Social Icons

NDOA YANGU, Ningejua!

NDOA YANGU, Ningejua!

NANI ANAJALI, TAIFA LIKIENDA GIZANI?


Nani anajali, taifa likienda gizani?
“Pole Bwana Misango kwa kufungiwa kwa kikaratasi chenu cha udaku (yaani gazeti hili) kinachomilikiwa na  chama cha wachaga (Chadema).
“Itabidi sasa kwa hiyo miezi mitatu, mjifunze adabu na kuiheshimu  serikali, maana ninyi ni wa …(tusi) sana, ,mnastahili kukomeshwa na ningekuwa mimi ndio JK (Rais Jakaya Kikwete) nisingewafungulia hadi namaliza urais wangu’.
Haya ni maneno ya msomaji wangu mmoja aliyenipigia simu mwanzoni mwa wiki hii, mara tu baada ya tangazo la serikali la kuyafungia magazeti mawili maarufu ya Mwananchi na Mtanzania.
Nilicheka kwa uchungu, kwa sababu masikini mtanzania huyu amesukumwa na ushabiki wa kisiasa kiasi cha kushindwa kujua kuwa gazeti la Tanzania Daima ni mali ya nani. Anaamini kwa sababu linaandika habari nyingi za Chadema, basi ni mali ya chama hicho!
Kwamba pamoja na kuwa bingwa wa kuzodoa wengine na kutoa maneno  ya hario, amekosa kabisa kujua kuwa Mtanzania na Tanzania Daima ni magazeti mawili tofauti kabisa na yenye sera na wamiliki wawili tofauti pia!
Ujumbe wa msomaji huyu, unatokana na hatua ya serikali ya  kufungia magazeti mawili ya Mwananchi na Mtanzania kwa tuhuma za uchochezi na kuhatarisha amani. 
Najua yamesemwa mengi kutoka kwa watu wengi, wakilaani na kulalamikia hatua hii ya serikali. Kwa wengine, wanaweza kudai kuwa kwa sababu watu wamepiga kelele kiasi cha kutosha,  hakuna haja ya kuendeleza malumbano. Sio kweli.
Tuanze na tamko la kufungia gazeti la Mwananchi. Kwa hili, watawala wetu wametuambia kuwa wamelifungia kwa siku hizo 14 kwa sababu liliandika habari za uchochezi na uhasama kwa nia ya kusababisha wananchi  wakose imani kwa vyombo vya dola hivyo kuhatarisha amani na mshikamano ulipo  nchini.
Watawala wametamka kuwa gazeti hili, lilichapisha habari zenye mwelekeo wa uchochezi na uvunjifu wa amani, kwa kuchapisha habari  ya SIRI ‘  juu ya MISHAHARA MIPYA SERIKALINI 2013”. Kisha likachapa habari  nyingine iliyosema “WAISLAM WASALI CHINI YA ULINZI MKALI” , na kukolezwa na picha ya mbwa  mkali mwenye hasira, iliyotoa  tafsiri ya kuwa Jeshi la Polisi lilipeleka Mbwa katika maeneo ya ibada ya waumini wa dini ya kiislam jambo ambalo halikuwa la  ukweli na ni uchochezi wa kulichonganisha Jeshi la Polisi na waumini wa dini ya iislam  maana mbwa ni najisi hapaswi kuingia  katika maeneo ya ibada.
Kwa gazeti la MTANZANIA lililofungiwa kwa siku tisini(90), linadaiwa kuandika  habari  yenye kichwa kisemacho “URAIS WA DAMU”, na tena  lilichapisha makala isemayo “MAPINDUZI HAYAEPUKIKI”. Likaibuka tena na Kichwa cha habari kisemacho “SERIKALI YANUKA  DAMU” taarifa hiyo ilikolezwa na picha zilizo unganishwa kwa ustadi mkubwa kwa kutumia kompyuta  kutapakaza rangi nyekundu mithili ya damu nyingi kumwagika .Katika habari hiyo gazeti hilo limedai bila uthibitisho kuwa Jeshi la Polisi linahusika  na wahanga waliomizwa na watu wasiojulikana kwa kumwagiwa tindikali na  waliyovamiwa na kujeruhiwa vibaya.
Mbaya zaidi gazeti hilo liishtumu serikali kuwa goigoi katika kushughulikia matukio yenye sura ya kigaidi. Hayo, serikali imesema ni uchochezi  wenye lengo la kuwafanya wananchi wavichukie vyombo vya ulinzi na usalama  wavione kuwa haviwasaidii.
Taarifa ya serikali, ikawataka wamiliki,wahariri na wanahabari kwa ujumla kuwa makini,kuzingatia weledi,miiko, madili yataaluma uandishi wa habari na kuweka mbele maslahi ya taifa letu kwa kuwa na uzalendo wa hali ya juu.
Kufungiwa kwa magazeti haya ni ishara mbaya ya giza nene linalolinyemelea taifa. Ni kuzima mshumaa wa matumaini, na uhuru wa watanzania kwa namna nyingi. Kwa watu wanaojali uhai wa taifa, kufungia magazeti ni kuua uhai wa taifa. Ikumbukwe kuwa wakati haya yakifungiwa, serikali yetu sikivu, iliapa kutolifungulia  gazeti la Mwanahalisi kwa kosa lile lile la kuandika habari za uchochezi.
