MAHAKAMA ya Wilaya ya Ukerewe mkoani Mwanza,
imemwamuru kwenda gerezani siku 14 Mbunge wa Ukerewe, Salvatori Machemli
(CHADEMA), kwa kosa la kudharau mahakama.
Machemli ambaye anakabiliwa na kesi ya uchochezi,
aliamriwa kwenda gerezani jana baada ya kushindwa kuhudhuria mahakamani
kusikiliza kesi yake.
Taarifa zilizoifikia Tanzania Daima kutoka
mahakamani hapo, zilisema kuwa katika kesi hiyo, Machemli anadaiwa kutumia
maneno ya uchochezi katika mikutano mbalimbali ya hadhara wilayani humo
mwaka jana, na kwamba amekuwa akienda nje ya wilaya hiyo na hata nje ya
nchi bila idhini ya mahakama.
Inadaiwa kwamba, Machemli alipofika mahakamani
hapo jana kwa lengo la kuhudhuria kesi yake hiyo, alifutiwa dhamana kisha
kuamriwa kuwekwa ndani.
“Ni kweli mahakama imetoa amri ya kuwekwa ndani
mheshimiwa Machemli kwa kosa la kudharau mahakama. Alikuwa hahudhurii
tarehe za kesi yake, kutokana na hali hiyo, leo alipokuja mahakamani
kuhudhuria kesi yake aliondolewa dhamana kisha akaswekwa ndani,” kilisema
chanzo chetu.
Ilidaiwa kwamba, hakimu anayesikiliza kesi hiyo
alimtaka Machemli kuwasilisha wadhamini wawili wapya wanaomiliki hati ya
nyumba, ambao walipatikana, lakini hakimu akabaki na uamuzi wake wa kutaka
mbunge huyo aende gerezani kwa siku hizo 14.
Akizungumza na Tanzania Daima kwa simu, Machemli
alithibitisha kuondolewa dhamana kisha kuwekwa ndani kwa kosa la kudharau
mahakama.
“Ni kweli wameniweka ndani. Ninapozungumza na wewe
hapa nipo mahakamani nasubiri wanipeleke ndani…daah haya ni majanga!
Nilikuwa nahudhuria vikao vya Bunge huku mahakamani sikuweza kufika.
“Lakini nilikuwa natuma watu wawili kuniombea
ruhusa, sasa yawezekana pengine hawakuwa wanakwenda ndiyo maana nimewekwa
ndani,” alisema Machemli.
|
No comments:
Post a Comment