LICHA ya serikali kutamba kuwa itawakamata
watuhumiwa wa shambulio la bomu katika mkutano wa CHADEMA eneo la Soweto
jijini Arusha, sakata hilo limegeuka kuwa siri ya Jeshi la Polisi kutokana na
hali ya sintofahamu inayoendelea kutawala.
Tukio hilo lilitokea Juni 15, mwaka huu, na sasa ni
zaidi ya miezi minne tangu kuuawa kwa wafuasi watatu wa CHADEMA, huku wengine
wengi wakiachwa majeruhi, lakini hadi leo hakuna taarifa kama kuna mtuhumiwa
aliyekamatwa.
Awali, tukio hilo ambalo nusura limuue Mwenyekiti wa
CHADEMA, Freeman Mbowe, aliyekuwa akihitimisha mkutano wa kampeni za uchaguzi
mdogo wa madiwani, lilipotoshwa kisiasa ili kujenga taswira kwa umma kuwa
chama hicho kililipanga chenyewe.
Tangu wakati huo, Jeshi la Polisi na viongozi wa
serikali mkoani Arusha wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa, Magesa Mulongo, wamekuwa
na kauli za kukinzana kuhusu wahusika wa tukio hilo.
Hivi karibuni, Mulongo alikaririwa akisema kuwa
watuhumiwa wametiwa mbaroni na kwamba watatangazwa wakati wowote na vyombo
vya dola, lakini Kamanda wa Polisi Mkoa, Liberatus Sabas, alipohojiwa
alionekana kumshangaa kiongozi huyo.
Alipotafutwa juzi, msemaji wa jeshi hilo makao
makuu, Advera Senso, naye alimtupia mzigo huo Kamanda wa Arusha akisema
aulizwe yeye.
Tanzania Daima Jumamosi liliwasiliana na Sabas,
lakini akasema atatoa taarifa hiyo muda ukifika bila kufafanua ni lini au
kama watuhumiwa wamekamatwa.
Itakumbukwa kuwa siku moja baada ya mlipuko huo,
serikali kupitia Waziri wa Nchi, Ofisi wa Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na
Bunge), William Lukuvi, ilitoa taarifa bungeni ikilenga kulikingia kifua
Jeshi la Polisi na kuibebesha lawama CHADEMA.
Katika tamko hilo, Lukuvi alisema uchunguzi wa awali
unaonyesha kuwa mlipuko huo ulikuwa wa bomu la kurushwa kwa mkono, na kwamba
aina ya urushaji wake haitofautiani na mbinu iliyotumika katika shambulio la
Mei 5, mwaka huu, katika Kanisa la Olasiti jijini Arusha.
Alisema kuwa zimekuwepo jitihada za makusudi za
baadhi ya vyama vya siasa, makundi ya kijamii na watu binafsi kupandikiza
chuki kwa raia dhidi ya Jeshi la Polisi.
Kwa mujibu wa Lukuvi, mlipuko huo ulikuwa wa bomu la
kurushwa kwa mkono, na kwamba lilirushwa kutoka upande wa mashariki kuelekea
magharibi kulikokuwa na gari aina ya Fuso lililokuwa linatumika kuhutubia.
Alidai kuwa polisi walimuona mlipuaji, lakini katika
harakati za kumkamata, wafuasi wa CHADEMA waliwashambulia kwa mawe na hivyo
mtuhumiwa akatokomea.
Kwa mbwembwe, Lukuvi alisema serikali itatoa zawadi
ya sh milioni 100 kwa wale watakaowezesha kukamatwa kwa watuhumiwa wa
milipuko hiyo.
Hata hivyo, taarifa ya Lukuvi iliota mbawa na kuzua
mkanganyiko baada ya Mbowe kutangaza kuwa wanao mkanda wa video unaowaonyesha
polisi kuwa wahusika wa shambulizi hilo.
Katika mkutano wake na waandishi, Mbowe alisema
tukio hilo lilikuwa ni la kupangwa na waligundua risasi za bunduki aina ya
SMG na bastola zilitumika mara baada ya mlipuko huo jambo lililozusha hofu.
Alilitaka Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi na
kuwakamata watuhumiwa huku akiapa kwamba video hiyo hawataikabidhi kutokana
na kutokuwa na imani na jeshi hilo, vinginevyo iundwe tume huru ya uchunguzi
ya kimahakama.
Baada ya polisi kushindwa kuwakamata watuhumiwa
ambao Waziri Lukuvi alilieleza Bunge kuwa waliwaona, lilimgeukia Mbowe na
kuanza kumshinikiza asalimishe video hiyo, kwa vitisho kwamba atachukuliwa
hatua asipotii amri.
Katika kutapatapa, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mulongo,
alisema kuwa serikali imegundua mtandao wa milipuko ya mabomu yaliyotokea
katika Kanisa la Olasiti na Uwanja wa Soweto kwenye mkutano wa CHADEMA.
Alitamba kuwa serikali itachukua hatua stahiki kwa
wahusika hao bila kujali cheo, umaarufu au nafasi ya kisiasa.
Mulongo alithibitisha kuwa tayari kuna askari wa
upelelezi wa FBI walishakuja Arusha wakishirikiana na wataalamu wa milipuko
toka Kenya, jambo ambalo lilikanushwa na Ubalozi wa Marekani nchini.
Mbali ya Mbowe, viongozi wengine mbalimbali
waandamizi wa chama hicho, akiwamo Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema
(CHADEMA) walinusurika katika mlipuko huo wa bomu.
|
NDOA YANGU, Ningejua!
WALIOLIPUA BOMU ARUSHA WATOWEKA
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment