanya unyang'anyi
huo mshitakiwa huyo alitumia panga alilokuwa nalo, akimtishia kumuua mama yake
mzazi kwamba iwapo akikatalia fedha hizo au kufanya lolote atamutoa uhai wake
kwa kumkata na panga hilo.
Akitoa hukumu hiyo hakimu Kasonso alisema
kuwa ameridhika pasipo kuacha shaka yoyote juu ya ushahidi uliotolewa na upande
wa mashitaka na kwamba kwa jinsi hiyo anamtia hatihani mshitakiwa huyo
kutumikia adhabu ya kifungo cha miaka 30 jela.
Alisema kuwa kitendo alichokifanya
mshitakiwa huyo ni cha kinyama hasa kwa kumfanyia mama yake mzazi na kuongeza
kuwa adhabu hiyo itakuwa fundisho kwake na kwa watu wengine wenye tabia kama
hiyo ya kutaka kujipatia fedha na mali kwa njia za unyang'anyi.
Hata hivyo mshitakiwa huyo alipotakiwa
kujitetea alishindwa kufanya hivyo na badala yake alibaki kimya bila kusema
lolote.
Mwisho
No comments:
Post a Comment