Kosa la mwanahalisi, ni kuanika kweupe mlolongo mzima wa mawasiliano ya kutekwa na kuumizwa vibaya kwa  kiongozi wa madaktari nchini, Dk Stephen Ulimboka na watu anaodai kuhusika na tukio hilo baya. Kwa serikali badala ya kufuatilia ikaamua kulinyamazisha!
Najua wapo watanzania na hasa watawala wababaishaji, wanaotumia nafasi zao kujineemesha, bila kujali maslahi ya mwananchi, wameshangilia! Hawajali kinachoweza kutokea, ama nini kitakachoingia vichwani kwa watu wengi kutokana na hatua hii. Hawajali ya kesho. Nani anajali?
Hawajali kwamba hata ukifungia gazeti, kuna teknolojia nyingine nyingi za kupashana habari. Kuna mitandano mingi ya mawasiliano inayoweza kutumika kutuma ujumbe kwa kasi mno. Inasikitisha kwamba  waliofungia magazeti  haya hawajali kuwa, tofauti na gazeti linalochapa nakala chache tu na kusambazwa kwa shida kubwa sehemu chache tu za nchi, mitandano ya jamii na mawasiliano mengine ni  ya hatari zaidi kwa sababu, mtu yeyote anaweza kusambaza habari za uongo, uzushi, uchochezi na kusababisha vurugu kubwa ndani ya kipindi kifupi na kwa eneo kubwa!
Ni hatari kwa taifa lililonyimwa mawasiliano, kwa sababu anaweza kuibuka ‘kichaa’ mmoja akatumbukiza ujumbe mchafu na kuchochea vurugu za kidini ama kikabila na ukaendea kama moto wa nyasi kavu msituni!
Ni giza nene kwa taifa, linalotaka nchi itawaliwe bila watu walioombwa kwa unyenyekevu katika kampeni kuwachagua watu fulani watawale, na ghafla wanakuwa mbogo kuhojiwa pale yanapokuja mashaka na mambo yasiyopenmdeza.
Andiko la mtu mmoja katika moja ya mitandao ya kijamii, inaonesha sura na haiba ya aina hii ya watawala. Andiko hilo linasema; (nanukuu) “ Haiwezekani gazeti liandike "Mapinduzi hayaepukiki" halafu liachwe bila hatua. Huo utakuwa ulevi wa uhuru wa maoni ambayo haitofautiani sana na
ya madaraka. Rwanda waliuana kwa uchochezi wa magazeti na redio!
Nakubali kwamba mauaji ya Rwanda yalichangia umwagaji damu. Nakubali kuwa hakuna uhuru usio na mipaka, na demokrasi bila utaratibu ni fujo.
Kama watu tunaojali taifa letu, na tunaosukumwa vema na moyo wa ukweli, tusiopenda kujipendekeza kwa yeyote, tudurusu kidogo tu hoja za serikali zilizosababisha kivangaito katika tasnia ya habari na taifa. Tunafanya hivi kwa sababu tunaijali nchi yetu na kamwe hatutaki  taifa liende kwa mtindo wa kufafaruka!
Hivi ni watanzania wangapi wana imani na utendaji kazi wa baadhi ya askari wa jeshi la polisi? Tuhuma ngapi zimesukumwa kwa jeshi hili na ni hatua ngapi zimechukuliwa dhidi ya wanaotuhumiwa ili liwe safi na kudumisha imani inayopiganiwa usiku na mchana?
Raia wangapi wameteswa na kufia mikononi mwa polisi? Mwandishi Daud Mwangosi alipigwa vibaya na kuuawa kikatili mikononi mwa nani? Nani alimwaga damu ya Mwangosi? Nani alimwaga damu ya wafanyabiashara wa Morogoro  waliosingizwa ujambazi? Nani alimpiga risasi Mwandishi Shaaban Matutu wa Tanzania Daima?
Plisi wamemkamata nani mateso ya Mhariri Kibanda, kuuawa kwa Padri huko Zanzibar?  Hivi walioumizwa wakihoji utendaji huu, ama mtu kuihoji serikali yako kuhusiana na usalama wako, ni uchochezi? Kumbe, watoe pongezi kwa dola inayoshindwa kuwakamata watu walioua, kumwagia watu tindikali na kuhatarisha usalama wa raia?
Hivi anayehoji uhakika wa maisha yake, na anayepuuza kufuatilia matukio haya mabaya kwa kuwaondoa watendaji wote wanaolichafua jeshi la polisi na vyombo vingine vya dola, nani anastahili kuitwa mchochezi?  nani anastahili kutimuliwa kati ya wale wanaondika, na mtendaji goigoi anayeshindwa kutimiza wajibu wake na hivyo kufanya serikali ichukiwe na wananchi?  Hivi serikali haikuwa na washauri wazuri katika hili? Hawakujali matokeo ya hatua hii?
Serikali inapotaka waandishi kuwa wazalendo, wafanye hivyo mara ngapi? Tumeandika na kuanika madudu na uozo kiasi gani? Nani kachukuliwa hatua, nani kakamatwa? Badala ya shukrani, tumetendewa mangapi, tumetishwa mara ngapi? Maisha ya waandishi yamekuwa ya wasiwasi kwa sababu tu tunahatarisha maslahi ya wachache kwa kiwango kikubwa. Nani amejali?


No comments:

Post a Comment