SIKU moja baada ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya
Ufundi kufanya marekebisho katika upangaji wa viwango vya alama za matokeo ya
wanafunzi wa kidato cha nne na sita kwa kufutwa daraja sifuri na kuwekwa
daraja la tano, wadau na wasomi wameponda mfumo huo.
Wakizungumza na gazeti hili, wadau hao walisema kuwa
tatizo si kushuka kwa kiwango cha ufaulu, bali uwepo wa elimu bora nchini.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM),
Bashiru Ally, alisema kuna mifumo miwili ya elimu nchini inayotumika, ambayo
ni ule wa watu masikini na wenye nafuu ya maisha.
Alisema hali hiyo inaanzia chekechea hadi vyuo
vikuu, huku akihoji wizara husika mfumo wa aina hiyo unamlenga nani, kwamba
tatizo lililopo ni ubora wa elimu hasa katika shule za umma.
Bashiru alisema kwenye mifumo hiyo inayotumika, ule
wa masikini upo kwenye shule nyingi za umma ambako ndiko kwenye watoto wengi
wanaofeli kutokana na kukosa vifaa vya kufundishia, maabara na walimu.
“Katika shule za umma watoto wengi hawasomi, hawana
maabara, sasa wizara inawatahini nini? Mageuzi yoyote ambayo yatashindwa
kuondoa matabaka hayawezi kuleta elimu tunayoitaka,” alisema.
Alisema ubora wa elimu utawahusu wanafunzi hao
wanaosoma shule za michepuo ya Kiingereza, kwani ndio watakaokuwa wanafaulu
kwa kuwa shule zao zina mfumo mzuri unaoeleweka na viwango walivyojiwekea
kama mwanafunzi hatafikia atarudia darasa ama kuachishwa shule.
Naye mhadhiri mwingine wa chuo hicho, Prof. Herme
Mosha, alisema kama wizara inataka kuongeza idadi ya watu katika ufaulu
waliofanya mtihani, inapaswa kuboresha elimu.
“Sio mara ya kwanza tumechezea vigezo, 2007
tulibadilisha viwango tulivyokuwa navyo tukaweka alama za chini, wanafunzi
wengi wakachaguliwa, matokeo yake mtihani wa mwisho wa kidato cha nne kukawa
na matokeo mabaya,” alisema.
Alisema lililofanyika sio utatuzi wa tatizo, bali
wizara iangalie nini kinasababisha ubora wa elimu kushuka.
Kwa mujibu wa Prof. Mosha, wizara husika iangalie ni
nini kinachowafanya wanafunzi wasisome badala ya kupandisha viwango kwa aina
hiyo waliyoitumia.
Dk. Kitila Mkumbo wa Chuo Kikuu kishiriki cha Elimu
cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alisema tatizo lililopo ni mfumo mbaya wa
ufundishaji, kwani kupanga madaraja kwa aina hiyo si suluhu ya kutatua
changamoto iliyopo.
Alisisitiza kuwa kwa staili hiyo, serikali haitoi
tatizo bali inajaribu kuficha tatizo, hivyo hakuna cha kushangilia kwa mfumo
huo walioutangaza.
Mwalimu wa sekondari, Josephat Ammy, alieleza kuwa
mfumo huo utamfanya mwanafunzi kubweteka na kutochukulia umuhimu suala la
elimu kwa kudhani kuwa uwezo wa kufaulu anao.
“Wao walitakiwa waje na suluhisho la elimu na kujua
kwanini wanafunzi wanafeli, sasa wanachofanya nini? Wanaondoa daraja ziro
halafu hao wa daraja la tano wanakwenda wapi?” alihoji.
Naye mmiliki wa shule za Green Acres, Julian Bujugo,
alisema kuwa mfumo huo sio mbaya kwani wanafunzi watafanya mtihani kwa
kutumia mitaala.
“Mfumo huu ulikuwepo hapo awali kabla ya kutolewa,
sioni kama una ubaya. Ni mzuri, utasaidia kwa wanafunzi tofauti na mwaka jana
walitunga mitihani ambayo haikuwa kwenye mitaala,” alisema.
Naye Rais wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT),
Gracian Mukoba, alisema kuwa kubadilisha alama itakayowasaidia watoto wengi
kuonekana wamefaulu haisaidii kwani ndiyo kwanza kunaongeza zao la ujinga.
Alisema kama walikuwa wanatafuta kufurahiwa na
wazazi na wanafunzi, basi wangeweka alama A, B, C plus bila kuwa na alama
hizo za daraja hadi la tano.
Kwa mujibu wa Mkoba, kilichofanyika ni siasa tu na
kucheza na saikolojia za wazazi, ambazo tayari zimeathiriwa na mfumo mbaya wa
elimu ambapo idadi kubwa ya watoto wanaofeli inaongezeka kila kukicha.
“Yaani hapa ni kama bomba, unakuta linatoa maji
machafu ya tope. Baada ya kuangalia nini chanzo chake wewe unaamua
kubadilisha koki na kuweka nyingine wakati si suluhisho,” alisema.
Mukoba alisema njia sahihi za kuboresha elimu
serikali inazijua kwa kuwa tayari walishatumia fedha nyingi kwa ajili ya
kuunda tume, kufanya utafiti, hivyo majibu tayari wanayo.
Naye mwalimu wa vituo vya elimu ya Taasisi ya Watu
Wazima, Stanslaus Sekuru, alisema kuwa mfumo huo utaboresha elimu kwa sababu
hapo awali wanafunzi walikuwa wakiumia sana.
Alitolea mfano daraja la nne akisema mwanafunzi anakuwa
na alama 26, lakini akiwa na alama C tatu anashindwa kuendelea na kidato cha
tano na mwenye daraja la tatu mwenye alama 25 na C tatu yeye anapewa nafasi
ya kuendelea.
Mwalimu Charles Mkwidu ambaye ni mratibu wa Kituo
cha Elimu ya Watu Wazima, alisema mpango huo ni mzuri ila uwekewe mkakati wa
kuwasaidia wanafunzi kupenda kusoma, hasa masomo ya sayansi kwani wengi
husoma wakati wa mitihani tu.
Naye mwanafunzi anayerudia mitihani, aliyeathiriwa
na matokeo ya mwaka jana, Jesca Charles, alisema huenda ikawasaidia au la kwa
kuwa mitaala ya elimu ndiyo iliyowaponza hadi wakafeli
|
NDOA YANGU, Ningejua!
SERIKALI YAPINGWA ALAMA ZA MITIHANI
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment