Social Icons

NDOA YANGU, Ningejua!

NDOA YANGU, Ningejua!

Kikwete aikoroga CCM


SIKU moja baada ya Rais Jakaya Kikwete kuridhia hoja za wapinzani na kutaka muswada wa sheria ya marekebisho ya sheria ya mabadiliko ya katiba urejeshwe bungeni, Chama cha Mapinduzi(CCM) kimetaharuki huku viongozi wake wakiwa na kauli tofauti kuhusu uamuzi huo.
Wakati Mbunge wa Ludewa, Deo Filikunjombe (CCM) akimpongeza Rais kwa hatua hiyo,na kumtahadharisha awe makini na wabunge wa chama hicho akidai wamekuwa wakitumia uwingi wao vibaya bungeni, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu),  Stephen Wassira amegoma kuzungumzia hatua hiyo akimsukumia mpira Waziri mwenzake.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti jana, viongozi hao walikuwa na mawazo ya kusigana ambapo baadhi walimuunga mkono Rais Kikwete na wengine wakionyesha kutokubaliana na uamuzi huo.
Kwa mtazamo wake, Filikunjombe alisema Kikwete ameonyesha ukomavu, na ndio Demokrasia ya kuwasikiliza wachache pia, kwenye Katiba hakuna mshindi, muswada uliopitishwa sio wa CCM, Katiba sio ya CCM inapaswa kuwa ya wananchi wote hata wachache wasikilizwe, katika hili hakuna mshindi, ushindani unakuwepo kati ya nani na nani wakati katiba ni ya watanzania wote.
“Katiba mpya haikuwa ajenda ya CCM, Rais aliichukua labda kutoka Chama kiingine akaona inafaa, CCM wamepokea suala la mabadiliko ya Katiba bila kukubali maumivu yake ndio maana tunafikia hatua hii, ni sawa na mtu unataka kufika mbinguni halafu hutaki kufa, tukubali mabadiliko na maumivu yake”. Alisema Filikunjombe.
Aliongeza kwamba “mimi ninamtia moyo Rais Kikwete asimamie vizuri suala la Katiba, ila ajue wabunge wengi wa Chama cha Mapinduzi tunamharibia, awe makini na sisi wabunge wa CCM, kwani mara nyingi tunatumia wingi wetu vibaya, na imekuwa aibu sasa mara ya pili Rais anarejesha muswada kufanyiwa marekebisho, ingefaa wabunge wa CCM tujitafakari sisi tunamtumikia nani? Kwenye hili Kikwete ameonyesha amedhamiria kwa dhati kuusimamia mchakato tumuunge mkono .”
Aidha akizungumzia kauli za Mawaziri waliotoa kauli za kejeli, kusema hakuna muda wa mazungumzo na wapinzani, au wapinzani wanaenda Ikulu kutafuta Juice, Filikunjombe alisema
“Hao wana akili mgando tu, yafaa waombe radhi watanzania, na hii ni kwa sababu hapa kwetu utamaduni wa kujiuzulu haupo, lakini vinginevyo hizo sio kauli za kusemwa na Mawaziri.”.
Kwa upande wake Wassira alipotafutwa aliomba aulizwe Chikawe katika maana kwamba yeye hakuwa na la kusema {On that sina Comment, mtafute Chikawe}
Hata hivyo Naibu Spika wa Bunge alionyesha kushangaa katika maana kuwa hajui wapinzani wanabishania nini na walienda kumuona Rais kwa suala lipi?
Alisema “Ni ishu gani hasa ambayo inahitaji udharura wa aina hiyo, unaposema watalirejesha bunge lijalo je Kanuni zinaruhusu? Mimi sioni mantiki yoyote, labda wanaozungumza hoja ya uteuzi wa wajumbe 166,kama Rais hataki hilo ni suala jingine ila sisi tuliona Rais ndio chombo kinachofaa kuchuja wajumbe hao, bila mamlaka ya kuchuja tunaweza kujikuta kuwa na wajumbe au wakatoka kanda moja wote, au dini moja wote au wa jinsia moja, hivyo mamlaka ya kuchuja inahitajika”.  
Kuhusu muswada kurejeshwa bungeni Ndugai alisema , hana uhakika kama utarejeshwa ila anachofurahi yeye ni kusikia kuwa muswada umesainiwa
Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mpinduzi, na Mbunge wa Donge, Sadifa Khamisi alisema “Bunge ni chombo huru, tutaangalia kama kuna masuala ya kubadili, na yanaposhindikana tutapiga kura na wingi wa kura ndio utakaoamua, alipoulizwa pengine wingi huo unaweza kutumika vibaya alisema “Wewe kama una mawazo yako unayotaka kaandike sisi tunamuunga Rais mkono ingawa bungeni huko nako masuala ni tofauti”.
Kauli ya Chama cha Mapinduzi kupitia msemaji wake, Nape Nnauye Kikwete kwa kusaini kama tulivyosikia inaonyesha anafuata sheria, lakini pia tunampongeza kwa kukutana na Wapinzani ameonyesha ukomavu, yale yatakayorejeshwa bungeni wabunge wataamua kama wakiona yana hoja wasikilize wakiona hayana hoja watajua wao, bunge ni muhimili huru”. Aidha kuhusu kejeli za Mawaziri walizotoa kwamba hakutakuwa na nafasi ya wapinzani kuzungumza na Rais, Nape alisema hajui na hajawahi kusikia, lakini pia kabla ya mwandishi kuhoji hilo ahoji kwanini wapinzani wameenda Ikulu wakati wanajua muswada umesainiwa na walisema Rais akisaini hawatakubali kuonana naye.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Alexanda Makulilo kwa upande wake alisema “Rais ametumia busara kuwasikiliza wapinzani, aliona wana hoja ndio maana akawasikiliza na kuomba marekebisho yafanyike, wabunge sasa wakafanye majadiliano vizuri, waone umuhimu wa hoja, waweke maslahi ya vyama pembeni, waangalie maslahi mapana ya katiba kwa manufaa ya nchi, maana wasipokuwa makini utakuta wanajadili ili wale waliotawala wabaki na wale ambao hawajatawala wanatengeneza mbinu za kutaka kuingia hayo si maslahi mapana ya Katiba”.
MWISHO.

No comments:

Post a Comment